T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Tue, 21 Jul 2026 23:55:32

Walimu wakataa nyongeza ya Sh8.4 bilioni, wasema nyongeza nzima inamezwa na ushuru

WALIMU nchini wamekataa nyongeza ya mishahara ya awamu ya pili ya Mkataba wa Pamoja wa Ajira (CBA) wa miaka ya 2025–2029, wakisema ni ndogo mno wala haiendani na gharama ya maisha inayozidi kupanda. Malalamishi hayo yameibuka baada ya Tume ya Kuajiri Walimu (TSC) kutoa barua inaoyoelekeza utekelezaji wa awamu ya pili ya mkataba huo kuanzia Julai 1, 2026. Walimu wengi waligundua kuwa nyongeza yao halisi ni kati ya Sh693 na Sh2,055 pekee kulingana na cheo na kiwango cha mshahara. Ingawa serikali ilitenga Sh8.4 bilioni kutekeleza awamu hiyo, walimu wanasema kiasi kinachoingia katika akaunti zao baada ya makato ya kisheria hakina tofauti kubwa na mshahara wa awali. "Mwalimu wa daraja ya C3 alitarajiwa kuongezewa Sh2,055, lakini hiyo ni kabla ya makato ya PAYE, SHA, Ushuru wa Nyumba na NSSF. Kinachobaki ni kidogo sana na hakiwezi hata kusaidia kulipa mkopo wa SACCO," alisema mwalimu mmoja wa Nairobi. Mkataba huo wa miaka minne una thamani ya Sh33.75 bilioni, ukihusisha nyongeza ya mishahara na masuala ya ustawi wa walimu. Hata hivyo, walimu wengi sasa wanasema matarajio yaliyotolewa na vyama vyao hayalingani na hali halisi. Katibu wa KUPPET tawi la Vihiga, Sabala Inyeni, alisema nyongeza hiyo haijazingatia mfumuko wa bei wala kupanda kwa gharama za usafiri. "Marupurupu ya usafiri hayajabadilishwa kwa zaidi ya miaka 15 ilhali bei ya mafuta imeendelea kupanda. Ongezeko hili haliendani na hali halisi ya maisha," alisema. Walimu wanaofanya kazi katika maeneo magumu na kame pia wameeleza kutoridhishwa kwao baada ya marupurupu ya mazingira magumu kukosa kuongezwa. Katibu wa chama cha walimu wanaohudumu katika maeneo hayo Ndung'u Wangenye, alisema baadhi ya walimu wameongezewa chini ya Sh500 huku wakifanya kazi katika mazingira magumu. "Walimu wa maeneo kame wanahisi wamesalitiwa. Marupurupu ya mazingira magumu ndiyo yanayowatia moyo kuendelea kufanya kazi huko, lakini hayajaguswa kabisa," alisema. Naibu Katibu Mkuu wa KUPPET Moses Nthurima, alisema walimu wengi hawajaridhishwa na matokeo ya mazungumzo ya CBA. "Serikali imechukua fedha nyingi kupitia makato ya SHA, ushuru wa nyumba, NSSF na kodi kuliko ilivyorejesha kupitia nyongeza ya mishahara. Ndiyo maana walimu hawaoni faida ya ongezeko hili," alisema.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Tue, 21 Jul 2026 22:55:39

Serikali yakubali ukosoaji wa ufadhili elimu ya juu; yaweka mpango wa 'kufaidi wote'

WANAFUNZI wote watakaofuzu kujiunga na vyuo vikuu nchini watapata ufadhili kamili wa masomo kutoka kwa serikali iwapo pendekezo jipya la ufadhili wa elimu ya juu litapitishwa na Bunge. Rais William Ruto alitangaza hatua hiyo Jumanne katika Ikulu, akisema serikali imewasilisha mapendekezo ya marekebisho ya sheria yatakayowezesha kila mwanafunzi anayefaulu mtihani wa kitaifa na kupata nafasi katika chuo kikuu au taasisi ya elimu ya juu kufadhiliwa kikamilifu bila kujali hali ya kifedha ya wazazi wake. "Kwa sasa tuna pendekezo bungeni litakalowezesha elimu ya juu kuwa ya wote. Haitajali mtoto anatoka katika familia gani, bali uwezo wake kitaaluma. Mwanafunzi yeyote anayefaulu na kupata nafasi chuoni atapata ufadhili kamili," alisema Rais Ruto. Aliwahimiza wabunge kuharakisha kupitisha marekebisho ya sheria ya Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu (HELB) ili wanafunzi watakaoanza masomo Septemba mwaka huu wanufaike kwa mfumo huo mpya. Tangazo hilo linaashiria kuwa serikali inaweza kuachana na mfumo wa sasa wa ufadhili wa elimu ya juu ulioanzishwa mwaka wa 2023 ambao umekoselewa na wanafunzi, wazazi na wadau wa elimu. Rais alisema mfumo wa awali haukufaulu kwani ulisababisha vyuo vikuu vingi kukumbwa na matatizo ya kifedha baada ya serikali kushindwa kutoa kiwango cha fedha ilichoahidi. "Baadaye tukaanzisha mfumo wa usawa ambapo wazazi walichangia sehemu ya karo, serikali ikatoa sehemu kupitia ufadhili na sehemu nyingine kupitia mkopo. Tulidhani ungeleta usawa lakini umeonekana kutotosha," alisema. Aliongeza kuwa chini ya mfumo mpya, wazazi watakuwa na hiari ya kuchangia karo za watoto wao, lakini iwapo hawataweza kufanya hivyo, serikali itagharimia masomo yote. "Hatutaki mwanafunzi yeyote ashindwe kuendelea na masomo kwa sababu ya ukosefu wa fedha," alisema Rais. Hata hivyo, maelezo ya kina kuhusu mfumo huo bado hayajatolewa. Katibu wa Elimu ya Juu, Dkt Beatrice Inyangala, alisema pendekezo hilo bado linashughulikiwa kabla ya kuwasilishwa rasmi kwa wadau na Bunge. "Bado tunalifafanua na kulikamilisha. Ni mchakato unaohitaji muda," alisema. Mwenyekiti wa Kamati ya Makamu Wakuu wa Vyuo Vikuu vya Umma, Prof Daniel Mugendi, pia alisema bado hajapokea maelezo kamili ya mfumo huo. "Hatujapata maelezo ya kina. Yakikamilika tutashirikishwa kwa majadiliano zaidi," alisema. Changamoto ya ufadhili wa elimu ya juu imekuwa ikisumbua serikali kwa miaka kadhaa. Madeni ya vyuo vikuu vya umma yameongezeka kutoka takriban Sh60 bilioni mwaka wa 2022 hadi zaidi ya Sh85 bilioni sasa. Wakati huo huo, Mkurugenzi Mkuu wa HELB Geoffrey Monari amependekeza taasisi hiyo ipate fedha kupitia masoko ya kifedha kwa kutoa dhamana ya kijamii ya thamani ya Sh500 milioni ili kuhakikisha wanafunzi wanapata ufadhili kwa wakati. Kwa sasa, takriban 450,000 wanaonufaika na mikopo ya HELB wanaendelea kulipa mikopo yao, hali inayowezesha bodi hiyo kukusanya karibu Sh700 milioni kila mwezi. Mbali na mikopo, HELB hutenga Sh237 milioni kila mwaka kama ufadhili kwa wanafunzi wenye mahitaji maalumu, ambapo Sh137 milioni huenda kwa wanafunzi wa vyuo vikuu na Sh100 milioni kwa wanafunzi wa vyuo vya TVET.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Tue, 21 Jul 2026 22:25:57

Gachagua akemewa kwa kauli yake kwamba watalii wasije Kenya sababu ya wahuni

KAULI ya aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua ya kuwataka watalii na wawekezaji wa kigeni kusubiri hadi baada ya Uchaguzi Mkuu wa 2027 kabla ya kuja Kenya imesolewa vikali serikalini, sekta ya utalii na hata baadhi ya washirika wake wa kisiasa. Akizungumza katika ibada ya kanisani mwishoni mwa wiki, Bw Gachagua alisema hali ya usalama nchini imezorota kutokana na ongezeko la ghasia za kisiasa na shughuli za makundi ya wahuni, akidai kuwa watalii na wawekezaji hawako salama. Kauli hiyo ilipingwa na Msemaji wa Serikali Isaac Mwaura, ambaye alisema utalii ni nguzo muhimu ya uchumi. Wakati huo huo, Rais William Ruto amekosoa Mahakama kwa kile alichosema ni kuwapa dhamana nafuu washukiwa wa uhalifu wanaotuhumiwa kuvuruga mikutano ya kisiasa, akisema hatua hiyo imechangia ongezeko la wahuni nchini. Akizungumza Ikulu, Nairobi, Jumanne, Rais alisema washukiwa wanaokamatwa kwa makosa ya jinai huachiliwa kwa dhamana ndogo na kurejea mitaani kuendelea na vitendo vyao. "Vijana wanaokamatwa kwa uhalifu hupelekwa mahakamani, wanapewa dhamana ya Sh200 na kuachiliwa kwa sababu ni watoto wetu. Kisha wanarudi katika mikutano ya kisiasa na kuendelea na vitendo vya kihuni," alisema Rais Ruto. Alisema Kenya lazima iwe na mjadala wa dhati kuhusu ongezeko la wahuni huku joto la kisiasa likizidi kupanda kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2027. Waziri wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen amesema uchunguzi unaendelea kubaini waliohusika na vurugu hizo.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Tue, 21 Jul 2026 21:55:42

Kenya yageuzwa ngome ya wahuni sasa wakitumiwa kutwaa ardhi, biashara na mali

KENYA inaendelea kugeuka kuwa paradiso ya wahuni wanaotumiwa kutwaa ardhi, nyumba, biashara na mali nyingine huku amri za mahakama zikipuuzwa na mamlaka zikionekana kushindwa kuwalinda waathiriwa. Katika miaka ya hivi karibuni, makundi ya vijana wenye silaha yamekuwa yakihusishwa na uvamizi wa hospitali, kufurusha familia kutoka nyumba zao, kutwaa majengo ya biashara na kuzuia utekelezaji wa amri halali za mahakama. Mojawapo ya visa vinavyoibua wasiwasi ni kile cha Hospitali ya Nakuru War Memorial, ambayo imefungwa kwa zaidi ya miaka miwili licha ya mahakama kuagiza ifunguliwe tena. Msimamizi mkuu wa wauguzi wa hospitali hiyo, Patricia Musale, anasema mgogoro ulianza Oktoba 2023 alipopigiwa simu akiarifiwa kuwa kundi la watu lilikuwa limevamia hospitali likidai limechukua usimamizi wake. Alipofika, lango kuu lilikuwa limefungwa na akalazimika kuruka ua kuingia ndani. "Muda mfupi baadaye, maafisa wa kaunti walichukua udhibiti wa hospitali na wagonjwa wote wakaanza kuhamishwa. Kabla ya usiku wa manane, kila mgonjwa alikuwa ameondolewa, wakiwemo watoto waliokuwa kwenye mashine za kuwasaidia kupumua," alisema. Hospitali ilipata amri za mahakama za kufunguliwa tena lakini kabla ya kutekelezwa, kundi jingine la zaidi ya vijana 200 lilivamia eneo hilo Januari 2024 na kuzuia mtu yeyote kuingia. "Tulipata amri kadhaa za mahakama lakini kila tunapofika tunawakuta wahuni wamezingira lango. Hata polisi wakifuatana nasi hakuna kinachofanyika," alisema Bi Musale. Kwa zaidi ya miaka miwili sasa, vifaa vya matibabu vya thamani ya mamilioni ya pesa vimekaa bila kutumika huku wafanyakazi wengi wakipoteza ajira na wagonjwa waliokuwa wakitegemea huduma kama za figo na matibabu ya Virusi vya Ukimwi wakiteseka. Mzozo huo unatokana na mgogoro wa umiliki wa ardhi kati ya hospitali na Serikali ya Kaunti ya Nakuru. Mnamo Februari 2024, Jaji Mkuu Martha Koome alieleza wasiwasi kuhusu uvamizi huo na ukaidi wa amri za mahakama, lakini hadi leo hospitali haijafunguliwa. Kisa kingine kinachoonyesha jinsi wahuni wanavyotumiwa kutwaa mali ni cha mfanyabiashara Avan Shah wa Nairobi. Bi Shah anasema Novemba 2022 dalali aliwasili nyumbani kwake akiwa ameandamana na takriban watu 30 waliokuwa na mapanga na marungu. "Walidai wanatekeleza amri ya mahakama. Kabla hatujathibitisha stakabadhi walikuwa tayari wameanza kubomoa nyumba. Polisi walifika lakini hawakutusaidia," alisema. Familia hiyo ilifurushwa kutoka nyumba waliyoishi kwa karibu miaka 50 na hadi sasa haijarejea huku kesi ikiendelea mahakamani. Kamati ya Ardhi ya Bunge la Kaunti ya Nairobi baadaye ilibaini kuwa kulikuwa na dosari katika usimamizi wa rekodi za ardhi hiyo na kupendekeza hatua zichukuliwe dhidi ya maafisa waliohusika. Visa hivi vinaonyesha mwenendo unaozidi kushika kasi ambapo migogoro ya ardhi, biashara na mali haiamuliwi tena mahakamani pekee bali pia kwa nguvu za makundi ya wahuni. Katika maeneo mengi nchini, wahuni hutumiwa kuwafurusha wapangaji, kufunga njia za kuingia katika majengo yanayobishaniwa, kutwaa biashara na hata kuzuia utekelezaji wa amri za mahakama. Hata madalali wanasema mara nyingi hulazimika kufanya kazi katika mazingira ya vitisho na ghasia. Wakenya wengi wanaishi kwa hofu kwamba siku moja wanaweza kupokonywa nyumba, biashara au ardhi yao kwa nguvu licha ya kuwa na haki kisheria. Kwa wengi, hali hiyo inaashiria hatari kubwa kwa utawala wa sheria, ambapo nguvu za makundi ya wahuni zinaanza kushinda mamlaka ya mahakama katika kuamua nani anamiliki mali nchini.

read more