T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Sun, 06 Sep 2026 23:55:59

Rais Ruto asisitiza Kenya haitauza madini ghafi nje ya nchi

RAIS William Ruto amesema Serikali yake inaandaa sera itakayokomesha usafirishaji wa malighafi kutoka Kenya kwenda nje, huku kampuni zikihitajika kuwekeza nchini, kuongeza thamani ya madini na kuunda nafasi za kazi. Akizungumza akiwa Kaunti ya Samburu, wakati wa hafla ya kutoa shukrani ya Katibu wa Ugatuzi, Michael Lenasalon, Rais Ruto alisema amechukua hatua binafsi kuhakikisha usafirishaji wa madini kutoka Magadi unakomeshwa. Alisema sera hiyo itahusu rasilimali zote za nchi, zikiwemo mafuta, dhahabu na madini adimu. "Kuanzia sasa, msimamo wetu wa kisera ni kwamba iwe ni soda ya Magadi, mafuta au madini yetu yote, ikiwemo dhahabu na madini adimu, tumeamua kwamba hatutasafirisha tena malighafi," alisema. Rais alisema Serikali itahakikisha madini yanachakatwa nchini ili kuongeza thamani na kutoa ajira kwa Wakenya. Alisema pia Serikali inashirikiana na mfanyabiashara Aliko Dangote kuanzisha kiwanda cha kusafisha mafuta Lamu. Aidha, alisema Serikali inashirikiana na wawekezaji wengine kuanzisha viwanda vya kusafisha dhahabu na kuchakata madini katika maeneo mbalimbali nchini. "Itakuwa si busara kwa Serikali kusafirisha malighafi, kuunda ajira na kuongeza thamani katika nchi nyingine wakati tuna vijana wengi wanaohitaji ajira," alisema. Rais alisema alilazimika kwenda Kajiado kushughulikia mkataba wa awali wa uchimbaji, ambao alisema ulikuwa ukinufaisha zaidi kampuni kuliko Wakenya.  Alisema mkataba huo, ambapo Kenya ilipata asilimia tano pekee huku asilimia 95 ya thamani ikitengenezwa nje ya nchi, umefutwa.  "Hatuwezi kufuata malighafi zetu nje ya nchi na kununua bidhaa kwa bei ya juu huku vijana wetu wakikosa ajira," alisema. Rais alisema tenda mpya itatangazwa na kampuni zaidi zitaruhusiwa kuwekeza Kajiado. Alisema Serikali haitaki kampuni moja pekee, bali inataka zaidi ya kampuni tano na hata 10 zitumie rasilimali hizo kuunda ajira na kuongeza thamani. Jumamosi, Rais alitangaza kuwa mkataba wa uchimbaji wa Tata Chemicals, iliyojulikana zamani kama Magadi Soda, utatangazwa upya kupitia zabuni yenye ushindani. Alisema mkataba huo ulikuwa wa kunyanyasa Kenya na hauwezi kuendelea. Rais Ruto pia aliahidi kuhakikisha ushirikiano wa kisiasa kati ya UDA na ODM unaendelea hata baada ya uchaguzi wa 2027.  Alishukuru ODM kwa kusaidia kupunguza joto la kisiasa nchini.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Sun, 06 Sep 2026 22:55:41

T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Sun, 06 Sep 2026 21:55:35

Wantam! Gachagua ainua mkono, asema Sifuna tosha kupambana na Ruto 2027

ALIYEKUWA Naibu rais Rigathi Gachagua amefungua mlango wa muungano usiotarajiwa wa kisiasa kati ya Mlima Kenya na Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna, akisema eneo hilo liko tayari kumuunga mkono iwapo atachaguliwa kuwa mgombea wa pamoja wa upinzani katika uchaguzi wa 2027. Katika hatua inayotofautiana na siasa za viongozi wa kikanda zinazoshuhudiwa kwa sasa, Bw Gachagua alisema yuko tayari kuwa mgombea mwenza wa Bw Sifuna au kumruhusu seneta huyo kuwa naibu wake, iwapo hilo litasaidia kumng'oa Rais William Ruto madarakani. "Niko tayari hata kuwa naibu wake. Yeye pia anaweza kuwa naibu wangu. Sifuna ni mshirika sawa katika mpango wa upinzani kutafuta mgombea urais wa pamoja," alisema Bw Gachagua alipohutubia Wakenya mjini Spokane, Amerika, Jumamosi jioni. Alisema upinzani haupaswi kuharakisha kumteua mgombea wake wa urais, akipendekeza uamuzi huo ufanywe kati ya Machi na Mei mwakani. "Hakuna haraka. Tutahakikisha tutamshinda Rais Ruto katika awamu ya kwanza ya uchaguzi," alisema. Kauli hizo ni ishara ya wazi kwamba Bw Gachagua yuko tayari kuangalia nje ya Mlima Kenya katika kutafuta nguvu za kisiasa za kukabiliana na Dkt Ruto. Kwa miezi kadhaa, Bw Gachagua amejitokeza kama mmoja wa viongozi wakuu wa kisiasa wa Mlima Kenya, baada ya kutofautiana vikali na Rais Ruto. Hata hivyo, msimamo wake wa sasa unaashiria kuwa mkakati wake unaweza kuwa mpana zaidi ya kutafuta tiketi ya upinzani. Anataka pia kuhakikisha kura za Mlima Kenya zitatumika katika muungano mpana wa upinzani wenye uwezo wa kumshinda Dkt Ruto badala ya eneo hilo kujitenga kwenye uchaguzi mkuu wa 2027. Bw Gachagua alipuuzilia mbali hoja kwamba Bw Sifuna hawezi kuungwa mkono Mlima Kenya kwa sababu anatoka magharibi mwa Kenya. Alimlenga Kiongozi wa Wengi katika Seneti Aaron Cheruiyot, ambaye amekuwa akihoji ikiwa Mlima Kenya utamuunga mkono Bw Sifuna iwapo atapewa tiketi ya upinzani. Bw Gachagua alikumbusha kwamba Mlima Kenya ulimuunga mkono kwa wingi Dkt Ruto katika uchaguzi wa 2022, licha ya Rais huyo kutotoka eneo hilo. "Wachache walimpigia kura Raila Odinga. Wote wawili hawakuwa watu wa mlima," alisema. Pia alikataa hoja ya Katibu Mkuu wa COTU Francis Atwoli kwamba Bw Sifuna ni mchanga mno kuwa rais. Bw Gachagua alimtaja aliyekuwa Rais wa Amerika Barack Obama, aliyechaguliwa akiwa na miaka 47, akisema umri haupaswi kutumiwa kuwazuia wanasiasa vijana kuwania urais. "Ikiwa Obama alichaguliwa kuongoza taifa lenye nguvu zaidi duniani akiwa na miaka 47 mwaka 2008, ni nini kinachomzuia Sifuna kuchaguliwa kuwa Rais wa Kenya akiwa na miaka 45 mwaka 2027?" aliuliza. Bw Gachagua amesema mara kwa mara kuwa ushindani wa upinzani dhidi ya Dkt Ruto ni suala la kuunganisha kura kuliko tamaa za mtu mmoja mmoja. "Niko tayari kumuunga mkono mgombea mwingine yeyote isipokuwa Rais Ruto mwaka 2027," alisema. Msimamo huo unaweza kuwa muhimu vyama vya upinzani vinapojadiliana kuhusu tiketi ya pamoja. Bw Gachagua anajenga DCP kuwa chama cha kitaifa, huku aliyekuwa Waziri wa Usalama wa Ndani Fred Matiang'i akiwa na tiketi ya Jubilee. Bw Sifuna naye amejitokeza kama mmoja wa wanasiasa vijana wenye sauti katika kundi la Linda Mwananchi. Viongozi wengine wa upinzani, akiwemo aliyekuwa Naibu Rais Kalonzo Musyoka na kiongozi wa Narc-Kenya Martha Karua, pia wanatajwa katika mazungumzo kuhusu muundo wa muungano wa 2027. Bw Gachagua pia aliitaka IEBC kuhakikisha uchaguzi wa 2027 unaaminika, hasa katika ununuzi wa vifaa, teknolojia na usimamizi wa mchakato wa uchaguzi.

read more