T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Sat, 05 Sep 2026 01:55:50

Mzozo wa fidia Mau wazuka tena familia 15,000 zikidai kuachwa nje

MPANGO wa kufidia familia zilizofurushwa kutoka Msitu wa Mau umeibua tena mzozo wa kibinadamu na kisiasa katika eneo la South Rift, huku maelfu ya waathiriwa wakidai serikali imewatelekeza. Zaidi ya familia 15,000 ambazo hazikujumuishwa katika mpango wa fidia sasa zinataka kulipwa. Zinadai baadhi ya maafisa wa serikali waliingiza majina ya jamaa na washirika wao katika orodha ya walionufaika, licha ya kutokuwa waathiriwa. Mzozo huo ulizuka baada ya Rais William Ruto kutangaza Agosti 26 katika uwanja wa Shule ya Sekondari ya Tendwet, Narok Kusini, kuwa serikali ilikuwa imelipa familia 13,000 zilizofurushwa Mau mwaka 2019. Serikali ilikuwa imesajili familia 28,000 kuwa waathiriwa wa zoezi hilo. Hata hivyo, haikutoa maelezo ya kwa nini familia 15,000 ziliachwa nje ya mpango wa fidia. Rais Ruto alisema Sh2.6 bilioni zimetolewa kwa familia 13,000, kila moja ikipokea Sh200,000 kupitia simu zao.  "Leo tunatoa Sh2.6 bilioni kwa jumla ya familia 13,000 zilizofurushwa kutoka Msitu wa Mau. Kila familia sasa itapokea Sh200,000 kama fidia," alisema. Alisema familia nyingine 2,000 zilizokuwa zinaishi katika kambi za wakimbizi wa ndani zilishapokea fidia ya Sh300,000 kila moja, hatua iliyowezesha kufungwa kwa kambi hizo baada ya zaidi ya miaka sita. Rais Ruto alisema suala la Mau lilikuwa limefikia mwisho. Hata hivyo, tangazo hilo limefufua mzozo huo badala ya kuumaliza. Familia zilizoachwa nje zimelalamika na kutishia kurejea katika Msitu wa Mau iwapo serikali haitazifidia kama wenzao waliolipwa. Katika mkutano uliofanyika Olmekenyu mnamo Alhamisi, maelfu ya waathiriwa walitaka serikali ieleze kwa nini waliondolewa kwenye orodha ya walionufaika. Walisema serikali ina siku saba kutoa suluhisho kabla yao kuchukua hatua zaidi. Diwani wa wadi ya Mara, Kipngeno Chepkwony, ambaye ndiye kiongozi pekee aliyezungumza na waathiriwa hao, aliitaka serikali kuchunguza suala hilo upya. "Tuongee na serikali na hasa Rais kuhusu suala hili ili tupate suluhisho la kudumu. Tusiruhusu suala hili kutumiwa kisiasa ili watu walioachwa nje ya mpango wa fidia waweze kuzingatiwa na kulipwa," alisema. Mmoja wa waathiriwa, Fred Mutai, alisema familia zimevumilia kwa muda mrefu.  "Familia zimeteseka kwa muda mrefu, lakini serikali imeongeza chumvi na pilipili kwenye kidonda cha zamani na kufanya hali ambayo tayari ilikuwa dhaifu kuwa mbaya zaidi," alisema.  Afisa wa DCP Leonard Cheruiyot alisema Sh200,000 hazitoshi na serikali ilipaswa kununua ardhi na kuwapa waathiriwa makazi mapya.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Sat, 05 Sep 2026 00:55:27

Ruto aagiza maafisa wa polisi kuheshimu haki za binadamu

RAIS William Ruto amewataka maafisa wa usalama nchini kuzingatia haki za binadamu, uwajibikaji na utaalamu wanapotekeleza majukumu yao, huku serikali ikiendeleza mageuzi makubwa yanayolenga kuboresha huduma za polisi nchini. Akizungumza Ijumaa katika hafla ya kufuzu kwa kundi la 59 la makurutu wa Huduma ya Polisi wa Utawala katika Chuo cha Kitaifa cha Polisi, Embakasi, Rais alisema kuwa mageuzi yanayoendelea katika Huduma ya Kitaifa ya Polisi yanalenga kujenga taasisi yenye uwajibikaji na inayowahudumia wananchi kwa ufanisi zaidi. "Katiba inataka Huduma ya Kitaifa ya Polisi kudumisha taaluma na nidhamu, kuzuia ufisadi, kuzingatia uwazi na uwajibikaji, kuheshimu haki za binadamu na kudumisha imani ya wananchi," alisema Rais Ruto. Aliongeza kuwa misingi hiyo inapaswa kuongoza kila hatua ya maafisa wa polisi, kuanzia kukamatwa kwa washukiwa, uchunguzi wa makosa ya jinai, usimamizi wa mikusanyiko ya umma hadi mahusiano yao ya kila siku na wananchi. Rais pia aliwakumbusha maafisa hao kuwa Katiba inalinda haki na uhuru mbalimbali ikiwemo uhuru wa kujieleza, kujiunga na vyama, kukusanyika, kuandamana na kushiriki shughuli za kisiasa, na kwamba polisi wana wajibu wa kulinda haki hizo. "Katiba yetu pia inahakikisha uhuru wa kujieleza, kujumuika, kukusanyika, kuandamana na kushiriki kisiasa. Hizi ni haki muhimu katika mfumo wetu wa kidemokrasia na lazima ziheshimiwe na kulindwa," alisema. Rais alisema mageuzi ya polisi yanafanywa kwa manufaa ya umma na yanagharamiwa kwa fedha za walipa kodi, hivyo kila hatua katika mchakato huo lazima iwe wazi na iweze kuchunguzwa na wananchi. "Mpango huu wote wa mageuzi unatekelezwa kwa maslahi ya umma na kwa kutumia rasilimali za umma," alisema, akiongeza kuwa kila kipengele cha mageuzi hayo kinapaswa kuhimili uchunguzi wa wananchi. Aliwaambia maafisa waliofuzu kuwa mafanikio ya mageuzi hayo hayatapimwa kwa sera, hotuba, sare mpya au vifaa vya kisasa pekee, bali kwa namna wananchi wa kawaida watakavyohudumiwa. "Yatapimwa kwa kuangalia kama afisa anaitikia anapohitajika, anatekeleza sheria bila upendeleo, anakataa rushwa, analinda walio katika mazingira magumu, anaheshimu utu wa binadamu na anawatendea Wakenya wote kwa usawa mbele ya sheria," alisema Rais. Aliwataka maafisa hao kutekeleza majukumu yao kwa ujasiri lakini pia kwa kujizuia na kuonyesha utu. "Hudumuni kwa ujasiri, lakini kwa kujizuia; tumieni mamlaka yenu, lakini kwa uwajibikaji; na tekelezeni sheria, lakini kwa ubinadamu," alisema. Kauli za Rais zilijiri huku Waziri wa Usalama wa Ndani na Utawala wa Kitaifa Kipchumba Murkomen akikanusha madai kwamba kuna vitengo vya polisi vinavyofanya kazi nje ya mamlaka ya Inspekta Jenerali wa Polisi Douglas Kanja. Murkomen alisema madai hayo hayana ukweli na yanalenga kupotosha umma kuhusu muundo wa uongozi ndani ya Huduma ya Kitaifa ya Polisi. "Wale wanaodai kwamba kuna vitengo ndani ya Huduma ya Kitaifa ya Polisi vinavyofanya kazi nje ya mamlaka ya Inspekta Jenerali ni wapotoshaji wa ukweli," alisema. Alisisitiza kuwa serikali itaendelea kuunga mkono uhuru wa Huduma ya Kitaifa ya Polisi na kuilinda dhidi ya ushawishi wa nje. "Tutaendelea kuunga mkono uhuru wa NPS dhidi ya aina yoyote ya kuingiliwa kutoka nje," alisema. Murkomen alisema mageuzi yanayotekelezwa kwa sasa yanatokana na mapendekezo ya Jopokazi la Kitaifa kuhusu Mageuzi ya Polisi lililoongozwa na aliyekuwa Jaji Mkuu David Maraga. Kwa mujibu wake, mageuzi hayo yanalenga kuunda huduma ya polisi yenye utaalamu, iliyoandaliwa vizuri, iliyo na vifaa vya kisasa na inayoweka maslahi ya wananchi mbele. Miongoni mwa hatua zilizokwisha kutekelezwa ni kuboresha mitaala ya mafunzo ya polisi ili kuweka mkazo zaidi kwenye haki za binadamu, katiba na utawala wa sheria. "Moja ya mambo yaliyofanyika ni kuboresha mtaala wa mafunzo. Sasa unajumuisha mafunzo kuhusu haki za binadamu, utawala wa kikatiba na utawala wa sheria," alisema Murkomen. Waziri huyo alisema serikali pia inawekeza pakubwa katika teknolojia na vifaa vya kisasa ili kuboresha operesheni za usalama na utoaji huduma kwa wananchi. Rais alisema ustawi wa maafisa wa polisi umepewa kipaumbele katika mageuzi hayo. Alieleza kuwa serikali imekamilisha awamu tatu za nyongeza ya mishahara, hatua iliyoongeza mshahara wa msingi wa konstebo wa polisi kwa asilimia 36.

read more