T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Sun, 19 Jul 2026 23:55:59

Raha tele walimu wakiongezwa mshahara mwezi huu

WALIMU nchini wataanza kupokea nyongeza ya mishahara kuanzia malipo ya mwezi huu baada ya Tume ya Kuwaajiri Walimu (TSC) kutekeleza awamu ya pili ya Mkataba wa Makubaliano (CBA) wa miaka ya 2025–2029. Marekebisho hayo ya mishahara, yaliyoanza kutumika Julai 1, 2026, yatawaongezea walimu pesa ya hadi Sh2,055 kwa mwezi kulingana na daraja lao la kazi. Walimu wa madaraja ya C2 na C3 ndio watanufaika zaidi, huku Walimu wa Sekondari I katika daraja la C3 wakipata nyongeza ya juu zaidi. Kupitia barua ya Julai 16, TSC iliagiza wakurugenzi wa elimu wa maeneo yote kuhakikisha viwango vipya vya mishahara vinaanza kutekelezwa mara moja hadi Juni 30, 2027. Mkataba huo ni awamu ya pili ya makubaliano yaliyotiwa saini kati ya TSC na vyama vya walimu vya KNUT, KUPPET na KUSNET. Walimu wataendelea kubaki katika madaraja yao ya sasa lakini watahamishiwa viwango vipya vya mishahara. Walimu ambao nyongeza yao ya kawaida ya kila mwaka huanza Julai 1 watapokea kwanza nyongeza hiyo kabla ya kuhamishiwa kwenye viwango vipya. TSC ilisema walimu wote waliokuwa kazini kufikia Julai 1, 2026 watanufaika na mabadiliko hayo isipokuwa walimu wa mafunzo kwa vitendo (interns). Aidha, tarehe zao za nyongeza za kila mwaka zitaendelea kubaki kama zilivyokuwa. Chini ya viwango vipya, Wakuu Wakuu wa Shule katika daraja la D5 sasa watapokea mshahara wa kati ya Sh133,351 na Sh164,977 kwa mwezi. Wakuu wa Shule waandamizi na Maafisa Wakuu wa Usaidizi wa Mtaala wa daraja la D4 watapata kati ya Sh120,016 na Sh148,480, huku Wakuu wa Shule na Naibu Wakuu wa daraja la D3 wakilipwa kati ya Sh107,634 na Sh131,405. Walimu wa daraja la D2, wakiwemo Naibu Wakuu wa Shule II na Walimu Wakuu waandamizi, watapokea kati ya Sh93,883 na Sh114,322 kwa mwezi, huku walimu wa daraja la D1 pia wakinufaika na viwango hivyo vipya. TSC ilieleza kuwa posho zote zinazolipwa kwa sasa zitaendelea bila mabadiliko. Hizo ni pamoja na posho ya nyumba, mazingira magumu, usafiri, mizigo, likizo ya kila mwaka na posho ya mwongozo kwa walimu wenye ulemavu pale inapohusika. Naibu Katibu Mkuu wa KNUT, Hesbon Otieno, alipongeza hatua hiyo lakini akasema chama hicho kitapigania kipindi kifupi zaidi cha CBA ili walimu waweze kujadiliana kuhusu mishahara na maslahi yao mara kwa mara. Aliongeza kuwa ingawa nyongeza hiyo italeta afueni kwa walimu, haitoshi kukabiliana kikamilifu na changamoto zinazowakabili, zikiwemo gharama ya juu ya maisha, uhaba wa walimu, kucheleweshwa kupandishwa vyeo na mzigo mkubwa wa kazi. Otieno alisema KNUT tayari imewasilisha pendekezo la kufupishwa kwa muda wa utekelezaji wa CBA kwa Rais William Ruto na sasa mazungumzo yataendelea kati ya chama hicho, TSC na Wizara ya Elimu. Kwa mujibu wa vyama vya walimu, pamoja na kuboreshwa kwa mishahara, serikali inapaswa kushughulikia pia changamoto nyingine zinazowakabili walimu kama vile uhaba wa wahudumu, huduma duni za matibabu, kuhudumu kwa muda mrefu katika nyadhifa za kaimu bila kunufaika na marupurupu yanayostahili pamoja na mazingira bora ya kazi ili sekta ya elimu iweze kuvutia na kuhifadhi walimu wenye taaluma na uzoefu.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Sun, 19 Jul 2026 22:55:07

Kindiki 'akemea' Waziri Ruku kuhusu matamshi yake ya kuleta mgawanyiko Mlimani

MGAWANYIKO wa kisiasa umeibuka ndani ya kambi ya Rais William Ruto baada ya Naibu Rais, Profesa Kithure Kindiki, kupinga hadharani wito wa Waziri wa Utumishi wa Umma, Geoffrey Ruku, wa kutaka Mlima Kenya Mashariki utengane kisiasa na wenzao wa Mlima Kenya Magharibi. Mvutano huo unajiri siku chache baada ya ushindi wa upinzani katika uchaguzi mdogo wa Ol Kalou kufufua mjadala kuhusu mwelekeo wa kisiasa wa eneo la Mlima Kenya, ambalo lina idadi ya juu ya wapigakura. Akizungumza katika ibada ya shukrani ya Dayosisi ya Anglikana ya Embu katika Chuo cha Ualimu cha St Mark's Kigari, Kaunti ya Embu, Profesa Kindiki alisema hataruhusu juhudi zozote za kuligawa eneo hilo kisiasa. "Sitaki watu wetu waanze kuzungumza lugha tofauti. Tumefanya mambo mengi pamoja, tuna historia ndefu na hakuna kinachoweza kuleta mgawanyiko. Kama Naibu Rais nitahakikisha Mlima Kenya unabaki umeungana. Kwa sasa mimi ndiye Naibu Rais na nitahakikisha jamii zetu zinaendelea kutembea pamoja," akasema. Aidha, aliwataka wakazi wa Mlima Kenya kuendelea kumuunga mkono Rais Ruto, akisema hiyo ndiyo njia bora ya kuhakikisha eneo hilo linatoa rais 2032. "Nataka tuwe na mazungumzo ya kweli na watu wetu. Baada ya William Ruto, ni sisi. Ile timu nyingine tuko nambari 20; tutafikiwa baada ya miaka 200," akasema. Kauli ya Profesa Kindiki inaenda kinyume na matamshi ya awali ya Bw Ruku ambaye amekuwa akirindima ngoma ya Mlima Kenya Mashariki kuwa na msimamo wake wa kisiasa na kiuchumi. "Ninapozungumzia mgawanyiko, ninarejelea masuala ya siasa za eneo letu. Nikiona jambo haliko sawa nitalizungumzia." Naibu Rais yuko sahihi kuhusu kuwaunganisha Wakenya," akasema Bw Ruku akikanusha ametofautiana na rais. Baadaye akiwa katika Kanisa la AIC Kabartonjo, Baringo Kaskazini, Bw Ruku alisema Mlima Kenya Mashariki umeamua kubaki ndani ya Kenya Kwanza na hautashawishiwa na kampeni za kiongozi wa DCP Rigathi Gachagua. Pia alipuuza madai kwamba ushindi wa upinzani katika uchaguzi mdogo wa Ol Kalou unaashiria Rais Ruto amepoteza uungwaji mkono wa Mlima Kenya.  "Gachagua anajigamba baada ya ushindi wa Ol Kalou akidai anadhibiti kura za Mlima Kenya. Kama Raila alikaribia kushinda bila kuungwa mkono na Mlima Kenya, Gachagua anategemea vipi kumshinda Rais Ruto 2027?" akauliza. Kwa mujibu wa mdadisi wa kisisa Prof Gitile Naituli mjadala wa kugawa Mlima Kenya unasukumwa zaidi na maslahi ya kisiasa kuliko maendeleo. "Mtu anayepaswa kuwa na wasiwasi ni Prof Kindiki. Hatakiwi kuruhusu mjadala wa mgawanyiko iwapo ana matumaini ya kumrithi bosi wake mnamo 2032. Hakuna atakayekuchukulia kwa uzito katika siasa za kitaifa ikiwa hujaunganisha ngome yako," akasema

read more