T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Mon, 07 Sep 2026 02:55:30

Mackenzie na wenzake kujua hatima yao mwezi huu

MSHUKIWA wa mauaji ya Shakahola, Paul Mackenzie, na washtakiwa wenzake wanatarajiwa kujua hatima yao mwezi huu katika kesi inayohusu vifo vya watoto 191. Uamuzi huo unatarajiwa kutolewa mwaka mmoja baada ya kesi hiyo kuanza Septemba mwaka uliopita. Mackenzie anakabiliwa na mashtaka hayo pamoja na washtakiwa wengine 30, ambao upande wa mashtaka umedai walihusika sana katika vifo vya watoto hao. Kesi hiyo ilikuwa ya aina yake, huku Biblia, Quran na Katiba zikitajwa kwa kina na upande wa mashtaka pamoja na washtakiwa katika juhudi zao za kutetea misimamo yao. Washtakiwa walitumia aya za Biblia kuhalalisha kukaa kwao msituni na vifo vilivyofuata, huku upande wa mashtaka ukirejelea Biblia kuonyesha kwamba hata wakati wa Yesu Kristo, aina fulani za dawa zilikuwepo za kukabiliana na magonjwa na dharura, na kwamba watu hawakutegemea maombi pekee kwa ajili ya uponyaji. Wakati mmoja, kesi ya mauaji ya Shakahola iligeuka kuwa kama darasa la thiolojia, huku maswali yakiibuliwa kuhusu iwapo wale wanaodaiwa kufunga hadi kufa kwa imani kwamba wangeenda mbinguni na kukutana na Yesu, kwa hakika wako mbinguni. Hata hivyo, hakukuwa na jibu la moja kwa moja, kwani hakuna aliyeweza kusema kwa uhakika ni hatima gani iliyowakuta wale waliokufa njaa. Wakati mwingine, Mackenzie alitaka upande wa mashtaka kuthibitisha kwamba wale anaodaiwa kuwaua kupitia kufunga hawako mbinguni. Upande wa mashtaka ulipuuza maswali hayo na kuyataja kuwa ni masuala ya kithiolojia, ukisisitiza kwamba lengo lake halikuwa kuamua masuala ya imani, bali kuthibitisha vipengele vya uhalifu katika hatia ziliosababisha maafa hayo. Upande wa mashtaka umeomba Mahakama Kuu kuamua Mackenzie ana hatia ya mauaji, ukisema umethibitisha kikamilifu kwamba vifo vilitokea, chanzo chake, jukumu la Mackenzie katika kuvisababisha, pamoja na hali yake ya akili wakati huo. Kulingana na upande wa mashtaka, ushahidi wa kisayansi wa uchunguzi wa miili na vipimo vya baada ya kifo ulithibitisha kuwa njaa ndiyo iliyokuwa sababu kuu ya vifo miongoni mwa waathiriwa wengi. "Ingawa sababu ya kifo cha baadhi ya miili haikuweza kubainishwa kimatibabu kwa sababu ilikuwa imeoza sana au kubaki mifupa pekee, mahakama inaweza kuhitimisha kwamba nao walikufa kwa njaa kutokana na mazingira yaliyozunguka vifo hivyo," alisema Naibu Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma, Bw Jami Yamina. Ushahidi uliowasilishwa na Serikali ulionyesha kuwa asilimia 48.9 ya miili yote iliyochunguzwa, wakiwemo watu wazima na watoto, walikufa kutokana na njaa, huku sababu ya kifo kwa asilimia 45.9 ikiwa haikubainika. Hata hivyo, washtakiwa wamejitetea kwamba ingawa kesi hiyo kuwa imezungukwa na msiba, imejaa majonzi na hisia nzito, mahakama si jukwaa la maombolezo, bali ni kitengo vha haki, kinachohitaji ushahidi. Kupitia kwa wakili wao Lawrence Obonyo, washtakiwa walisema kutokea kwa kifo pekee, hata kama ni cha kusikitisha kiasi gani, hakumaanishi moja kwa moja kwamba washtakiwa wana hatia. Bw Obonyo aliitaka mahakama isiruhusu uzito wa janga la Shakahola kufunika kile alichokitaja kuwa udhaifu na mapengo katika ushahidi wa upande wa mashtaka. Upande wa mashtaka uliita mashahidi 120 kuthibitisha kesi yake, huku washtakiwa wakiita mashahidi zaidi ya 21 kujitetea.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Mon, 07 Sep 2026 01:55:03

Ofisi 3 zinazohusishwa na Rais Ruto zafyonza Sh100 bilioni-ripoti

OFISI tatu zinazohusishwa na Rais William Ruto zilitumia Sh33 bilioni katika mwaka uliokamilika Juni 2026, kiwango cha juu zaidi kuwahi kutumiwa na ofisi za maafisa wakuu wa Serikali, kwa mujibu wa ripoti mpya ya Wizara ya Fedha. Matumizi hayo ya ofisi za Rais William Ruto, Naibu Rais Kithure Kindiki na Mkuu wa Mawaziri Musalia Mudavadi yanafanya jumla ya fedha zilizotumiwa na ofisi hizo tangu Kenya Kwanza iingie madarakani mwaka 2022 kufikia Sh100.23 bilioni. Kwa miaka minne, matumizi ya urais yamezidi Sh89.9 bilioni zilizotumiwa na mtangulizi wake, Uhuru Kenyatta, katika miaka 10 ya uongozi. Ripoti ya Wizara ya Fedha kuhusu hali ya uchumi na bajeti ya mwaka wa kifedha 2025/26 inaonyesha Ikulu ilitumia Sh18.4 bilioni. Katika miezi mitatu ya mwisho ya mwaka huo, Aprili hadi Juni 2026, Ikulu ilitumia Sh6.8 bilioni. Hii ni sawa na wastani wa Sh570 milioni kwa wiki au Sh81.3 milioni kila siku. Katika kipindi hicho, Rais Ruto aliandaa shughuli mbalimbali katika Ikulu, huku maelfu ya watu wakifika katika hafla kadhaa. Miongoni mwa waliomtembelea Ikulu ni wanachama wa Maendeleo ya Wanawake mnamo Aprili 1, 2026, pamoja na viongozi wa mashinani kutoka kaunti mbalimbali. Mnamo Mei 11, Ikulu pia iliandaa karamu ya kitaifa kwa wajumbe wa Mkutano wa Africa Forward. Ikulu imekuwa ikitumia kiasi kikubwa cha fedha tangu Rais Ruto aingie madarakani. Kati ya Julai 2022 na Juni 2026, ilitumia jumla ya Sh43 bilioni, sawa na asilimia 43 ya zaidi ya Sh100 bilioni zilizotumiwa na ofisi zilizo chini ya Urais. Katika robo ya kwanza ya mwaka wa kifedha 2025/26, Ikulu ilitumia Sh4.56 bilioni. Kiasi hicho kilishuka hadi Sh3.17 bilioni katika robo ya pili, kabla ya kupanda hadi Sh3.85 bilioni katika robo iliyomalizika Machi 2026. Katika robo ya mwisho, matumizi yalipanda kwa karibu theluthi mbili hadi Sh6.83 bilioni. Kati ya Sh18.4 bilioni zilizotumiwa na Ikulu katika mwaka huo, Sh17.12 bilioni zilitumika katika shughuli za kawaida. Fedha hizo ziligharamia mishahara ya wafanyakazi, mafuta ya magari ya viongozi, marupurupu na tiketi za ndege za maafisa wanaosafiri ndani na nje ya nchi, pamoja na chakula cha wageni. Kwa mwaka huu wa kifedha, Ikulu imetengewa takriban Sh13.5 bilioni, ingawa kiasi hicho kinaweza kubadilika wakati wa marekebisho ya bajeti. Ofisi ya Rais ilifuata Ikulu kwa matumizi ya Sh8 bilioni. Kati ya kiasi hicho, Sh6.68 bilioni zilitumika katika shughuli za kawaida. Hii ni wastani wa Sh667.75 milioni kila mwezi au karibu Sh22 milioni kila siku. Ofisi ya Naibu Rais Kindiki ilitumia Sh5.2 bilioni, huku Sh100 milioni pekee zikitumika kwa shughuli za maendeleo. Kwa upande wake, Ofisi ya Mudavadi ilitumia Sh602 milioni, zote zikiwa za shughuli za kawaida. Idara ya Serikali ya Masuala ya Bunge ilitumia Sh433 milioni, huku Idara ya Serikali ya Masuala ya Baraza la Mawaziri ikitumia Sh226 milioni. Kwa jumla, matumizi ya ikulu, Ofisi ya Rais, Ofisi ya Naibu Rais na Ofisi ya Mkuu wa Mawaziri yalifikia asilimia 98 ya Sh32.9 bilioni zilizotumiwa na Urais. Mwaka wa kifedha 2024/25, Urais ulitumia Sh21 bilioni, chini ya Sh22.8 bilioni zilizotumiwa mwaka uliotangulia na Sh23.3 bilioni zilizotumika katika mwaka wa kwanza wa serikali ya Rais Ruto, 2022/23. Msemaji wa Ikulu Hussein Mohamed alisema matumizi yote yaliidhinishwa na wabunge. Alisema ofisi zilizo chini ya urais hazitekelezi miradi moja kwa moja, bali zinahusika zaidi na sera, uratibu na kusaidia utekelezaji wa majukumu ya Rais na Naibu Rais.

read more