T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Mon, 13 Jul 2026 09:05:10

Bei ya mafuta yaanza kupanda tena baada ya Amerika kurejelea vita na Iran

TEHRAN, Iran: MASHAMBULIZI baina ya wanajeshi wa Amerika na Iran yaliyoendelea tokea wikendi yamechangia kupanda tena kwa bei ya mafuta ulimwenguni. Iran ililenga vituo vya kijeshi vya Amerika katika eneo la Ghuba na kutangaza kuwa imefunga tena Mlango-bahari wa Hormuz. Wanajeshi wa Iran Jumatatu walisema walilenga kambi za jeshi la Amerika nchini Bahrain na Kuwait na kuharibu vifaa vya kijeshi nchini Oman. Pia Iran ilishambulia ghala la silaha katika kambi ya jeshi la Anga la Prince Hassan nchini Jordan huku ikilipiza kisasi shambulizi lolote linalotekelezwa na Amerika. Amerika nayo ilishambulia mifumo ya ulinzi wa anga ya Iran, kambi ya jeshi pwani na boti za kijeshi. Ilitumia ndege za kivita, meli za kijeshi na ndege zisizo na rubani (droni). Mapigano hayo yanaonyesha kuwa muafaka wa kusitisha vita kati ya nchi hizo mbili sasa umekiukwa. Muafaka huo uliafikiwa mnamo Juni na ulilenga kufungua Mlango-bahari wa Hormuz na kusitisha vita kabisa kwa siku 60. Katika mahojiano mafupi na Reuters Jumapili, Rais wa Amerika Donald Trump alitabiri kuwa mara hii watalemea Iran katika vita hivyo. "Tunawashinda vibaya," akasema Trump. Kiongozi huyo tayari ameweka wazi kuwa hatilii manani muafaka uliotiwa saini ambao anasema umekufa japo akasema iwapo Iran inataka kunusurika bado kutakuwa na mazungumzo. Mwakilishi wa Iran kwenye mazungumzo na Amerika, Mohammad Baqer Qalibaf amesema kuwa wapo tayari kwa vita na hawatakubali kuhadaiwa tena. "Enzi za makubaliano yanayoegemea upande mmoja zimekwisha. Tuliwaambia watimize ahadi zeo au walipe gharama na sasa ukweli unaonekana," akasema. Vita vilivyoanzishwa na Amerika-Israel dhidi ya Iran mnamo Februari 28 vimevuruga usalama katika eneo la Ghuba na kuenea katika Mashariki ya Kati. Iran imeonyesha uwezo mkubwa wa kijeshi na umekuwa ukishambulia kambi za wanajeshi wa Amerika Mashariki ya Kati. Vita hivyo vimesababisha maelfu ya watu kuuawa, wengi wao wakiwa Iran na Lebanon. Iran imezima shughuli katika Strait of Hormuz na sasa kando na bei ya mafuta kupanda kuna mfumuko wa bei ya bidhaa kote ulimwenguni. Aidha Iran inasisitiza kuwa itafungua mkondo huo na kuruhusu meli za kupitisha mafuta iwapo Amerika itazima shughuli za kijeshi katika Pwani yake.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Mon, 13 Jul 2026 08:39:52

Kampuni inavyotumia ubunifu kuvutia wateja wa maua

WAKATI mamia ya wageni wa humu nchini na kutoka mataifa mbalimbali walipofurika katika Maonyesho ya Kimataifa ya Kibiashara ya Maua (IFTEX) jijini Nairobi, kampuni moja ya Kenya ilivutia wengi kwa ubunifu wa kipekee uliosimamisha shughuli katika Ukumbi wa Visa Oshwal. Banda la Ole Engai Growers lilikuwa miongoni mwa yaliyopigwa picha zaidi katika maonyesho hayo ya mwaka huu, 2026 baada ya kuwasilisha sanamu ya farasi mwenye ukubwa wa wastani wa mnyama huyo, iliyotengenezwa kwa maua mabichi yaliyolimwa kwenye mashamba ya kampuni hiyo. Farasi huyo wa maua, aliyebuniwa kuadhimisha Mwaka wa Farasi katika kalenda ya Mwaka Mpya wa Kichina, aliunganisha sanaa na kilimo kwa njia iliyovutia wageni katika maonyesho yaliyofanyika kati ya Juni 2 na 4. Sanamu hiyo ilionekana kana kwamba ilikuwa hai kutokana na umbo lake lililoundwa kwa ustadi mkubwa, likiwa na kichwa, manyoya shingoni, mwili na miguu iliyopambwa kwa maua meupe, ya kijani na ya krimu. Ua aina ya gypsophila ndilo lililotumika zaidi kuunda mwili wa farasi huyo, likimpa mwonekano mweupe na laini kama wingu. Muundo huo uliashiria nguvu, kasi na ustahimilivu—sifa zinazohusishwa na farasi katika utamaduni wa Kichina, na pia ukuaji wa kampuni hiyo katika sekta ya maua. "Mwaka huu, 2026, ni Mwaka wa Farasi kulingana na kalenda ya Kichina. Tulitaka kuonyesha nguvu, ukuaji na uvumilivu kama kampuni kupitia maua tunayozalisha wenyewe," alisema Mkurugenzi Mwenza kampuni hiyo, Anjili Shah. Anjili alieleza kuwa wazo hilo lilibuniwa na timu ya kiufundi ya kampuni ikiongozwa na mbunifu mkuu ambaye amekuwa akiandaa mabanda yaliyoshinda tuzo katika maonyesho ya IFTEX kwa miaka kadhaa. Ubunifu huo uliiwezesha Ole Engai Growers kutwaa Tuzo ya Fedha ya Ubora wa Ubunifu (Silver Award for Design Excellence), baada ya mwaka uliopita kushinda tuzo ya banda bora zaidi. [caption id="attachment_190053" align="aligncenter" width="300"] Tuzo ya Ole Engai Growers baada ya kutumia muundo wa farasi wenye mvuto wakati wa Maonyesho ya IFTEX 2026. Picha|Sammy Waweru[/caption] Mwanzilishi mwenza na mkurugenzi wa kampuni hiyo, Sanir Shah, alisema maonyesho hayo yalionyesha uwezo wa kampuni hiyo kuzalisha maua ya kiwango cha juu na kubuni kazi za kipekee bila kutegemea maua kutoka kwa wazalishaji wengine. "Ole Engai Growers huzalisha maua katika shamba lenye ukubwa wa karibu hekta 29 eneo la Kaptagat, Eldoret, Kaunti ya Uasin Gishu," Sanir alifichua. Mbali na gypsophila, kampuni hiyo pia hulima maua aina ya delphinium ya rangi mbalimbali, asters, kangaroo paws, dianthus na kiwi mellow kulingana na mahitaji ya soko. Kulingana na Sanir, kampuni hiyo huuza nje takribani tani 1,200 za maua kila mwaka, masoko makubwa yakiwa Ulaya huku Mashariki ya Kati ikiandikisha ukuaji wa oda. Hata hivyo, alisema sekta hiyo inakabiliwa na changamoto kubwa kutokana na kupanda kwa gharama za usafirishaji wa mizigo kwa njia ya ndege. "Miaka mitano iliyopita tulikuwa tukilipa karibu Dola 1.4 za Amerika kwa kilo moja ya maua kusafirishwa. Sasa gharama imevuka Dola 4 kwa kilo. Hii imeathiri faida yetu," alisema. Baraza la Maua Kenya (KFC), pia, limeeleza kuwa gharama hizo zimeongezeka kutokana na kupanda kwa bei ya mafuta, jambo linaloongeza gharama za usafirishaji wa bidhaa zinazoharibika haraka kama maua. [caption id="attachment_190054" align="aligncenter" width="300"] Ole Engai Growers huzalisha maua katika shamba lenye ukubwa wa karibu hekta 29 eneo la Kaptagat, Eldoret, Kaunti ya Uasin Gishu. Picha|Sammy Waweru[/caption] "Kwa sasa, usafirishaji pekee unachangia zaidi ya asilimia 40 ya gharama zote za kuuza maua nje wakati wa msimu wa mauzo bora," anasema Clement Tulezi, Afisa Mkuu Mtendaji KFC. Aidha, bei ya mbolea imeongezeka kwa karibu asilimia 25 huku gharama za uzalishaji zikiongezeka kwa kati ya asilimia 20 na 30. Changamoto nyingine ni mabadiliko ya tabianchi ambayo yamevuruga ratiba za uzalishaji kutokana na mvua zisizotabirika. Anjili alisema hali hiyo imefanya upangaji wa shughuli za shambani kuwa mgumu zaidi. Licha ya changamoto hizo, Ole Engai Growers inaendelea kupanua uzalishaji na kutafuta masoko mapya, hasa Mashariki ya Kati ya nchi za Uarabuni. Kwa ujumla, sekta ya maua nchini Kenya inaendelea kuwa mhimili muhimu wa uchumi. Mwaka 2025 iliiingizia nchi karibu Dola milioni 845 za Amerika (zaidi ya Sh110 bilioni), huku Kenya ikiendelea kuuza maua katika zaidi ya nchi 60 duniani, asilimia 70 ya mauzo hayo yakielekezwa katika soko la Umoja wa Ulaya (EU).

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Mon, 13 Jul 2026 06:54:54

Upinzani unahitaji umoja thabiti kabla ya 2027 au ikulu isalie ndoto ya mchana

VIONGOZI wa upinzani wanapaswa kusuluhisha mizozo yao na kuendesha mijadala kwa faragha, ili kusitiri mapungufu yanayoweza kudhoofisha taswira yao mbele ya umma. Kwa sasa, misimamo yao imekosa uthabiti katika juhudi za kushughulikia umoja, jambo linalohatarisha mageuzi ya uongozi wa taifa. Takribani kila kiongozi wa upinzani ameonyesha nia ya kugombea urais mnamo 2027. Hali hii inadhihirisha wazi kuwa umoja miongoni mwao bado ni changamoto kubwa katika mikakati ya kukabiliana na Rais William Ruto kwenye kinyang'anyiro cha urais. Iwapo mbinu yao ni kumtangaza mmoja wao baadaye kuwa mgombea wa urais, basi ni vyema waendelee kwa umakini. Lakini iwapo hawana mkakati huo, wanakosea pakubwa, kwani Rais Ruto na kikosi chake wako tayari kutumia udhaifu wao kama daraja la kujipatia ushindi. Upinzani wenye nia ya mageuzi haupaswi kuwa na sauti mbili. Mgawanyiko ndani ya umoja ni hatari. Badala ya mizozo ya vyama, viongozi wanapaswa kutoa suluhu kupitia meza moja ya mazungumzo faraghani. Licha ya vyama vyao kuwa tofauti, viongozi kutoka pembe zote za Kenya wanapaswa kuungana na kuunda muungano mmoja, utakaomteua kiongozi mwenye ushawishi mkubwa zaidi kupambana na Rais Ruto. Hatua ya kila mmoja kuona kuwa anatosha bila kumpa nafasi aliye na nguvu zaidi ni unafiki na ubinafsi unaoweza kusambaratisha upinzani na kumpa Rais Ruto kibarua chepesi. Mfano mzuri ni Jaji Mkuu mstaafu David Maraga, aliyeshirikiana na vuguvugu la Linda Mwananchi katika hafla ya kundi hilo kule Gusii. Sio lazima upinzani ujenge makao yake ndani ya Linda Mwananchi, lakini ni muhimu kutafuta jukwaa linaloweza kuwasetiri ilimradi wawe wamoja. Hatua zinazofaa ni mbili pekee: Muungano wa Upinzani Ulio Ungana au Linda Mwananchi. WAMBULWA ni mwanafunzi wa chuo Kikuu Cha Maseno

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Mon, 13 Jul 2026 07:18:24

Wizara ya Fedha yatakiwa kuondoa VAT kwenye mitambo na mashine za uchakataji mazao

WIZARA ya Kilimo na Maendeleo ya Mifugo inaendelea na mazungumzo na Wizara ya Fedha na Hazina ya Kitaifa ili kuondoa ushuru (VAT) kwenye mitambo ya uchakataji na uongezaji thamani wa mazao ya kilimo, hatua inayolenga kusaidia ukumbatiaji matumizi ya teknolojia, kuongeza uzalishaji na kuboresha ushindani wa bidhaa za Kenya katika soko la kimataifa. [caption id="attachment_190047" align="aligncenter" width="300"] Waziri wa Kilimo Mutahi Kagwe akiendesha trekta aina ya Sonalika wakati wa uzinduzi wake KICC, Nairobi na Elgon Kenya. Picha|Sammy Waweru[/caption] , anasema pendekezo hilo linahusu mitambo inayotumika kuchakata maziwa, chai na mazao mengine ya kilimo. Anasema kupunguza gharama ya kununua vifaa hivyo kutaboresha uwekezaji katika mtandao mzima wa thamani wa sekta ya kilimo. Akizungumza jijini Nairobi majuzi katika hafla ya kampuni ya Elgon Kenya kuzindua usambazaji wa trekta za Sonalika, ukumbi wa KICC, Kagwe alisema matumizi ya teknolojia ya kisasa ni nguzo muhimu katika mpango wa serikali wa kubadilisha kilimo kuwa biashara ya kisasa, yenye faida na inayovutia vijana. "Mbali na matrekta, tunataka pia vifaa vya uchakataji na uongezaji thamani wa mazao viondolewe VAT. Hatua hii itaimarisha biashara ya kilimo, kuongeza ushindani wa bidhaa zetu na kukuza mauzo ya mazao nje ya nchi," alisema. Waziri alibainisha kuwa matrekta tayari hayatozwi ushuru, jambo lililosaidia kupunguza gharama za kuyapata. Kuondoa VAT kwenye mitambo ya uchakataji kutachochea uwekezaji na ukuaji wa viwanda vijijini. Kagwe alisema changamoto kubwa zinazokwamisha matumizi ya teknolojia ni gharama kubwa za mitambo na baadhi ya wakulima kung'ang'ania mbinu za zamani za uzalishaji. "Ndio maana ushiriki wa vijana ni muhimu. Wako tayari kukumbatia teknolojia mpya na mbinu za kisasa za kilimo," alisema. [caption id="attachment_190048" align="aligncenter" width="300"] Dkt Bimal Kantaria, Mkurugenzi Mkuu Elgon Kenya akitazama trekta la Sonalika. Picha|Sammy Waweru[/caption] Kagwe aliongeza kuwa matumizi ya teknolojia na mifumo ya kidijitali yatavutia vijana wanaotazama kilimo kama biashara badala ya shughuli ya kujikimu. Kwa miaka mingi, matrekta mengi yamekuwa yakiuzwa kwa zaidi ya Sh4 milioni, hali inayofanya wakulima wengi kushindwa kuyamudu. Hata hivyo, Kagwe alisema matrekta ya Sonalika yanayouzwa kwa bei ya kuanzia karibu Sh1.4 milioni yataongeza upatikanaji wa teknolojia hiyo kwa wakulima, vyama vya ushirika na biashara za vijijini. Mkurugenzi Mkuu wa Elgon Kenya na Mwenyekiti wa Agriculture Sector Network (ASNET), Dkt Bimal Kantaria, alisema kampuni hiyo inalenga kuwapa wakulima wadogo matrekta bora kwa gharama nafuu. "Sonalika ina zaidi ya matrekta milioni moja yanayotumika duniani, huku India ikizalisha karibu milioni moja kila mwaka," Dkt Kantaria alielezea. Alisema Elgon Kenya imeshirikiana na benki za Equity, Stanbic na Prime kutoa mikopo ya hadi asilimia 90 kununua trekta, hivyo mkulima anaweza kulinunua akiwa na kima cha Sh200,000 huku pesa zilizosalia akilipa mashirika hayo ya kifedha polepole. Aidha, Elgon Kenya inapanga kuanzisha matumizi ya droni na suluhu za kilimo zinazotumia akili bandia (AI), ili wakulima waweze kupata huduma za kisasa kupitia simu za mkononi.

read more