T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Sun, 06 Sep 2026 04:55:13

Siri ya ziara ya Gachagua Amerika

KIONGOZI wa chama cha Democracy for the Citizens Party (DCP), Rigathi Gachagua, anatarajiwa kuanza rasmi shughuli zake za kisiasa nchini Amerika kesho Jumatatu baada ya kukamilisha mapumziko ya siku 10 akiwa pamoja na mkewe, Mchungaji Dorcas Rigathi. Bw Gachagua, ambaye aliondoka nchini Agosti 26 kuelekea Amerika, alisema aliamua kwanza kutumia muda wa faragha na familia kabla ya kuanza mikutano yake ya kisiasa na wafuasi wa chama hicho walio Amerika. Mwanasiasa huyo amekuwa akichapisha picha akiwa na mkewe wakifurahia mapumziko, ikiwemo safari za boti zenye mwendo kasi na matembezi asubuhi.  "Familia ni muhimu sana. Nilihitaji kwanza kupata muda wa kutosha pamoja na mke wangu ambaye ameendelea kunipa nafasi ya kushughulikia siasa nyumbani Kenya. Baada ya mapumziko hayo nitaanza mikutano ya kisiasa kuhusu hali ya nchi, umuhimu wa kujenga DCP, haja ya kuwa na mgombea mmoja wa urais wa upinzani, pamoja na malengo na bajeti yetu," alisema Gachagua.  Kiongozi huyo wa DCP alisema atakuwa na mikutano ya hadhara na ya faragha huku akijaribu kujenga chama chake kama mshirika muhimu katika juhudi za kuleta mabadiliko ya kisiasa nchini Kenya kupitia njia za kidemokrasia. Alisema mojawapo ya malengo yake ni kuhimiza muungano wa upinzani kutafuta viongozi bora watakaowania nyadhifa mbalimbali katika serikali ya kitaifa na za kaunti.  "Nitakutana na wafuasi kutoka Mlima Kenya na sehemu nyingine za nchi. Tumeanzisha sera ya kukusanya wote na kutomtenga yeyote ndani ya DCP. Tunauza maono ya chama na ajenda ya kitaifa kuhusu kwa nini ni muhimu kuondoa Kenya katika hali ya sasa chini ya utawala wa Rais William Ruto. Tuna malengo, mikakati na pia pengo la kifedha ambalo tunahitaji kuziba," alisema. Kwa mujibu wa Gachagua, siku 45 zijazo atakazokuwa Amerika zitalenga kutafuta uungwaji mkono kisiasa na kifedha kutoka kwa Wakenya wanaoishi ughaibuni kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2027. Ratiba iliyotolewa na DCP inaonyesha kwamba hadi Septemba 10 atakuwa katika mji wa Spokane, jimbo la Washington, ambako atahudhuria mikutano ya hadhara pamoja na vikao vya faragha na watu wanaotajwa kuwa muhimu kwa ajenda ya chama.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Sun, 06 Sep 2026 03:55:48

Visiki vya Kalonzo kuingia Ikulu 2027

KINARA wa Wiper Patriotic Front, Kalonzo Musyoka, ana uzoefu, ngome ya kisiasa ya kuaminika na nafasi nzuri katika kinyang'anyiro cha kutafuta mgombeaji urais wa upinzani mwaka 2027. Lakini wachambuzi wa siasa wanasema safari yake ya Ikulu sasa inakabiliwa na mtihani mkubwa. Baada ya miaka mingi akiwa katikati ya siasa za kitaifa, Kalonzo atalazimika kuthibitisha kwamba ana uwezo wa kujenga uungwaji mkono nchini kote, wala si kutegemea hadhi yake au uzoefu au huruma ya kisiasa. Kalonzo alikuwa Makamu wa Rais wakati wa utawala wa marehemu Mwai Kibaki kuanzia 2008 hadi 2013. Pia alikuwa mgombea mwenza wa Raila Odinga katika uchaguzi wa urais wa 2013 na 2017. Hata hivyo, mwaka 2022 Raila aliteua Martha Karua kuwa mgombea mwenza wake. "Historia hiyo imempa Kalonzo uzoefu mkubwa katika kampeni za urais na kujenga miungano ya kisiasa. Lakini 2027 anahitaji kubadilisha historia hiyo ili kuwa kinara wa kivumbi cha urais wa upinzani," asema mchanganuzi wa siasa Dkt Isaac Gichuki. Uchunguzi wa shirika la maoni la Infotrak uliochapishwa Julai ulimweka Kalonzo katika nafasi ya kwanza - asilimia 27 - miongoni mwa wanaotajwa kugombea urais kwa tikiti ya muungano wa upinzani. "Lakini kura hizo pekee haziwezi kumhakikishia tiketi ya upinzani," asema Gichuki. Ngome moja tu Ngome ya Kalonzo imekuwa Machakos, Kitui na Makueni. Kaunti hizo zilikuwa na zaidi ya wapigakura 1.6milioni waliosajiliwa katika uchaguzi wa 2022. Japo wachambuzi wanasema huo ni msingi mkubwa, wanatahadharisha kwamba mgombea urais hawezi kutegemea eneo moja pekee. "Kalonzo atalazimika kutanua ushawishi wake hadi Magharibi, Nyanza, Bonde la Ufa, Pwani, Mlima Kenya, Nairobi na Kaskazini Mashariki," asema mchanganuzi Job Kimanzi.  Changamoto nyingine ni kizazi kipya cha wapigakura. Takwimu za IEBC zinaonyesha vijana ni sehemu kubwa ya wapigakura waliosajiliwa. Maandamano ya Gen Z mwaka 2024 yalionyesha wazi kwamba vijana wanaweza kujipanga kitaifa bila kutegemea vyama vya jadi. Hilo linabadilisha kabisa mchezo wa kisiasa. Kalonzo sasa atalazimika kueleza kwa nini uzoefu wake serikalini unafaa kwa kijana wa miaka 25 anayekabiliwa na ukosefu wa ajira, kodi kubwa na gharama ya maisha. Ushindani upinzani Kalonzo pia anakabiliwa na ushindani kutoka kwa vigogo wenza wa upinzani wanaojikuza. Gachagua amekuwa akifanya mikutano ya kisiasa na mashauriano katika maeneo mbalimbali, huku pia akilenga Wakenya wanaoishi nje ya nchi. Kwa upande mwingine, kundi la Linda Mwananchi linaloongozwa na Sifuna limechagua mkakati wa kufika mashinani. Kundi hilo limefanya mikutano Magharibi, Nyanza, Pwani na hivi karibuni Meru. Kalonzo naye ameanzisha jukwaa la kidijitali la Komboa Kenya, akazindua Bajeti ya Mwananchi na kufanya kampeni katika baadhi ya maeneo nje ya Ukambani. Amefanya pia mikutano na viongozi wa Linda Mwananchi. Hata hivyo, kasi ya shughuli hizo ndiyo itakuwa muhimu. Mgombea urais hawezi kuonekana kutumia muda mwingi kujadili uundaji miungano kuliko kukutana na wapigakura nyanjani. Vijana na siasa mpya Maandamano ya 2024 yalionyesha kuwa siasa za Kenya zinaingia katika awamu mpya. Vijana walijipanga kupitia mitandao ya kijamii na majukwaa mengine bila kutegemea miundo ya vyama vya kisiasa. Maandamano hayo yalifika kaunti nyingi nchini na kuibua masuala ya gharama ya maisha, ukosefu wa ajira, ufisadi na kutengwa kwa vijana katika maamuzi ya nchi. Kwa Kalonzo, hii ina maana kuwa uzoefu wake wa kisiasa pekee hautoshi. Anahitaji sera zinazogusa maisha ya vijana. Ajira, teknolojia, biashara, elimu, uwajibikaji na mageuzi ya taasisi zinapaswa kuwa sehemu ya ujumbe wake. Zaidi ya hayo, vijana wanataka nafasi ya kushiriki katika siasa, si kuwa watazamaji au wapigakura wakati wa uchaguzi pekee. Kalonzo anaweza kufaidi kutokana na uzoefu wake, ngome ya kisiasa na nafasi yake katika kura za maoni. Lakini hakuna moja kati ya mambo hayo yanampa tikiti ya urais moja kwa moja. Anahitaji kuonyesha kwamba anaweza kupata kura nje ya Ukambani. Anahitaji kujenga miundo ya Wiper katika maeneo mapya, kuvutia viongozi wenye ushawishi na kuonyesha kuwa chama kina uwezo wa kupiga kampeni ya kitaifa. Upinzani nao unahitaji kuchagua mgombea kwa kuangalia uwezo wa kufika maeneo mengi, nguvu za mashinani, uwezo wa kujenga miungano, sera na uwezo wa kuvutia wapigakura ambao bado hawajaamua. Uzoefu wa Kalonzo akiwa makamu wa rais ni wa kuendesha serikali. Ngome yake ya kisiasa inampa nguvu ya kuketi meza ya kujenga. Kura za maoni zimempa mwanzo mzuri. Lakini hayo yote hayatoshi. Muda wa kulinda ngome, kufikia wapigakura wasio na msimamo, kushawishi vijana na kupanua Wiper kote nchini ni sasa. Aliyekuwa Waziri wa Usalama Fred Matiang'i alikuwa na asilimia 26, Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna asilimia 19, huku aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua akiwa na asilimia tisa.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Sun, 06 Sep 2026 02:55:52

IEBC inavyojiandaa kwa uchaguzi wa 2027

TUME Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) imeingia katika awamu muhimu ya maandalizi ya uchaguzi mkuu wa 2027 huku ikiwa na chini ya mwaka mmoja kuhakikisha changamoto zilizopo zinatatuliwa. Mwenyekiti wa IEBC, Erastus Ethekon, amesema tume hiyo inaendelea na maandalizi mbalimbali, ikiwemo usajili wa wapigakura, teknolojia, ununuzi wa vifaa, elimu ya wapigakura, usafirishaji, kuajiri na kuwapa mafunzo maafisa wa uchaguzi. Bw Ethekon alisema tume hiyo tayari imeanza michakato mikuu ya ununuzi wa teknolojia, karatasi za kura na vifaa vingine vitakavyohitajika katika uchaguzi. Alisema awamu ya kwanza ya Usajili Endelevu wa Wapigakura ilisajili wapigakura wapya milioni 2.3 dhidi ya lengo la milioni 2.5. Kufikia Agosti 17, 2026, jumla ya wapigakura wapya 2,920,600 walikuwa wamesajiliwa, huku IEBC ikilenga kuwa na orodha ya wapigakura takriban milioni 28.5 mwaka 2027. Hata hivyo, tume hiyo inakabiliwa na changamoto kadhaa, zikiwemo ukosefu wa fedha, ucheleweshaji wa sheria muhimu na wasiwasi kuhusu vurugu za kisiasa. Katika mahojiano na Taifa Jumapili, Bw Ethekon alisema tume hiyo inahitaji hadi Sh35 bilioni kukamilisha maandalizi yake. Kuhusu madai ya upendeleo katika zabuni ya teknolojia, mwenyekiti huyo alisema hakuna kampuni ambayo imeshinda zabuni hiyo. Alisema mchakato wa ununuzi unaendelea kwa kuzingatia Katiba na sheria za ununuzi wa umma. "Kufikia sasa, hakuna zabuni iliyotolewa kwa kampuni yoyote," alisema. Alisema maamuzi ya mwisho yatafanywa baada ya mchakato wa wazi na wa uwazi kukamilika. Kuhusu madai ya upinzani kwamba IEBC inaegemea upande wa serikali, Bw Ethekon alisema tume hiyo haiwezi kuendeshwa kwa matakwa ya wanasiasa. "Wajibu wetu si kufurahisha serikali, upinzani, vyama vya kisiasa au mtu yeyote. Wajibu wetu ni kwa Katiba na watu wa Kenya," alisema. Kuhusu gharama ya uchaguzi, Bw Ethekon alisema Kenya ina mfumo wa kipekee kwa sababu chaguzi sita hufanyika siku moja; wa Rais, Bunge la Kitaifa, Seneti, ugavana, Mwakilishi wa Wadi na mwakilishi wa wanawake. Alisema gharama hizo pia zinahusisha usafirishaji, teknolojia, karatasi za kura, maafisa wa uchaguzi, elimu ya wapigakura, usalama na vifaa. "Tunaomba rasilimali zinazohitajika kuendesha uchaguzi unaotakiwa na Katiba," alisema. Kuhusu kuchelewa kwa maandalizi, mwenyekiti huyo alisema IEBC haijafikia hatua ya hofu, lakini muda sasa unapaswa kuchukuliwa kama rasilimali muhimu ya kitaifa. "Je, tuna wasiwasi? Tuko macho. Je, tunaingiwa na hofu? Hapana," alisema. Alisema kuchelewesha maamuzi muhimu kunaweza kuathiri majaribio ya teknolojia, usambazaji wa vifaa, mafunzo na maandalizi ya dharura. Bw Ethekon pia alikiri kuwa vijana wamepoteza imani kwa taasisi za uchaguzi, akisema IEBC lazima itumie njia mpya kuwafikia. Alisema vijana wanahitaji taarifa za wazi na fursa za kuwasiliana na tume hiyo mara kwa mara, si wakati wa uchaguzi pekee. "Imani hujengwa kupitia matendo," alisema

read more