T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Fri, 17 Jul 2026 04:13:28

Raia 7 wa Amerika wanaougua Ebola wawekwa karantini nchini Kenya

WAAMERIKA saba wa shirika la misaada wanaougua Ebola wamewekwa kwenye kituo cha karantini nchini Kenya, ripoti iliyochapishwa kwenye shirika la habari la kimataifa Reuters imeonyesha. Kulingana na ripoti hiyo, afisa mkuu wa shirika la Samaritan's Purse Franklin Graham ananukuliwa akithibitisha habari hizo akisema hatua hiyo imetokana na vikwazo vya kiusafiri vilivyowekwa na utawala wa Rais Donald Trump kuhusu raia walioambukizwa wanaorejea nyumbani. Habari hizi zinaweza kugutusha Wakenya wengi ambao wamekuwa wakipinga kuanzishwa kwa kituo cha karantini ya Ebola nchini kwa misingi kwamba hatua hiyo italeta ugonjwa huo hatari katika ardhi ya Kenya ambayo haijawahi kuthibitisha kuweko kwa maradhi hayo, na pia kwamba mifumo ya afya huenda isiwe thabiti kiasi cha kuweza kupambana na msambao wa maradhi hayo. Kumekuwa pia na kesi mahakamani ambapo Waziri wa Afya Aden Duale aliitwa kuthibitisha kwamba ujenzi wa kituo cha karantini uliokuwa umeanzishwa katika kambi ya kijeshi ya Nanyuki, Laikipia umethibitishwa. Bw Duale alikuwa ameshutumiwa na korti kwa kupuuza maagizo ya kusitisha ujenzi huo hadi kesi iliyowasilishwa na kupinga ujenzi huo kusikizwa na kuamuliwa. Mahakama ilikuwa tayari kutoa adhabu kwa Bw Duale ila ikabadili nia pale waziri alipowasilisha stakabadhi kuthibitishia mahakama kwamba imetekeleza maagizo ya kusitisha ujenzi wa karantini hiyo. Awali, utawala wa Rais Trump kupitia ripoti mbali mbali ulikuwa umesisitiza kwamba utaheshimu maamuzi ya korti ya kutojenga kituo cha karantini na kutuma raia wake wanaougua nchini Kenya. Hata hivyo, Rais William Ruto amekuwa akitetea ujenzi wa kituo cha Laikipia, akisema hicho kilikuwa kimoja kati ya vituo vingine vilivyokuwa vinajengwa nchini na kwamba Kenya ina jukumu la kuwa rafiki mwema wa kusaidia raia wa Amerika walioambukizwa, akisema pia ujenzi wenyewe ulikuwa unafanywa kwa pesa za Amerika.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Fri, 17 Jul 2026 02:55:24

Mtoto kukojoa kitandani baada ya miaka mitano si jambo la kupuuzwa – Wataalamu

KWA miaka mingi, Monica (si jina lake halisi) aliamini kuwa mtoto kukojoa kitandani ni jambo la kawaida. Lakini mtazamo huo ulibadilika baada ya kifungua mimba wake ambaye alikuwa ameacha kukojoa kitandani akiwa na umri wa miaka mitatu, kurejea tabia hiyo alipokuwa katika darasa la sita. "Nilishtuka sana. Hii ni kwa sababu, nilijua amekomaa na kwamba hangesumbuliwa na tatizo kama hilo," alisema mwanamke. Monica anasema hali hiyo iliandama wanawe wengine jambo lililomfanya aanze kujiuliza ikiwa kuna tatizo la kiafya lililokuwa limejificha. "Nyumbani tulikuwa tunachukulia jambo hili kuwa la kawaida. Lakini nilipowapeleka katika shule za bweni ndipo niligundua uzito wake kwa sababu walikuwa wakikumbana na dhihaka na kuchekwa na wenzao shuleni jambo ambalo lilinisumbua msno," anasema. Anasema wasiwasi wake uliongezeka zaidi alipopigiwa simu kutoka shuleni na kuarifiwa kuwa mwanawe mwenye umri wa miaka 17 bado alikuwa anakojoa kitandani. "Nilihofia unyanyapaa huu unaweza kuathiri hali yake ya kisaikolojia na hata masomo yake," anaongeza. Licha ya kuchunguza historia ya familia bila kupata mtu mzima aliyewahi kuwa na tatizo hilo, Monica anasema bado ana hofu kwamba kitinda mimba wake anaweza pia kurejea tatizo hilo la kukojoa kitandani miaka ijayo kama ndugu zake. Daktari bingwa wa watoto waliobalehe katika Hospitali ya Aga Khan, Dkt Njeri Karianjahi, anasema mtoto anapoendelea kukojoa kitandani baada ya kutimiza miaka mitano, hasa ikiwa alikuwa ameacha na baadaye akarudia, hali hiyo haipaswi kupuuzwa. Anasema wazazi wanapaswa kumpeleka mtoto huyo hospitalini ili afanyiwe uchunguzi wa kina kubaini chanzo cha tatizo. "Kwanza tunachunguza mara ngapi mtoto anakojoa kitandani, kama ana maumivu wakati wa kukojoa, ana hisia za kutaka kukojoa mara kwa mara, pamoja na ubora wa usingizi wake," anaeleza. Kwa mujibu wa Dkt Karianjahi, uchunguzi wa mwili husaidia kubaini iwapo kuna dalili zinazoweza kuashiria tatizo kwenye mfumo wa mkojo au mfumo wa neva. Aidha, uchunguzi wa mkojo hufanywa kubaini iwapo kuna maambukizi, huku vipimo vya figo vikifanywa endapo kuna wasiwasi kuhusu utendakazi wake. "Vipimo hivi hutusaidia kutofautisha mtoto ambaye hakuwahi kukamilisha hatua ya kudhibiti mkojo na yule ambaye alianza kukojoa tena baada ya kuacha kabisa," anasema. Jane (si jina lake halisi) pia anakiri kuwa binti yake mwenye umri wa miaka 16 bado anakabiliwa na changamoto hiyo.Anahisi usingizi mzito ndio unaomfanya ashindwe kuamka kwenda msalani usiku. "Alipokuwa na umri wa kati ya miaka sita na 11 alikuwa anakojoa karibu kila usiku kitandani. Sasa hali imepungua na kuna usiku ambapo hakoji kabisa," anasema. Yeye na mumewe wamekuwa wakimuamsha mara tatu kila usiku ili aende msalaani kabla. "Niliwahi kumpeleka hospitalini lakini hatukupata dawa yoyote. Kwa sasa tunaendelea na utaratibu wa kumuamsha usiku, jambo ambalo linasaidia kwa kiasi," anaeleza. Sababu zinazochangia Kwa mujibu wa Dkt Karianjahi, hali ya kukojoa kitandani usiku (nocturnal enuresis) inaweza kusababishwa na sababu mbalimbali, hivyo haiwezi kutibiwa bila uchunguzi wa kina. Anasema watoto wadogo hukosa uwezo wa kudhibiti mkojo kikamilifu na ndiyo maana wanaweza kukojoa hadi mara 15 au 20 kwa siku. "Mtoto anavyoendelea kukua, mawasiliano kati ya ubongo, uti wa mgongo na mfuko unaobeba mkojo huimarika na hivyo uwezo wa kudhibiti mkojo huongezeka," anasema. Hata hivyo, kwa baadhi ya watoto mfumo huo hukomaa polepole au huathiriwa na matatizo mengine ya kiafya, jambo linalowafanya waendelee kukojoa kitandani hata baada ya kubalehe. Utafiti uliochapishwa mwaka 2025 na kampuni ya Adisu unaonyesha kuwa takriban asilimia 7.2 ya watoto na vijana duniani bado hukumbwa na tatizo la kukojoa kitandani. Mazingira na afya ya akili pia huchangia Mtaalamu wa maendeleo ya watoto, vijana na jamii kutoka Koinonia Community, Jack Matika, anasema mazingira ambayo mtoto anakulia yanaweza pia kuchangia tatizo hilo. Anasema watoto wanaolelewa katika mazingira yasiyo salama wanaweza kuzoea kukojoa walipo badala ya kutoka nje usiku kwa hofu ya usalama wao. "Kwa mfano, watoto wanaoishi mitaani huwa na mazoea hayo kutokana na mazingira wanayoishi. Hata wanaporejea katika familia au vituo vya malezi, huwa vigumu kuacha tabia hiyo bila msaada wa kitaalamu," anaeleza. Jack pia anasema msongo wa mawazo na tatizo la kisaikolojia yanaweza kuwa sababu ya watoto au vijana kuendelea kukojoa kitandani. "Baadhi ya watoto waliowahi kudhulumiwa au kupitia matukio ya kutisha huendelea kupata changamoto hii. Msongo wa mawazo unaweza kuathiri namna ubongo, uti wa mgongo na mfuko unaobeba mkojo vinavyowasiliana," anasema. Kwa sababu hiyo, anasisitiza kuwa wazazi wasiwadharau wala kuwaadhibu watoto wanaopitia hali hiyo, bali wawatafutie matibabu mapema. Wataalamu wanashauri wazazi kuwapeleka watoto hospitalini ikiwa bado wanakojoa kitandani baada ya kutimiza miaka mitano au ikiwa walikuwa wameacha lakini wakaanza tena. Mbali na matibabu, hatua zinazoweza kusaidia ni pamoja na kupunguza kunywa maji saa chache kabla ya kulala, kuhakikisha mtoto anaenda msalani kabla ya kulala, pamoja na kumuamsha mara moja usiku. Hata hivyo, wataalamu wanatahadharisha kuwa hatua hizi hazipaswi kuchukua nafasi ya uchunguzi wa kitaalamu, hasa iwapo tatizo linaendelea kwa muda mrefu au limeanza tena baada ya mtoto kuwa ameacha kabisa kukojoa kitandani. Kwao, kukojoa kitandani baada ya umri wa miaka mitano si tabia ya uvivu wala ukaidi, bali ni ishara inayoweza kuonyesha tatizo la kiafya au la kisaikolojia linalohitaji kutambuliwa na kutibiwa mapema.

read more