T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Sat, 18 Jul 2026 01:55:05

Matiang'i awaonya viongozi dhidi ya kufadhili wahuni

NAIBU Kiongozi wa Chama cha Jubilee, Dkt Fred Matiang'i, ameonya kuwa Kenya iko katika hatari kutokana na uhuni wa kisiasa. Aliwataka viongozi kuacha kufadhili makundi ya wahuni na kukemea ghasia za kisiasa ambazo amesema zimesababisha vifo vya watu wasio na hatia katika maeneo mbalimbali nchini. "Katika historia ya siasa za Kenya hatujawahi kushuhudia kiwango hiki cha vurugu za kisiasa zikifanywa na viongozi wanaohusishwa na serikali," alisema. Dkt Matiang'i alitoa kauli hiyo alipozuru maeneo ya Keumbu katika eneo la Nyaribari Chache, Gionseri, Bobasi na Nyamokenye, Kaunti ya Kisii. Alisema siasa hazipaswi kuwagawanya Wakenya na kwamba wanaofadhili makundi ya wahuni wanapaswa kukumbuka kuwa Kenya lazima ibaki na umoja kabla, wakati na baada ya uchaguzi mkuu wa 2027. Akirejelea uzoefu wake alipokuwa Waziri wa Usalama wa Ndani, Dkt Matiang'i alihoji kwa nini serikali imeshindwa kutekeleza wajibu wake wa kikatiba wa kulinda maisha na mali ya wananchi. "Serikali ina rasilimali za kutosha na taarifa za kijasusi za kufuatilia, kusaka na hata kuteka wakosoaji wa kisiasa, lakini inadai haina uwezo wa kuwazuia wahuni wanaotembea hadharani wakiwa na silaha kuwashambulia wananchi," alisema. Aliongeza kuwa mashambulizi hayo hayawezi kutokea bila viongozi wa usalama wa eneo husika kujua au kuhusika. Pia aliwaonya wanasiasa wanaowaajiri na kuwatuma wahuni kufanya mashambulizi akisema wanacheza mchezo hatari ambao utawageukia siku zijazo. "Vurugu zikizidi na kushindwa kudhibitiwa, wale wahuni mnaolea watawageukia. Hakuna atakayekuwa salama, hata walio madarakani wenye ulinzi mkali," alisema. Dkt Matiang'i aliwahimiza wananchi na viongozi wa dini kukataa fedha za kisiasa na "fedha zilizochafuliwa na damu" zinazotumiwa kuwashawishi vijana kujiunga na makundi ya wahuni. Akizungumzia mashambulizi yaliyotokea Keumbu wiki mbili zilizopita, alisema ameunda timu ya mawakili na wataalamu wa teknolojia kukusanya ushahidi na taarifa zitakazotumika kushtaki waliohusika. Alisema timu hiyo inachambua video za shambulio hilo ili kubaini wahusika pamoja na wafadhili wao wa kisiasa na kuhakikisha wanachukuliwa hatua za kisheria. "Nimekuja Keumbu kulaani vikali vitendo vya uvunjaji sheria dhidi ya Wakenya wasio na hatia. Ninawasihi watu wa Gusii kudumisha uvumilivu ambao ndio msingi wa demokrasia yetu," alisema. Dkt Matiang'i alitembelea Keumbu ambako viongozi wa mrengo wa Linda Mwananchi walivamiwa wiki mbili zilizopita katika tukio lililosababisha kuuawa kwa Vincent Osiemo maarufu kama Mapinduzi. Baadaye alihudhuria mazishi ya Osiemo huko Gionseri, Bobasi, ambako alitoa wito wa umoja miongoni mwa jamii ya Wagusii. Aidha, alisema uchaguzi mdogo wa Ol Kalou umefungua ukurasa mpya katika siasa za Kenya. "Nmpongeza ndugu yangu Rigathi Gachagua, chama cha DCP, hasa Seneta Methu na timu yake ya Ol Kalou, kwa ushindi huo wa kihistoria," alisema.

read more

Other Headlines


T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo 31 minutes ago

NCIC yasema itaendelea kufuatilia matamshi ya Duale, Gachagua na wengine sita

TUME ya Kitaifa ya Uwiano na Utangamano (NCIC) imesema itaendelea na uchunguzi dhidi ya Waziri wa Afya Aden Duale na aliyekuwa Naibu wa Rais Rigathi Gachagua kuhusu matamshi ya chuki na uchochezi wa kikabila, licha ya wawili hao kutangaza hadharani kwamba hawataitikia wito wa tume hiyo. Mwenyekiti wa NCIC Askofu Kepha Nyamweya, alisema tume hiyo haitaruhusu wanasiasa kuamua namna uchunguzi wake unavyofanywa na kwamba itaendelea kutekeleza wajibu wake bila uoga, upendeleo wala msukumo wa kisiasa. "Kuna wakati wa siasa na kuna wakati wa kazi na hatuwezi kuruhusu mchezo wa aina hiyo. Mtu hawezi kusema atafika mbele ya tume baada ya mwingine kufika. Tutafanya kazi yetu kwa mujibu wa sheria," akasema Bw Nyamweya. Kauli hiyo ilijiri baada ya Bw Duale kusema hatafika mbele ya NCIC hadi pale Bw Gachagua atakapoitwa kwanza kujibu matamshi yake yaliyofasiriwa kuwa ya uchochezi. "Kama hakuna Gachagua, hakuna Duale," alisema waziri huyo, akisisitiza kuwa sheria inapaswa kutumika kwa usawa kwa wote. Hata hivyo, Bw Nyamweya alisema watu wanaochunguzwa hawawezi kuielekeza tume yake jinsi ya kutekeleza majukumu yake. "Tunatoa wito kwa wanaohitajika kufika mbele yetu. Wakikosa kufika, sheria imeweka utaratibu wa kushughulikia hali hiyo. Tutachukua hatua bila mapendeleo," akaongeza. Kwa upande wake, Bw Gachagua ameendelea kutetea matamshi yake aliyosema "watamuua nyoka pamoja na mayai yake," akidai yalikuwa ya kimethali, yakimaanisha kuwashinda kisiasa Rais William Ruto na washirika wake kupitia kura, wala si kutumia vurugu. Alisema iwapo NCIC inahitaji maelezo yake, imuandikie rasmi naye atajibu. Mbali na viongozi hao wawili, NCIC pia imeanzisha uchunguzi dhidi ya Waziri wa Utumishi wa Umma Geoffrey Ruku, Gavana wa Busia Paul Otuoma, Naibu Gavana wa Mandera Ali Maalim Mohamud, Mbunge wa Sirisia John Waluke pamoja na Tipape Naini Musa na Dkt Dennis Adison Ouma kwa madai ya matamshi ya chuki na uchochezi. Tume imesisitiza kuwa wote wanaochunguzwa wanachukuliwa kuwa hawana hatia hadi uchunguzi utakapokamilika. Nyamweya alionya kuwa matamshi ya kisiasa nchini yanazidi kuwa makali huku baadhi ya viongozi wakitumia lugha inayowagawa wananchi kwa misingi ya kikabila badala ya kushindana kwa sera. "Lugha inatumiwa kuwafanya wapinzani waonekane maadui badala ya majirani wenye mitazamo tofauti. Hali hii inaweza kuhatarisha umoja wa taifa," alisema. Alieleza kuwa NCIC imepewa mamlaka chini ya Sheria ya Uwiano na Utangamano ya kuchunguza matamshi ya chuki, kuwaita mashahidi, kukusanya ushahidi na kuwasilisha faili kwa Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP) kwa hatua zaidi. Bw Nyamweya alikanusha madai kwamba tume hiyo inaweza kushinikizwa kisiasa, akisema itaendelea kutekeleza wajibu wake kwa haki huku ikishirikiana na Baraza la Kidini Kenya kuimarisha juhudi za kuzuia matamshi ya chuki na kuhakikisha uchaguzi wa 2027 unafanyika kwa amani.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo 1 hours ago

Dalili Nyayo za Kijana Wamalwa na Raila zinamwongoza Sifuna

SENETA wa Nairobi, Edwin Sifuna anaendelea kutamba katika ulingo wa siasa. Nyota yake Sifuna inaendelea kung'aa kwenye ramani ya humu nchini kwa mwendokasi wa ajabu. Sifuna ni mwanafunzi mmakinifu wa siasa za watangulizi wake Raila Amollo Odinga na kigogo wa siasa Michael Kijana Wamalwa ambao walionyesha umahiri hata katika wimbi kali la upinzani. Baada ya kubanduliwa katika wadhifa wa katibu mkuu wa chama cha ODM, Seneta Sifuna hajafa moyo. Ufuasi wake Unaendelea kushamiri huku akifanikiwa kupata kibali katika kila eneo analozuru nchini. Hili linashuhudiwa kupitia umati wa watu wanaojitolea kuhudhuria mikutano anayoandaa pamoja na wenzake katika mrengo wa Linda Mwananchi. Safari yake Sifuna katika siasa ni sura ya siasa ya aliyekuwa waziri mkuu na kinara wa ODM Raila Odinga. Raila ndiye mwanasiasa wa pekee aliyelipinga wimbi la chama kikuu cha upinzani cha FORD katika mwaka wa 1994 na baadaye kujiuzulu. Raila alithamini demokrasia na nguvu za wananchi zaidi ya nguvu za dola. Sifuna amehitimu katika chuo cha mwamba aliyegundua kuanza mapema akiwa na nguvu na mvuto kwa wananchi. Hulka yake seneta huyo inachukuliana na yake Kijana Wamalwa ambaye alipendwa na wengi wa wapigakura katika ukanda wa magharibi. Ni wazi kuwa Sifuna ni mmoja wa viongozi walioweza kuwavutia wananchi wengi zaidi kisiasa katika eneo la Magharibi. Siasa yake inatikisa ngome za wanasiasa wakongwe wakiwemo Musalia Mudavadi, Moses Wetang'ula, Wycliffe Oparanya na wengine. Mvutano kati ya Raila na Wamalwa ulichangia FORD Kenya kusambaratika baada ya Jaramogi Oginga kufariki dunia. Raila alionekana kama aliyetaka kurithi chama naye Wamalwa akitaka kuwa kiongozi wa chama hicho. Hatimaye Ford Kenya iligawanyika mara tatu. Hii ndiyo njia ya chama cha ODM baada ya Raila kuondoka. Sharti Sifuna ajichongee kao lake la siasa kwa nyakati zijazo akifahamu kuwa ufuasi na ushabiki humwandama mtu jasiri anayejijengea chama chake. Raila aliviunda vyama kadhaa kama silaha yake dhidi ya serikali. Ni bayana kuwa Sifuna yuko njiani kukiunda chama chake. Tukielekea katika uchaguzi mkuu wa 2027, Sifuna ana nafasi murua ya kujinadi kupewa fursa ya kugombea kiti cha urais au kumpiga pambaja mgombea mwingine kuwania kiti hicho. Kibarua kikubwa ni kuwa kuna wanasiasa wa upinzani ambao huenda hawatampa nafasi hiyo kwa madai ya kukosa tajriba ya kisiasa. Kinachobakia ni kujijenga kisiasa wala si kutafuta ushindi wa kiti cha urais. Kadi yake Sifuna kama mgombea wa urais ni bora hasa kwa ushawishi alio nao kwa vijana na wananchi wanaotaka mabadiliko. Hata hivyo, haijadhihirika iwapo viongozi katika upinzani watakubali kumuunga mkono ama ukosefu wa umoja katika upinzani utalemaza uwezo wake. Sifuna hana la kupoteza upinzani ukishinda au ukikosa kushinda urais. Atakuwa ameuboresha msingi wake wa kisiasa kwa siku za usoni.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo 2 hours ago

Kindiki kona mbaya tishio kutoka pande tatu zikimuandama

NAIBU wa Rais Prof Kithure Kindiki anakabiliwa na mtihani mkubwa wa kisiasa huku mjadala kuhusu iwapo atasalia mgombeaji mwenza wa Rais William Ruto katika Uchaguzi Mkuu wa 2027 ukizidi kushika kasi na kuzua maoni mseto. Japo amehudumu kwa chini ya miaka miwili tangu achukue nafasi hiyo, Prof Kindiki sasa ana kibarua cha kupambana na changamoto kutoka pande tatu zinazotishia mustakabali wake kisiasa. Mtihani wa kwanza unatokana na aliyekuwa Naibu wa Rais Rigathi Gachagua, ambaye ameanzisha kampeni kali katika ukanda wa Mlima Kenya Mashariki, ngome ya kisiasa ya Profesa Kindiki. Baada ya ushindi wa chama chake katika uchaguzi mdogo wa Ol Kalou, Bw Gachagua ameahidi kufuatilia kila ziara ya Rais Ruto katika eneo hilo kwa mikutano ya kisiasa akinuia kupunguza ushawishi wa serikali kabla ya uchaguzi wa mwaka ujao. Tangu ateuliwe naibu rais (DP), Prof Kindiki amekuwa akiongoza hafla za kufungua miradi ya maendeleo katika eneo hilo ikiwemo uzinduzi wa barabara, nyumba za gharama nafuu na hata miradi ya kilimo. Baadhi ya wafuasi wake wanasema ziara hizo zimedumisha imani ya wakazi kwamba eneo la Mlima Kenya bado lina sauti serikalini, ila Bw Gachagua anataka kuhakikisha imani hiyo haigeuki kuwa kura kwa Kenya Kwanza 2027. Kibarua cha pili kinatokana na siasa ambazo zinaendelea ndani ya Kenya Kwanza baada ya ushirikiano mpya na ODM. Hii ni kwa sababu viongozi wa ODM wameweka wazi kuwa wanataka nafasi ya naibu rais ikiwa ushirikiano wao na UDA utaendelea kabla na baada ya uchaguzi wa 2027. Baadhi ya viongozi wa chama hicho, akiwemo Naibu Kiongozi Simba Arati na Kiongozi wa Wachache katika Bunge la Kitaifa Junet Mohamed, wamesema nafasi hiyo inapaswa kutolewa kwa ODM. Chama hicho kimewataja Gavana wa Homa Bay Gladys Wanga, Waziri wa Madini Hassan Joho na Wycliffe Oparanya kama wanaotosha kuwa mgombeaji mwenza wa Rais Ruto. Wadadisi wa masuala ya kisiasa wanasema msukumo wa ODM unamweka Profesa Kindiki katika hali ngumu kwa sababu Rais Ruto anaweza kulazimika kutathmini kusalia naye au kumwondoa na kutumia nafasi hiyo kuimarisha ushirikiano na ODM. Prof Kindiki amejipata katika hali ngumu zaidi baada ya taarifa kudai kuwa baadhi ya majukumu yaliyokuwa yakihusishwa na afisi ya naibu rais yamehamishiwa kwa Kinara wa Mawaziri Musalia Mudavadi. Hata hivyo, Prof Kindiki amekanusha madai hayo na kuyataja kuwa habari za uongo. Mkuu wa Uchumi wa Ubunifu na Miradi Maalum katika Afisi ya Rais Dennis Itumbi naye alisisitiza kuwa majukumu ya kila afisi yamebainishwa kwenye Katiba na sheria, na hakuna mamlaka yaliyoondolewa kutoka kwa Naibu Rais. Licha ya magumu yanayomkabili Profesa Kindiki, wadadisi kadhaa wa kisiasa wanaamini bado ndiye chaguo bora zaidi kwa Rais Ruto. Wanasema ameonyesha uaminifu, utulivu, uwezo na amekuwa akiepuka migogoro ya hadharani na rais, tofauti na waliomtangulia. Mdadisi wa masuala ya kisiasa Steve Ngari anasema Profesa Kindiki ameonyesha sifa zinazotarajiwa kwa afisi yake na anafaa kuendelea kusalia katika kambi ya Rais. Aidha, kura za maoni za Infotrak zimemweka Prof Kindiki kileleni mwa wanaopendelewa kuwa mgombea mwenza wa Rais Ruto kwa asilimia 34, akifuatiwa na Gladys Wanga kwa asilimia 11 na Oburu Oginga kwa asilimia tano. Kwa mujibu wa Bw Ngari, kumwondoa Prof Kindiki kunaweza kuwakera wapigakura wa Mlima Kenya Mashariki ambao wanaona nafasi ya naibu rais kama ishara ya ushawishi wao serikalini. "Kazi ya Naibu Rais ni kuhudumu kama msaidizi wa karibu wa Rais. Kindiki ameonyesha sifa ambazo zinamwezesha kuendelea kuhudumu kwa wadhifa," akasema Bw Ngari. Pia, kunaweza kuibua taswira kwamba uaminifu na utendakazi hauthaminiwi ndani ya Kenya Kwanza. Waziri wa Utumishi wa Umma Geoffrey Ruku naye ameendelea kumtetea Prof Kindiki, akisisitiza kuwa hakuna nafasi iliyo wazi ya naibu rais na kwamba, Rais Ruto tayari ameamua mgombea wake mwenza.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo 13 hours ago

Chelsea yahemea saini za wakongwe

CHELSEA inaonekana kubadili mbinu yake ya usajili wa wachezaji baada ya kuelekeza macho kwa wachezaji wazoefu wenye umri uliokomaa. Hii ni baada ya klabu hiyo ya Stamford Bridge kutupia ndoano difenda wa Crystal Palace Maxence Lacroix, straika wa Brighton Danny Welbeck na kiungo wa kati wa Brentford Jordan Henderson. Hatua hiyo ni tofauti na mwelekeo waliochukua miaka minne iliyopita wa kusajili wachezaji chipukizi kwa mikataba mirefu. Baada ya klabu hiyo kununuliwa na BlueCo mwaka 2022, Chelsea ilitumia fedha nyingi kusajili nyota waliokuwa tayari wamejijengea majina makubwa. Raheem Sterling aliwasili kutoka Manchester City akiwa na miaka 27, Kalidou Koulibaly (31) alitua kutoka Napoli ya Italia huku Pierre-Emerick Aubameyang (33) akiingia kutokea Barcelona ya Uhispania. Lakini ukosefu wa mataji ulimgarimu kocha Thomas Tuchel kazi yake. Wakati wa kipindi kirefu cha uhamisho 2022 wamiliki wa BlueCo walipiga abautani kugeukia chipukizi. Aliyefungua ukurasa huo ni Enzo Fernandez kisha wakafuata mastaa wengine ikiwemo Moises Caicedo na Cole Palmer ambao wameonyesha ukwasi wao kwa kiwango fulani. Hata hivyo, kulikuwepo pia mastaa walioishia kuwa moto wa karatasi - Mykhailo Mudryk, Joao Feli na Wesley Fofana. Sasa baada ya miaka minne ya kukamata nafasi ya 12, sita, nne na 10 msimu jana pamoja na mataji 'madogo ya Conference League na Kombe la Klabu Bingwa Duniani, wamiliki wamegeukia tena mastaa wakongwe wenye uzoefu. Lacroix 26, ndiye mwenye umri mdogo kati ya watatu hao kwani Welbeck ana umri wa miaka 35 naye Henderson miaka 36. Chelsea inasemekana kuwa tayari kutoa Pauni milioni 52 (Sh9.2 billioni) kumsajili Lacroix. Naye Welbeck anaripotiwa kuwa tayari kujiunga na miamba hao kwani amebakisha mwaka mmoja pekee katika mkataba wake Brighton. Iwapo Welbeck atatua Chelsea huenda akachukua nafasi ya Liam Delap, 23, ambaye alisajiliwa kutoka Ipswich Town mwaka jana akiwa mmoja wa washambuliaji waliopigiwa upatu mkubwa kung'ara. Kocha mpya Xabi Alonso, ambaye amewasili kutoka Bayer Leverkusen ya Ligi Kuu ya Ujerumani (Bundesliga), anasemekana kupendelea kikosi chenye mseto wa chipukizi na wazoefu. Sajili hizi kongwe zikifua dafu mashabiki wa Blues watasubiriwa kuona iwapo watawapaisha kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu (EPL).

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo 17 hours ago

Ndovu 14 wafa kwa njia ya kutatanisha mbugani Amboseli

SHIRIKA la Huduma kwa Wanyamapori Kenya (KWS) limeanzisha uchunguzi kuhusu vifo vya kutatanisha vya ndovu 14 katika Mbuga ya Wanyama ya Amboseli mwezi uliopita. Viongozi wa Kaunti ya Kajiado nao wanataka ripoti ya haraka kubaini kilichosababisha vifo vya ndovu hao. Mizoga ya wanyama hao, waliokuwa wa umri na jinsia tofauti, ilipatikana katika maeneo mbalimbali ya hifadhi hiyo ndani ya kipindi cha wiki mbili. Madaktari wa mifugo wa KWS walichukua sampuli kwa uchunguzi wa maabara ili kubaini chanzo cha vifo hivyo. Afisa mmoja wa KWS, aliyezungumza kwa masharti ya kutotajwa jina, alisema ndovu hao walikuwa wakifuatiliwa na madaktari baada ya kuonyesha dalili za ugonjwa kabla ya kufariki. "Madaktari walijaribu kuwapa matibabu lakini hawakupata nafuu. Mwanzoni ilidhaniwa walikuwa na uchovu wa misuli, lakini matibabu hayakufaulu. Baada ya uchunguzi wa mizoga na ukusanyaji wa sampuli, ilizikwa ndani ya hifadhi," akasema. "Hii ndiyo idadi kubwa zaidi ya tembo kufa kwa muda mfupi katika mfumo wa ikolojia wa Amboseli," akaongeza. Mkuu wa Mawasiliano wa KWS, Duncan Juma, alisema sampuli zilifikishwa kwa maabara ya Serikali na uchunguzi unaendelea. Vifo hivyo vimewatia wasiwasi viongozi wa eneo hilo wakiongozwa na Gavana wa Kajiado Joseph Ole Lenku, ambao wametaka KWS ichapishe mara moja ripoti ya uchunguzi. "Jamii zimeishi na ndovu hao kwa miaka kadhaa. Hatujawahi kushuhudia idadi kubwa namna hii ikifa kwa muda mfupi," akasema Bw Lenku. Seneta wa Kajiado Samuel Seki pia aliikosoa KWS, akiishutumu kwa kutumia kesi mahakamani kuchelewesha uhamishaji wa usimamizi wa mbuga ya Amboseli kwa Serikali ya Kaunti ya Kajiado pamoja na mapato yake.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo 19 hours ago

Iran yasema ingali inadhibiti Hormuz licha ya kunyeshewa mabomu na Amerika wiki 2 mfululizo

DUBAI, UAE: IRAN imesema ingali inadhibiti Mkondo-Bahari wa Hormuz wala haikusudiii kurejelea mazungumzo ya amani na Amerika baada ya Rais Donald Trump kusitisha kampeni ya mabomu ya wiki mbili ambayo wandani wake walimweleza imetimiza azma yake. Kufuatia mashambulizi makali ya mabomu siku 13 mfululizo yaliyosababisha Tehran kulenga ngome za Amerika kulipiza kisasa, Trump alisimamisha kampeni hiyo wikendi. Iran ilisema itasitisha mashambulizi yake binafsi kwa kipindi ambacho Amerika itasimamisha. Mwisho wa kampeni ya mabomu ya Amerika ulisababisha bei za mafuta kuporomoka kwa matumaini kuwa michakato ya usambazaji bidhaa iliyotatizwa duniani itarejelea shughuli zake. Lakini kwa ishara kuwa Tehran huenda tayari inafanyia majaribio mkataba mpya wa kusitisha vita, Jordan iliripoti kuangusha droni mbili na duru za usalama za Iraqi zikasema droni hizo zililenga wapiganaji wa Wakurdi wa Iran eneo la Iraq Kaskazini. Majeruhi hawakuripotiwa katika visa hivyo. Uamuzi wa Trump kusitisha kampeni unaashiria ushauri kutoka kwa jeshi lake kwamba mabomu, yaliyonuiwa kuvunja udhibiti wa Irani kwenye mkondo, yamefikia upeo ambao yangeweza kufanikisha, kulingana na afisa wa Amerika na ripoti kadhaa za vyomvo vya habari. Afisa wa Amerika alisema kwamba makamanda wa jeshi walimshauri rais kwamba wameishiwa na vituo vya kushambulia. Mwenyekiti wa Wakuu wa Wahudumu, Jenerali Dan Caine, alielezea wasiwasi kuhusu kumalizika kwa silaha za kujikinga angani, alisema afisa. Balozi wa Amerika kwa Umoja wa Mataifa, Mike Waltz, alisema Jumapili kuwa Trump alisitisha kampeni kuruhusu majadiliano. Trump, Waziri wa Masuala ya Kigeni Marco Rubiona maafisa wengine wa Amerika wameelezea Iran kama "inayosihgi kuwepo mkataba." Lakini msemaji wa Wizara ya Masuala ya Kigeni Iran, Esmail Baghaei, alisema katika kikao cha vyombo vya habari jana kwamba Iran haijaomba kurejelea mazungumzo ya amani na Amerika. Jumbe bado zilitumwa kati ya pande husika kupitia wapatanishi na Iran haikutelekeza diplomasia, lakini "ripoti kuhusu Iran kuomba majadiliano na Amerika ni za uongo," alisema Baghaei. "Hii haimo katika DNA yetu." Tehran vilevile iliashiria ingali inadhibiti mkondo muhimu zaidi wa maji na masoko ya nishati duniani.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo 21 hours ago

Walimu wapata matumaini baada ya TSC kutangaza nafasi 34,000 za kuwapandisha vyeo

TUME ya Huduma kwa Walimu (TSC) imetangaza nafasi 34,016 za kupandisha walimu vyeo katika shule za msingi, sekondari na vyuo vya mafunzo ya walimu. Waliopandishwa wapo katika madaraja 30, kuanzia Mwalimu Mkuu Mwandamizi II (Senior Teacher II) hadi Mkuu wa Shule (Chief Principal). Walimu wametakiwa watume maombi ya kazi hizo kupitia mtandao wa TSC kabla ya Agosti 10, 2026, huku TSC ikisisitiza kuwa maombi yanayowasilishwa moja kwa moja kupitia kwa mwalimu kufika na stakabadhi katika afisi za tume hayatakubaliwa. "Walimu wenye sifa zinazohitajika wanapaswa kutuma maombi yao kupitia tovuti ya TSC www.teachersonline.go.ke kabla ya Jumatatu, Agosti 10, 2026. Hakuna kuwasilisha stakabadhi katika afisi za TSC," ilisema TSC katika tangazo lake. Hatua hiyo inawapa matumaini walimu wengi ambao wamekwama katika madaraja yale yale kwa miaka mingi licha ya kutimiza masharti ya kupandishwa vyeo. Serikali imetenga Sh2 bilioni katika bajeti ya sasa kufanikisha shughuli hiyo. Hivi majuzi, TSC iliambia Bunge kuwa walimu 178,871 wa shule za msingi na upili wameendelea kubaki katika madaraja yao kutokana na uhaba wa fedha kwa muda mrefu. Walimu wengi waliokwama wako katika daraja la C3 kwa sekondari na C1 kwa shule za msingi. Kati ya nafasi zilizotangazwa, nyingi zinalenga madaraja ya kati ya taaluma. Kuna nafasi 13,490 za Senior Teacher II, nafasi 5,956 za Senior Master IV, na nafasi 4,210 za Senior Teacher I, ambazo zinatarajiwa kuwapa maelfu ya walimu nafasi ya kupanda vyeo. Tangazo hilo limekuja wakati Muungano wa Walimu wa Shule za Upili na Vyuo Anuwai (KUPPET) ukiendelea kushinikiza TSC kutangaza nafasi za kupandisha walimu 135,000 ambao wamekwama kwa muda mrefu katika madaraja yao ya kazi. Katibu Mkuu wa Kuppet, Akello Misori, alisema walimu wengi wamekuwa wakisubiri kupandishwa vyeo kwa miaka mingi licha ya kustahili. Kwa upande mwingine, wakuu wa shule kupitia chama cha KESSHA pia wameitaka TSC kuharakisha mchakato huo, wakisema walimu wakuu wengi hasa walio katika daraja la D3 wamevunjika moyo kwa kukosa nafasi za maendeleo ya kazi. Mwenyekiti wa TSC, Dkt Jamleck Muturi, alisema serikali imewapandisha vyeo walimu 274,285 katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita, lakini akakiri kuwa wengi bado wamekwama katika madaraja yao. TSC pia ilisema waliofaulu katika mahojiano watatakiwa kuwasilisha hati halali za zinazozingatia masharti ya Sura ya Sita ya Katiba kabla ya kuteuliwa rasmi, na watapangiwa shule ambako nafasi hizo zinapatikana.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo 22 hours ago

Raia wa kigeni apigania mali baada ya ndoa yake na mkewe Mkenya kuvunjika

RAIA wa Ireland aliyekuwa amehamia Kenya kwa matumaini ya kuanza maisha mapya na mwanamke aliyefahamiana naye kupitia mtandao sasa amejikuta akihusika katika kesi tatu mahakamani zinazohusu mamilioni ya pesa, mali na kuvunjika kwa ndoa yao. Bw Joel Patrick Fitzpatrick anasema aliuza mali aliyorithi kutoka kwa marehemu mama yake nchini Ireland na kuhamia Watamu, Kaunti ya Kilifi, akiwa na hamu ya kuanzisha biashara na kujenga makazi pamoja na Bi Martha Wanjiru Muhoro, ambaye baadaye alifunga naye ndoa ya serikali mnamo Julai 23, 2025. Hata hivyo, chini ya mwaka mmoja tangu ahamie Kenya, mwanajeshi huyo mstaafu wa Jeshi la Wanamaji la Marekani sasa anakabiliwa na kesi kadhaa, zikiwemo za madai kuhusu matumizi yasiyo halali ya urithi wake. Katika kesi ya hivi punde iliyo mbele ya Mahakama ya Mazingira na Ardhi mjini Malindi, Bw Fitzpatrick anataka Mahakama imzuie Bi Muhoro kuuza, kuhamisha umiliki, kukodisha au kufanya shughuli yoyote kwa ardhi ya Gede/Dabaso, akidai ilinunuliwa kwa Sh25 milioni alizomtumia ili anunue kwa niaba yake. Jumanne iliyopita, Mahakama ilimpa Bi Muhoro wiki mbili kuwasilisha majibu yake baada ya wakili wake kuomba muda zaidi. Mahakama pia iliongeza amri ya kudumisha hali ilivyo na kuagiza pande zote mbili kubadilishana stakabadhi za kesi kabla ya kesi hiyo kutajwa Oktoba 12 kwa maelekezo zaidi. Kulingana na stakabadhi za Mahakama, Fitzpatrick ni mshauri wa masuala ya biashara, siasa na mazingira. Katika kesi nyingine ya madai, anaitaka Mahakama iamuru arejeshewe zaidi ya Sh35.8 milioni ambazo anadai alituma kwenye akaunti ya Benki ya Family inayomilikiwa na Bi Muhoro, huku akiomba akaunti hiyo izuiwe ili fedha zilizomo zisitolewe hadi kesi itakapoamuliwa. Stakabadhi za Mahakama zinaonyesha kuwa wawili hao walifahamiana kupitia tovuti ya kutafuta wapenzi mwaka 2023. Bw Fitzpatrick anasema alirithi asilimia 75 ya mali za marehemu mama yake, ikiwemo nyumba katika Kaunti ya Dublin nchini Ireland, na akamkabidhi Bi Muhoro jukumu la kuandaa uhamisho wake kwenda Kenya kwa kutafuta ardhi, kufuatilia taratibu za uhamiaji na kusimamia mipango ya kifedha. Anadai alimtumia fedha nyingi, zikiwemo euro 250,000 (takriban Sh36.9 milioni) mwezi Aprili 2025 kwa ajili ya kununua ardhi na gari, pamoja na uhamisho mwingine wa euro 10,000 (takriban Sh1.5 milioni) mara nne, euro 15,000 (takriban Sh2.2 milioni) mwezi Septemba na euro 226,860 (takriban Sh33.4 milioni) mwezi Oktoba, ambazo anasema zilikuwa sehemu ya mwisho ya urithi wake. Anadai Bi Muhoro alimshawishi fedha zote zipitie kwenye akaunti yake hadi atakapohamia Kenya, lakini baadaye hakumjumuisha katika umiliki wa ardhi na gari licha ya kuwa ndiye aliyefadhili ununuzi wake. Bw Fitzpatrick anasema amebaki hana mali na ana hofu kuwa fedha zilizobaki zinaweza kutolewa kwenye akaunti hiyo kabla ya kesi kusikilizwa. Kwa upande wake, Bi Muhoro anakiri kupokea fedha hizo lakini anakanusha kuzitumia vibaya. Anasema matumizi yote yalifanywa kwa uwazi na kwa makubaliano ya pamoja walipokuwa wakijiandaa kuanza maisha yao ya ndoa. Pia anasema aliacha kazi yake ya ualimu nchini Qatar kwa ombi la Fitzpatrick na kurejea Kenya kujiandaa kwa harusi yao. Anaeleza kuwa mali hizo zilisajiliwa kwa jina lake kwa sababu wakati huo Fitzpatrick, akiwa raia wa kigeni, hakuwa na stakabadhi zilizohitajika kusajili mali hizo kwa jina lake. Bi Muhoro anasema baadaye uhusiano wao ulivurugika na kumshutumu Bw Fitzpatrick kwa ukatili na unyanyasaji, akiiomba Mahakama itupilie mbali kesi hiyo.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo 23 hours ago

Omtatah apinga kinga ya IMF na Benki ya Dunia inayowazuia kushtakiwa nchini

SENETA wa Busia Okiya Omtatah akishirikiana na wanaharakati Bernard Muchiri na Naomi Misati, wamewasilisha kesi katika Mahakama Kuu wakitaka sheria inayoyapa mashirika ya kifedha ya IMF na Benki ya Dunia, kinga dhidi ya mashtaka, ushuru na kufichua taarifa kuwa kinyume cha Katiba. Walalamishi wanapinga Kifungu cha Sheria ya Bretton Woods ya 1963, wakisema kimepitwa na wakati wala hakiendani na Katiba ya 2010. Kwa mujibu wa kesi hiyo, sheria hiyo inaipa serikali mamlaka makubwa ya kuingia mikataba ya kimataifa ya kifedha, kukopa fedha na kutumia hazina ya umma bila usimamizi wa kutosha wa Bunge. Aidha, sheria hiyo inalinda IMF na Benki ya Dunia dhidi ya kuwajibishwa katika mahakama za Kenya. Wanadai kuwa Kifungu cha tano cha sheria hiyo kinazipa taasisi hizo kinga dhidi ya kushauri mahakama, ushuru, ukaguzi, kutwaliwa kwa mali, jambo ambalo linawanyima Wakenya haki ya kupata haki, kusikilizwa kwa usawa na kupata taarifa. Aidha, wanasema sheria hiyo inaruhusu serikali kutekeleza mikataba ya kimataifa bila idhini ya Bunge na kutoa fedha kutoka Hazina Kuu ya Fedha moja kwa moja kwa IMF na Benki ya Dunia bila kuidhinishwa kila mwaka na wabunge. Bw Omtatah na wenzake wanaeleza kuwa hali hiyo inadhoofisha mamlaka ya Bunge na Mahakama katika kusimamia matumizi ya fedha za umma. Pia inakiuka masharti mbalimbali ya Katiba, pamoja na sura inayohusu usimamizi wa fedha za umma. Mahakama Kuu imewaagiza washtakiwa na wahusika wengine kuwasilisha majibu yao ndani ya siku 14. Kesi hiyo itatajwa tena Septemba 29, 2026, kwa mwelekeo zaidi.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Mon, 27 Jul 2026 22:55:30

Serikali yasema imepata shamba la kuzipa makao familia 21,000 zilizofurushwa Mau

SERIKALI inakaribia kutatua moja ya migogoro ya muda mrefu katika Bonde la Ufa baada ya kuthibitisha kuwa imepata mashamba makubwa katika Kaunti ya Narok ili kuzipa makazi mapya familia zilizofurushwa kutoka Msitu wa Mau pamoja na watu wengine wasio na ardhi. Hatua hiyo inalenga kumaliza mateso ya zaidi ya familia 21,000 zilizofurushwa katika oparesheni mbalimbali za serikali ndani ya kipindi cha miaka 21 iliyopita. Tangazo hilo linajiri huku Rais William Ruto akitarajiwa kuzuru Kusini mwa Bonde la Ufa mwezi ujao. Waziri wa Usalama wa Ndani, Kipchumba Murkomen, alisema serikali iko katika hatua za mwisho za kuwafidia waathiriwa wa Mau na kuwapa makazi mapya waliokosa ardhi katika Kaunti ya Narok. Akizungumza Kapkwen, Kaunti ya Bomet, alisema Wizara ya Ardhi inakamilisha taratibu za mwisho na kwamba orodha ya walionufaika itatangazwa hivi karibuni. Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo na Maendeleo ya Mifugo, Dkt Paul Kipronoh Ronoh, pia alisema maagizo ya Rais Ruto ya kuwahamisha waathiriwa hao tayari yanatekelezwa. "Serikali imefanikiwa kupata ardhi ya kuhamishia familia zilizofurushwa kutoka Msitu wa Mau katika maeneo ya Narok Kusini na Narok Magharibi pamoja na watu wasio na ardhi Angata Barikoi, eneobunge la Kilgoris," akasema. Kiongozi wa Wengi katika Seneti, Aaron Cheruiyot, alisema serikali tayari imelipia baadhi ya mashamba hayo na hatimiliki zimekabidhiwa Wizara ya Ardhi. Pia alisema serikali iko katika hatua za mwisho za kununua zaidi ya ekari 5,000 zinazomilikiwa na familia ya aliyekuwa Mkuu wa Mkoa, marehemu Isaiah Cheluget, katika eneo la Tendwet, Narok Magharibi. Kwa mujibu wa Seneta huyo, uhakiki wa majina ya waathiriwa umekamilika na serikali sasa inakamilisha utaratibu wa kugawa fidia na ardhi. Suala la kufurushwa kwa wakazi wa Mau limekuwa ajenda ya kisiasa kwa zaidi ya miongo miwili. Tangu 2005, marais na wagombea mbalimbali wameahidi kuwafidia na kuwapa makazi mapya walioathiriwa, lakini ahadi hizo zimekuwa zikicheleweshwa. Katika muhula wa pili wa Rais Uhuru Kenyatta, maelfu ya familia zilifurushwa tena kutoka maeneo yanayopakana na msitu, huku nyumba, mashamba na mali nyingine zikiharibiwa katika operesheni iliyoongozwa na aliyekuwa Kamishina Ukanda wa Bonde la Ufa George Natembeya. Rais Ruto amesema serikali yake tayari imelipa familia 2,000 fidia ya Sh300,000 kila moja na imeahidi kuwahamisha jumla ya familia 12,000 ili ziishi maisha ya kibinadamu. Hata hivyo, baadhi ya viongozi na wakazi wanasema kiwango hicho cha fedha hakitoshi kununua ardhi wala kujenga nyumba. "Kiasi cha Sh300,000 hakitoshi hata kununua kiwanja, sembuse kujenga nyumba. Watu walipoteza mashamba, mifugo, mazao na mali nyingine. Wanastahili fidia ya haki," alisema kiongozi wa eneo hilo Johnstone Kiptanui. Seneta wa Narok Ledama Ole Kina, ambaye hapo awali aliunga mkono kufurushwa kwa wakazi hao ili kulinda msitu, sasa anasema wakati umefika serikali iwape makazi mapya na fidia kwa kuwa lengo la kuhifadhi Msitu wa Mau. Hatua ya serikali ya kuharakisha mpango huo inachukuliwa kuwa jaribio la kumaliza mgogoro ambao umeathiri maelfu ya familia na umekuwa ukitumiwa kama ajenda ya kisiasa katika kila uchaguzi mkuu tangu 2007.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Mon, 27 Jul 2026 21:55:28

Mawaziri wa Ruto wazozana Wahome akimponda Duale, Kindiki naye akimkemea Ruku

UHASAMA mkali unaendelea kulikumba Baraza la Mawaziri la Rais William Ruto huku mawaziri wake wakijibizana hadharani na kuibua maswali kuhusu uwezekano wa kutekeleza mabadiliko kuelekea kura ya 2027. Licha ya Rais Ruto kusema akiwa kituo cha kibiashara cha Amagoro, Teso, Busia kuwa hajaanza siasa, mawaziri wake wanaendelea kuzozana huku malumbano yao yakichukua mkondo wa siasa za kikabila. Uhasama wa ndani kwa ndani umeibua maswali kuhusu uwezo wa baraza hilo la mawaziri kuwajibikia Wakenya ipasavyo, miezi 12 kabla ya kura kuwadia. Tukio la hivi punde ni majibizano makali kati ya Waziri wa Afya Aden Duale na Waziri wa Ardhi Alice Wahome kuhusu matamshi ambayo Bw Duale anadaiwa kutoa dhidi ya jamii ya Mlima Kenya. Aidha, Naibu wa Rais Prof Kithure Kindiki ametofautiana vikali na Waziri wa Utumishi wa Umma Geoffrey Ruku kuhusu Mlima Kenya Mashariki kutengana na Magharibi na kujiamulia kivyake mustakabali wake wa kisiasa. Kwenye video ambayo ilisambaa katika mitandao ya kijamii, Bw Duale akiongea kwa lugha ya mama, anadaiwa kulinganisha jamii ya Agikuyu na ya Wasomali kwa kutumia idadi yao nchini huku akidai jamii yake ya Wasomali imekuwa ikibaguliwa na tawala zilizopita za marais Jomo Kenyatta, Mwai Kibaki na Uhuru Kenyatta wote huku nyingine zikinufaika. Akiongea katika Kaunti ya Mandera, Bw Duale alilinganisha jamii ya Agikuyu na fisi ambaye hutaka kula kila kitu isitake jamii nyingine zinufaike kwa miradi ya serikali. Katika video hiyo, Bw Duale alimshukuru Rais Ruto kwa kumaliza kile alichosema ni uongozi ambao umekuwa ukipendelea jamii moja na kubagua jamii nyingine. Waziri wa Ardhi, Alice Wahome ni kati ya viongozi kutoka Ukanda wa Mlima Kenya ambao sasa wanataka Bw Duale aombe msamaha kwa kauli yake. Waziri huyo tayari amesema hawezi kuomba msamaha kwa sababu aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua amewahi kuyatoa matamshi yanayoweza kufasiriwa kama ya kikabila lakini hajawahi kuchukuliwa hatua zozote. Vilevile Bw Duale amesema kuwa hatafika mbele ya Tume ya Kitaifa ya Uwiano na Utangamano (NCIC) iwapo Bw Gachagua hatafanya hivyo kwanza. "Makosa mawili hayafanyi jambo liwe sawa na ni mpumbavu tu ndiye asiyebadilisha fikra zake," akaandika Bi Wahome kwenye mtandao wa X. Bi Wahome ambaye alihudumu kama mbunge wa Kandara kabla ya kuteuliwa waziri, ni wa kwanza kwenye baraza la mawaziri kumshambulia Bw Duale na kumtaka aombe msamaha. Mbali na waziri huyo baadhi ya viongozi kutoka Mlima Kenya akiwemo Gavana wa Kirinyaga Anne Waiguru na Mbunge wa Githunguri Gathoni Wamuchomba wamemshambulia Bw Duale kutokana na matamshi yake hayo. Waziri huyo naye amejitetea kuwa matamshi yake, 'Waraabe la-tagis bartay, ka-ridis waa ku dhib', ni methali ya Kisomali wala haikulenga jamii fulani. "Ujumbe wangu ulilenga kuhakikisha kuna umoja jinsi ambavyo serikali imekuwa ikifanya bila kujali dini au kabila," akasema Bw Duale. "Nilenga kuonyesha ugumu wa kumalizwa kwa mtindo ambao upande mmoja umekuwa ukinufaika kwa kipindi kirefu. Sikulenga jamii yoyote au kumdunisha yeyote. Kuna jaribio la kufasiri matamshi yangu visivyo," akasema. Uhasama mwingine ulioonekana wazi katika baraza la mawaziri ni ule kati ya Prof Kindiki na Bw Ruku kuhusu Mlima Kenya Mashariki kuwa na mwelekeo wa kisiasa 2027. Mlima Kenya Mashariki una kaunti za Embu, Tharaka-Nithi, Meru na sehemu ya kaunti za Kirinyaga na inakadiriwa itakuwa na karibu kura milioni mbili mnamo 2027. Eneo hili limekuwa likipiga kura kwenye kapu moja na wenzao wa Nyandarua, Murangá, Nyeri, Kiambu, Laikipia na Nakuru. Bw Ruku anasema mtindo huu umefanya wabaguliwe na hata sasa wanaonewa gere kwa kushikilia wadhifa wa Naibu Rais. "Mimi siwachukii Wakikuyu lakini lazima tufurahie utambulisho wetu. Tulikuwa na majenerali waliopigania uhuru wa nchi kutoka Mlima Kenya Mashariki ndiyo maana tuliwaunga Jomo Kenyatta, Kibaki na Uhuru," akasema mnamo Juni 30 katika ibada ya Kanisa Kaunti ya Kiambu. "Haiwezekani kuwa mwana wa kiume kutoka Mlima Kenya Mashariki akifanya kazi na Rais Ruto basi viongozi wa Mlima Kenya Magharibi wanatuambia serikali ni mbaya na tunafaa kutoka. Hatutatoka," akaongeza Bw Ruku. Hata hivyo, Naibu wa Rais alionekana kumkemea siku chache baadaye akisema eneo hilo limeungana kwa kipindi kirefu na linastahili kuendelea kufanya hivyo. "Sitaki watu wazungumze lugha tofauti kwa sababu tumefanya mambo mengi pamoja, tuna historia pevu na hakuna kitu ambacho kitatutenganisha," akasema Prof Kindiki mnamo Julai 19 wakati wa ibada katika Kaunti ya Embu. Aidha, Prof Kindiki alikiri kuwa anajikuna kichwa kuhusu unaibu rais ambao unamezewa mate na viongozi wengine kama Waziri wa Vyama vya Ushirika Wycliffe Oparanya lakini akasisitiza hawabanduki serikalini. "Najua tumeongezeka akina Oparanya wamekuja lakini hatuondoki, tutang'ang'ana hapa ndani," akasema Kindiki. Wikendi iliyopita, Prof Kindiki aliwachemkia viongozi ambao wanamezea mate wadhifa wake na kumsawiri kama asiyefaa kushikilia wadhifa huo. "Serikali haiwezi kuwa mzuri wakati naibu rais akitoka upande wao na ni mbaya akitoka hapa. Wakati Uhuru alikuwa rais tulimuunga mkono na hatuwezi kubali jamii ya eneo hilo liongee lugha tofauti," akasema Profesa Kindiki. "Ni haki yao kuenda mahali wameenda lakini upande wao wamepangana na namba zote zimeenda na tuko namba 20. Rais Ruto akimaliza muhula wake urais utakuja pande hii," akasema. Wikendi viongozi wa ODM kutoka Nyanza na Magharibi walisisitiza kuwa UDA ikiwahi urais naye mgombeaji mwenza anastahili kutoka chama hicho cha chungwa. "Watu wakuje pole pole na wajue kwamba huwezi kuruka laini. UDA ikipata urais, sisi lazima tupate naibu rais na huyo ni Oparanya," akasema Kiongozi wa Wachache Junet Mohamed wikendi akiwa Kakamega. Kwa mujibu wa Mchanganuzi wa Masuala ya Kisiasa Profesa Lumala Masibo ni wazi kuwa baraza la mawaziri lina vita vya ndani kwa ndani hasa baada ya Profesa Kindiki kuonekana kuanza kuridhiana na Bw Gachagua. "Baadhi sasa wanamwona kama anayejipanga kivyake na hata alivyoongea wikendi, anaonekana kama mtu ambaye si mtiifu sana kwa Rais tena. Anaweza aje kudai unaibu rais utasalia kwake ilhali si anayeteua mshikilizi wa nafasi hiyo," akasema Profesa Masibo. Kauli yake inatokana na hatua ya Bw Gachagua kuwaamrisha viongozi wanaoumuunga mkono wasimshambulie Profesa Kindiki bali wamlenge Rais Ruto moja kwa moja. "Baada ya Ol Kalou ni dhahiri kuwa Rais amepoteza Mlima Kenya na shida sasa ni kupambania nafasi ya mgombeaji mwenza. Pia baadhi ya mawaziri kutoka Mlima Kenya sasa wanajificha nyuma ya kauli ya Bw Duale kumridhisha Gachagua kwa sababu ya umaarufu wake mlimani," akaongeza.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Mon, 27 Jul 2026 10:23:43

Prof Okumu ateuliwa mkuu mpya wa Chuo Kikuu cha Kenyatta

BARAZA la Chuo Kikuu cha Kenyatta jana lilimteua Profesa John Okumu kuwa Naibu Chansela wa chuo hicho baada ya kuibuka mshindi katika mchakato wa kuajiri ulioendeshwa na Tume ya Utumishi kwa Umma (PSC). Uteuzi huo ulitangazwa Jumatatu kupitia taarifa iliyotiwa saini na Mwenyekiti wa Baraza la Chuo Profesa Clara S. Momanyi, ambaye alisema uamuzi huo ulifanywa kwa mujibu wa Sheria ya Vyuo Vikuu na kwa idhini ya Waziri wa Elimu. Profesa Okumu anafahamu vyema Chuo Kikuu cha Kenyatta kutokana na kuhudumu katika nyadhifa mbalimbali za uongozi kwa miaka mingi. Aliwahi kuwa Naibu Chansela anayesimamia Masuala ya Kitaaluma kwa miaka 10, pamoja na kushikilia nyadhifa nyingine za juu za usimamizi. Baraza lilimsifu kama msomi na msimamizi mwenye tajriba kubwa katika uongozi wa elimu ya juu, utafiti na maendeleo ya taasisi. Prof Momanyi alisema ana imani kuwa tajriba na uwezo wa Profesa Okumu katika kupanga mikakati, kusimamia taasisi na kushirikiana na wadau utasaidia kuimarisha maendeleo ya chuo hicho. "Tunamkaribisha Profesa Okumu katika nafasi hii muhimu na tunatoa wito kwa wanajamii wote wa chuo na wadau kumpa ushirikiano anaohitaji ili atekeleze wajibu wake na afanikiwe," akasema. Profesa Okumu alikuwa akishikilia wadhifa huo kwa muda tangu mwishoni mwa Januari 2026 baada ya kumrithi Profesa Paul Wainaina, aliyestaafu baada ya kuhudumu kwa miaka minane. Katika mahojiano yaliyofanywa na PSC, Profesa Okumu alipata alama 84.5, akiwashinda Profesa Stephen Odebero na Profesa Godfrey Mse. Hata hivyo, uteuzi huo ulikumbwa na changamoto za kisheria baada ya Profesa Waceke Wanjohi, Naibu Chansela wa Masuala ya Kitaaluma na mmoja wa waliowania wadhifa huo, kufikisha kesi Mahakama Kuu akidai ndiye aliyepata alama za juu zaidi na kwamba aliondolewa isivyo haki. Mnamo Aprili, Jaji Njoki Mwangi alitoa amri za muda zilizokizuia chuo kujaza nafasi hiyo hadi kesi hiyo isikizwe, huku pia akiamuru mkataba wa Profesa Wanjohi uongezwe. Mvutano huo uliibua sintofahamu kuhusu hatima ya nafasi hiyo kwa miezi kadhaa kabla ya Baraza la Chuo kuthibitisha rasmi uteuzi wa Profesa Okumu. Uteuzi huo unatarajiwa kuleta utulivu katika uongozi wa Chuo Kikuu cha Kenyatta na kuweka msingi wa utekelezaji wa mipango yake ya maendeleo.

read more