T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo 13 hours ago

BATUK: Wabunge wadai Kenya haijaingia katika makubaliano na Uingereza

Wabunge wamesisitiza kuwa hakuna makubaliano mapya yaliyofikiwa kati ya Kenya na Uingereza kuhusu mkataba wa ushirikiano wa kijeshi na Kenya (BATUK). Kauli hiyo inajiri baada ya Uingereza kusema kuwa kumekuwa na maendeleo makubwa katika kutekeleza baadhi ya mapendekezo yaliyotolewa na Kamati ya Bunge kuhusu Ulinzi. Uingereza ilisema maafisa wake wakuu walikutana na maafisa wa serikali ya Kenya, wabunge na wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Masuala ya Kigeni Juni kujadili hatua iliyofikiwa. "Maafisa wakuu wa Uingereza walikutana na maafisa wa Serikali ya Kenya, wabunge na wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Masuala ya Kigeni mwezi Juni kujadili maendeleo yaliyofikiwa hadi sasa," ilisema taarifa hiyo. Uingereza pia ilisema taratibu za pamoja za kushughulikia mabomu na vilipuzi ambavyo havijalipuka zimekamilishwa. Miongoni mwa masuala mengine yaliyoshughulikiwa ni mahitaji ya ulinzi wa mazingira na matumizi ya ardhi, ambayo yamewasilishwa kwa mamlaka husika. Uingereza pia ilisema imeweka hatua mpya za kuzuia unyanyasaji wa kingono. Hata hivyo, Kamati ya Bunge kuhusu Ulinzi iliambia Bunge Jumanne kuwa mkataba huo bado haujaidhinishwa. Mwenyekiti wa kamati hiyo, Nelson Koech, alisema makubaliano hayo hayawezi kuanza kutumika hadi masharti yaliyowekwa na Kenya yatimizwe. Bunge linataka vifungu vya 6(5) na 23 virekebishwe ili mauaji yawe chini ya mamlaka ya mahakama za Kenya. Wabunge pia wanataka BATUK iwe na mpango wa uwajibikaji kwa jamii unaohusisha maeneo inayofanyia shughuli zake. Bw Koech alisema kamati haitakubali mkataba unaokiuka Katiba au kudhalilisha Wakenya. Alisema kujumuishwa kwa mauaji katika vifungu vinavyopendekezwa kutaimarisha uwajibikaji na kuhakikisha wahalifu wa makosa hayo makubwa wanawajibishwa nchini. Mbunge wa Laikipia wa Kike Jane Kagiri aliunga mkono msimamo huo, akisema mtu yeyote anayefanya uhalifu nchini Kenya anapaswa kufikishwa mbele ya mahakama za Kenya. Kwa sasa, mkataba huo unaacha makosa kadhaa makubwa chini ya mamlaka ya Kenya, lakini mauaji hayajajumuishwa katika orodha hiyo. Hali hiyo imeibua wasiwasi kwamba Uingereza inaweza kudai mamlaka ya kushughulikia kesi za mauaji yanayohusisha wanajeshi wake. Bw Koech alisema masharti ya kamati bado hayajatimizwa licha ya serikali kutangaza kuanza tena kwa mafunzo ya pamoja ya kijeshi kati ya Kenya na Uingereza katika kituo cha BATUK, Laikipia. Alisema mazungumzo na kubadilishana mawasiliano kumeendelea, lakini Uingereza bado haijatoa ahadi ya kutosha kuhusu madai ya Kenya. BATUK imekuwa ikifanya shughuli nchini Kenya chini ya Mkataba wa Ushirikiano wa Ulinzi kati ya Kenya na Uingereza uliopitishwa mwaka 2016. Mkataba mpya uliwasilishwa Bungeni mwaka 2021 baada ya muda wa mkataba wa awali wa miaka mitano kuisha. Hata hivyo, Bunge la 12 lilimaliza muda wake kabla ya kuidhinisha mkataba huo. Mkataba huo uliwasilishwa tena kwa Bunge la 13 mwezi Novemba 2022. Baada ya kushirikisha wananchi, kamati ilipendekeza uidhinishwe kwa masharti kwamba vifungu vya 6(5) na 23 virekebishwe kabla ya kuanza kutumika.

read more

Other Headlines


T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo 17 hours ago

Linda Mwananchi ilivyopokonywa jina

VUGUVUGU la Linda Mwananchi limetishia kufanya maandamano ya kila siku nje ya Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Kisiasa (ORPP) iwapo ombi lake la kusajiliwa kama chama cha kisiasa halitashughulikiwa. Hatua hiyo inazidisha mvutano kati ya vuguvugu hilo na ofisi ya Msajili wakati Linda Mwananchi ikijaribu kujibadilisha kuwa chama rasmi cha kisiasa kabla uchaguzi mkuu wa 2027. Akizungumza wakati wa ziara ya Linda Mwananchi ya kukutana na wananchi katika Kaunti ya Busia siku ya Ijumaa, Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi alilaumu watu ambao hakuwataja kwa kujaribu kunyakua jina linalohusishwa na vuguvugu hilo. Osotsi alisema kundi hilo litampa Msajili hadi kesho kutatua suala hilo. Alionya kuwa iwapo suala hilo halitatatuliwa basi wafuasi wa Linda Mwananchi wataanza kufanya mikutano ya kila siku nje ya ofisi za ORPP. "Ruto ametuma wakora kule kwa ofisi ya msajili wa vyama eti wanajaribu kunyakua hii jina yetu. Mimi nataka kuambia William Ruto, Ibara ya 38 inaruhusu Mkenya yeyote kuunda chama," alisema Osotsi. Akaongeza: "Tunaambia huyo msajili kama hutapatiana hiyo jina Jumatatu, tutaandaa mikutano ya kila siku kwa hiyo ofisi." Mzozo huo umejikita katika maombi ya kusajili chama na namna Ofisi ya Msajili inashughulikia jina linalopendekezwa na Linda Mwananchi. Mvutano huo ulipata sura mpya baada ya ORPP kuripotiwa kusajili Liberty National Democratic Alliance, kinachojulikana kama LINDA Party. Hatua hiyo imeibua mvutano mpya na Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna pamoja na washirika wake katika Linda Mwananchi. Usajili wa chama kinachotumia jina LINDA umeleta changamoto mpya kwa juhudi zao. Kwa mujibu wa ripoti, chama hicho kipya kinahusishwa na kundi tofauti ambalo pia lilikuwa limejitahidi kupata utambulisho wa kisiasa kwa kutumia jina "Linda". Kundi hilo pinzani limepinga madai ya Linda Mwananchi kwamba ndilo lenye haki ya kutumia jina hilo. Madai hayo yameibua swali kuhusu kundi lenye haki ya kutumia jina na nembo zinazohusishwa na "Linda". Mzozo huo pia umewekea Ofisi ya Msajili shinikizo kutoka pande zote. Viongozi wa Linda Mwananchi wamekuwa wakisisitiza kuwa tayari wamejenga utambulisho wa kisiasa kupitia jina hilo, hivyo wanafaa kupewa nafasi ya kukitumia chama hicho. Hatua ya hivi majuzi inafuatia mikutano kati ya viongozi wa Linda Mwananchi na Msajili wa Vyama vya Kisiasa John Cox Lorionokou. Ripoti zinasema kuwa Msajili alikubali kupitia upya uamuzi wa awali wa kukataa jina la Linda Mwananchi baada ya mashauriano na wawakilishi wa vuguvugu hilo. Hatua hiyo ilikuwa imeibua matumaini miongoni mwa viongozi na wafuasi wa Linda Mwananchi kwamba mchakato wa usajili ungeendelea. Hata hivyo, usajili ulioripotiwa wa LINDA Party umeleta changamoto mpya na kugubika Linda Mwananchi na mzozo mwingine kuhusu jina inalotaka kutumia. Wadadisi wanasema haki inayotokana na Kifungu 38 cha Katiba - kinachowapa raia haki ya kuunda au kushiriki katika uundaji wa chama cha kisiasa - inaambatana na masharti ya kisheria yanayosimamia usajili wa vyama vya kisiasa nchini. Ofisi ya Msajili ina jukumu la kusajili na kudhibiti vyama pamoja na kusimamia taratibu za kisheria zinazohusu kuanzishwa kwa vyama. Linda Mwananchi sasa inataka ORPP itatue mzozo huo ili iweze kukamilisha miundo yake kabla ya uchaguzi ujao. Usajili wa chama ni hatua muhimu katika kubadilisha vuguvugu hilo kuwa chombo rasmi cha uchaguzi. Kwa sasa, viongozi wake wameweka Jumatatu kuwa siku ya mwisho kwaMsajili wa Vyama kushughulikia suala hilo kabla kuanza kwa mikutano ya kila siku nje ya ofisi hiyo.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo 16 hours ago

Tofauti zaibuka kuhusu tarehe ya kuandaa uchaguzi

INGAWA Katiba ya 2010 iliweka tarehe ya uchaguzi ili iwe wazi na ya kutabirika, suala hilo limefikishwa mahakamani angalau mara tano tangu 2015. Kesi hizo zimehusisha majaji 13 na kuzua tafsiri tofauti kuhusu maana ya kifungu kinachosema uchaguzi ufanyike "Jumanne ya pili ya Agosti katika kila mwaka wa tano". Mzozo huo umeibuka tena baada ya Jaji wa Mahakama Kuu Malindi Mugure Thande kuamua kuwa uchaguzi mkuu ulipaswa kufanyika Agosti 2026 badala ya 2027. Mwanasheria wa masuala ya Katiba Waikwa Wanyoike anasema mkanganyiko huo unatokana na dhana kwamba Katiba inamhakikishia kila kiongozi aliyechaguliwa kipindi cha miaka mitano. Vita vya kwanza vilianza kabla ya uchaguzi wa 2017 baada ya watu watatu kupinga tarehe iliyokuwa imewekwa na Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka nchini (IEBC). Walidai kuwa uchaguzi wa madiwani wa kaunti (MCAs) Agosti 8, 2017 ungekatiza kipindi chao cha miaka mitano kwa karibu miezi minane. Jaji Edward Muriithi aliamua Aprili 2017 kuwa kulikuwa na mkanganyiko kati ya vifungu viwili vya Katiba kuhusu muda wa madiwani na tarehe ya uchaguzi. Hata hivyo, Mahakama ya Rufaa ilibatilisha uamuzi huo Novemba 2017 na kusema tarehe ya uchaguzi iliyowekwa na Katiba haiwezi kubadilishwa. Kesi nyingine iliwasilishwa mwaka 2018 na mwanaharakati Okiya Omtatah na Nyakina Wycliffe Gisebe. Walidai uchaguzi ulipaswa kufanyika Agosti 2021 badala ya 2022. Jaji Weldon Korir alikataa kesi hiyo Novemba 2020, akisema uchaguzi wa viongozi wote unapaswa kufanyika siku moja baada ya kipindi cha miaka mitano. Mwaka 2022, aliyekuwa Seneta mteule Paul Njoroge alipinga tarehe ya uchaguzi wa urais wa Agosti 9. Jaji Anthony Mrima alikataa hoja hiyo. Mzozo huo ulifika Mahakama ya Juu mwaka 2025 baada ya mwanasheria Dkt Owiso Owiso na wanaharakati Khelef Khalifa na Ashioya Biko kutaka mahakama hiyo ieleze kifungu cha 136(2)(a). Mahakama hiyo ya majaji saba haikugusia kiini cha kesi na ikaiondoa Agosti 15, 2025 kwa misingi ya mamlaka yake. Walalamishi hao walienda Mahakama Kuu ya Malindi, ambako Jaji Thande aliamua kuwa uchaguzi mkuu ulipaswa kufanyika Jumanne, Agosti 11, 2026. Bw Wanyoike anaunga mkono tafsiri hiyo akisema Katiba haimhakikishii Rais, wabunge na maseneta kipindi kamili cha miaka mitano. Hata hivyo, mwanasheria Dudley Ochiel anapinga akisema historia ya kutunga Katiba inaonyesha wazi kuwa Kenya ilikusudia kuwa na mzunguko wa uchaguzi wa miaka mitano. "Historia ya Katiba haiungi mkono nia ya kuanzisha vipindi vya miaka minne kwa viongozi waliochaguliwa," alisema. Mwanasheria Ndung'u Wangenye anasema Mahakama ya Juu ndiyo itakayotoa jibu la mwisho kuhusu suala hilo. "Suluhisho la mwisho litakuwa uamuzi wa Mahakama ya Juu," alisema.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo 15 hours ago

Malumbano ya ubabe Mlimani kati ya Gachagua, Munya raha kwa Ruto

MALUMBANO yanayoendelea kati ya aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua na baadhi ya viongozi wa eneo la Mlima Kenya huenda yakawa habari njema kwa Rais William Ruto anapojiandaa kutetea kiti chake katika uchaguzi wa 2027. Kinachoonekana kama mzozo wa kawaida kuhusu vyama kinaweza kuwa na athari kubwa kwa siasa za upinzani, hasa katika eneo hilo lenye idadi kubwa ya wapigakura. Mzozo huo ulizuka baada ya viongozi wa vyama kadhaa kupinga kauli zinazohusishwa na Gachagua, kwamba vyama vidogo vinafaa kuvunjwa ili vijiunge na Democracy for the Citizens Party (DCP). Miongoni mwa waliopinga wazo hilo ni kinara wa Democratic Party (DP) Justin Muturi, kinara wa Party of National Unity (PNU) Peter Munya na kinara wa Devolution Empowerment Party (DEP) Lenny Kivuti. Viongozi hao walisema umoja wa upinzani haupaswi kujengwa kwa masharti au shinikizo, bali kupitia mashauriano, kuheshimiana na ushirikiano wa hiari. Hata hivyo, malumbano hayo yanaibua swali kubwa kuhusu nani atakuwa na ushawishi mkubwa Mlima Kenya kuelekea 2027. Tangu kuondolewa kwake kama Naibu Rais, Gachagua amekuwa akijaribu kujijenga kama kiongozi mkuu wa kisiasa wa eneo hilo. DCP imekuwa chombo muhimu katika mkakati huo, huku washirika wake wakijaribu kuunganisha wanasiasa wa mlimani chini ya chama kimoja kabla ya mazungumzo ya muungano wa kitaifa. Lakini msimamo wa Muturi, Munya na Kivuti unaonyesha kuwa si viongozi wote wanaompinga Ruto wako tayari kufuata mkondo wa Gachagua. Hilo linaweza kuwa pigo kwa mpango wa Mlima Kenya kuzungumza kwa sauti moja kuelekea 2027. Eneo hilo huwa na nguvu kisiasa linapoungana. Katika chaguzi zilizopita, viongozi walioweza kuunganisha kura za eneo hilo walipata usemi mkubwa katika mazungumzo ya kisiasa kitaifa. Lakini sasa kuna dalili za vituo vingi vya nguvu vita vya ndani vikionekana kuchacha. Jambo linalojitokeza kwenye mzozo huo ni kwamba baadhi ya viongozi wanaompinga Ruto sasa wanatumia nguvu nyingi kumjibu Gachagua, kuliko kueleza namna watakavyompinga Rais katika uchaguzi ujao. Badala ya mjadala kuwa Ruto dhidi ya upinzani, unaanza kuwa Gachagua dhidi ya viongozi wengine wa upinzani na wachambuzi wa siasa wanasema hili linaweza kumfaa Ruto. "Kadiri viongozi hao wanavyobishana kuhusu nani anafaa kuongoza Mlima Kenya, ndivyo wanapoteza muda wa kujenga kampeni moja kubwa ya kitaifa dhidi ya serikali.Kila tofauti ya maoni inaongeza uwezekano wa upinzani kuingia 2027 ukiwa umegawanyika," asema mchambuzi wa siasa Dkt Isaac Gichuki. Kiini cha mzozo huo ni: nani ana haki ya kuzungumza kwa niaba ya Mlima Kenya? Washirika wa Gachagua wamemtaja kama kiongozi wa kisiasa wa eneo hilo kufuatia kuondolewa kwake mamlakani. Lakini wapinzani wake wanasema hakuna mtu aliyepewa mamlaka ya kuwa msemaji wa eneo lote. Muturi, Munya na Kivuti wanasisitiza kwamba hakuna mkutano uliowahi kufanyika kumpa Gachagua mamlaka hayo. Pia wanakumbusha kuwa hata marais wa zamani Jomo Kenyatta, Mwai Kibaki na Uhuru Kenyatta hawakuwahi kudai vyama vingine vivunjwe ili kuonyesha uaminifu kwao. Wanasema Gachagua anaweza kuwa na ushawishi mkubwa, lakini sio eti hana mpinzani. Viongozi hao pia wanaonekana kuhofu kwamba DCP inaweza kuwa chama kikubwa kinachotawala vyama vingine vidogo. Kwao, kulazimisha vyama vidogo kuvunjwa hakutaimarisha demokrasia. Kwa Ruto mzozo huo unaweza kuwa faida kubwa. "Viongozi wanaompinga wanapogawanyika nafasi ya kujenga upinzani mmoja wenye nguvu hupungua. Aidha, mivutano ya hadharani inaweza kuwafanya wapigakura wa Mlima Kenya kutokuwa na uhakika kuhusu upande wa kuunga mkono," asema Dkt Lilian Kimani, mchanganuzi wa siasa. Anasema hii inaweza kumpa Ruto nafasi ya kujaribu kurejesha ushawishi wake katika eneo ambalo wapinzani wameanza kujishindia.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo 14 hours ago

Hofu kijijini watoto 10 wakijitia kitanzi

HOFU imetanda katika eneo la Ndabibi Central, Naivasha, baada ya watoto wasiopungua 10 kujitia kitanzi katika kipindi cha mwaka mmoja. Wakazi wanasema visa hivyo vimeacha familia zikijiuliza kinachowasukuma watoto wadogo kujiua. Miongoni mwa waliofariki ni Cynthia Muthoni, mwanafunzi wa Gredi ya Sita. Asubuhi ya Juni 6, alionekana kuwa sawa nyumbani kwao. Rachael Wahu Kariuki na binti yake walikuwa wameenda mtoni kufua nguo kabla ya kurejea nyumbani. Mchana, Wahu alimwacha Muthoni akiosha vyombo na kumuagiza apike chakula kabla ya yeye kurejea kazini. Karibu saa tisa alasiri, mama huyo alirudi nyumbani na kumpata binti yake akiwa katika hali nzuri. Aliondoka tena baada ya kuitwa shuleni. Muda mfupi baadaye, majirani wawili walifika kwa pikipiki na kumuomba awafuate. Walimpeleka kwa jirani, ambapo Wahu aliambiwa binti yake alikuwa amefariki baada ya kujitia kitanzi. Dada yake ndiye aliyegundua na kuwaarifu majirani. "Nilimwacha akiwa na furaha. Hakuwa amefanya kosa lolote na hatukuwa tumegombana. Sijui ni nini kilimfanya ajitie kitanzi," alisema Wahu kwa machozi. Mama huyo alisema Muthoni alikuwa amewahi kuugua ugonjwa wa figo. Dawa alizokuwa akitumia zilifanya mwili wake uvimbe na akaanza kuogopa kuchekwa na wanafunzi wenzake. Alikuwa pia amekataa kurejea shuleni na alitaka kujiunga na mafunzo ya ufundi. Kilomita chache kutoka hapo, familia ya Kiragu Mochogua ilikuwa ikiomboleza kifo cha binti yao wa miaka 16, Jane Wanjiru. Jane alikuwa ameenda kutafuta kuni lakini hakurudi nyumbani.Baba yake alimfuata msituni baada ya kuona nyayo zake.Huko ndiko alipompata binti yake akiwa amefariki. Mama yake, Phyllis Wambui, alisema Jane alikuwa akisumbuliwa na matatizo ya afya na aliacha shule akiwa Darasa la Tano. Dada yake mdogo pia aliacha shule akiwa Darasa la Tatu ili kumhudumia. Familia ilikuwa imeanza kupanga kumrudisha Jane shuleni baada ya afya yake kuimarika. Lakini alifariki kabla ya mpango huo kutimia. Kifo cha Beth Nyaguthie Juma, mwanafunzi wa Gredi ya Sita, pia kimeongeza majonzi katika eneo hilo. Kaka yake, Peter Chege Juma, alisema alipokea simu ya dharura kutoka kwa majirani na kukimbia nyumbani. Alisema kifo cha dada yake kilimvunja moyo kiasi kwamba aliondoka nyumbani kwao na kukodisha nyumba. "Mama yetu alifariki 2024. Dada yangu alikuwa kitindamimba. Kifo chake kilituacha na maumivu makubwa," alisema. Chifu msaidizi wa Ndabibi Central, Aseth Kariuki, alisema visa hivyo vinazidi kuwa vya kutisha. Alisema watoto wenye umri wa kati ya miaka 12 na 15 ndio walioathirika zaidi. "Mwaka huu pekee, tumewazika watoto watano waliofariki baada ya kujitia kitanzi Ndabibi. Tulipofuatilia visa hivyo, wazazi na walimu walisema hawakuona ishara zozote za hatari," alisema. Mercy Wangui Mburu, mwalimu na mhudumu wa kulinda watoto, alisema angalau watoto 10 wamefariki kwa kujitia kitanzi katika eneo hilo tangu Juni mwaka uliopita. Watoto wengine saba wamejaribu kujiua.Wengi wa walioathirika wana umri wa miaka 12 hadi 17. Wangui alisema wahudumu wa jamii wamelemewa na visa hivyo. "Tunahitaji washauri wa kitaalamu. Hata kama watakaa hapa kwa miezi miwili. Tunataka kuelewa watoto hawa wanapitia nini kwa sababu wanateseka kimya kimya," alisema. Alitaka serikali za kitaifa na kaunti kuingilia kati na kuimarisha huduma za afya ya akili katika shule, makanisa na familia. Mtaalamu wa ushauri nasaha Meshack Ondieki alisema wazazi wanapaswa kuwasikiliza watoto wao na kuzingatia mabadiliko katika tabia zao. Alisema ishara za kuangaliwa ni pamoja na kujitenga na familia, kushuka kwa matokeo shuleni, kupoteza hamu ya shughuli walizopenda na kubadilika kwa uhusiano wao na wenzao. Pia alisema kukosa hamu ya kula, uchovu wa mara kwa mara, kupuuza usafi wa kibinafsi na kukataa kushiriki shughuli za kawaida vinaweza kuwa ishara kwamba mtoto anapitia matatizo ya kihisia. Alisema mabadiliko hayo hayafai kupuuzwa kama tabia za kawaida za ujana, hasa yanapotokea kwa pamoja. Kulingana na takwimu za Kaunti ya Nakuru zilizotajwa na wataalamu wa afya ya akili, zaidi ya visa 400 vinavyohusiana na kujiua viliripotiwa kati ya Januari 2020 na Aprili 2025. Takwimu hizo zinaonyesha ukubwa wa changamoto inayokabili watoto na vijana katika eneo hilo.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo 18 hours ago

ODM sasa yamkalia Ruto ngumu kuhusu 2027, yataja matakwa 8

CHAMA cha ODM kimeweka matakwa manane mbele ya Rais William Ruto kabla ya uchaguzi wa 2027, huku viongozi wa chama hicho wakitarajiwa kuyajadili katika mkutano wa siku tatu wa serikali jumuishi unaoanza Naivasha leo Jumapili. Mkutano huo unawakutanisha magavana, manaibu wao na wabunge wa ODM, UDA na vyama vingine vinavyounga mkono serikali jumuishi. Ingawa mkutano huo umeelezwa kuwa wa kuimarisha uhusiano na kujenga mwafaka, ODM inataka serikali itekeleze makubaliano yaliyofikiwa kabla ya chama hicho kuendelea kushirikiana na UDA kuelekea uchaguzi wa 2027. ODM inataka utekelezaji wa ajenda ya vipengele 10 iliyokuwa msingi wa makubaliano ya kisiasa kati ya Rais Ruto na marehemu aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga. Mwenyekiti wa ODM Gladys Wanga alisema viongozi watapitia hatua zlizopigwa katika kutekeleza makubaliano hayo. Ajenda hiyo inahusisha masuala yaliyokubaliwa na pande hizo mbili wakati wa mazungumzo yaliyolenga kupunguza mvutano wa kisiasa nchini. ODM pia inataka serikali kutoa mwelekeo kuhusu miswada iliyotokana na Kamati ya Mdahalo wa Kitaifa (Nadco). Baadhi ya mapendekezo ya Nadco yalihusu kuanzishwa kwa afisi ya Kiongozi Rasmi wa Upinzani na Waziri Mkuu. Chama hicho kinataka kujua hatua ambayo serikali imechukua kutekeleza mapendekezo hayo. ODM inataka hatua zaidi kuchukuliwa kuhusu fidia kwa waathiriwa wa ukatili wa polisi. Bi Wanga alisema suala hilo litakuwa miongoni mwa mambo yatakayojadiliwa katika mkutano huo. Hii ni mojawapo ya masuala ambayo chama hicho kinataka serikali ishughulikie kama sehemu ya makubaliano yaliyofikiwa. ODM pia inataka kuwe na uwazi kuhusu mustakabali wa ushirikiano wake na UDA kuelekea uchaguzi wa 2027. Chama hicho kinataka kujua jinsi ushirikiano huo utakavyofanya kazi na nafasi ya kila chama katika maandalizi ya uchaguzi. Huku uchaguzi ukikaribia, viongozi wa vyama hivyo wameanza kushindana kuhusu maeneo ya kisiasa na nafasi mbalimbali. ODM inataka ngome zake za jadi za kisiasa zilindwe katika mpango wa ushirikiano wa uchaguzi. Suala la kutengewa maeneo limekuwa chanzo cha mvutano kati ya ODM na UDA. ODM imekuwa ikitaka ngome zake ziheshimiwe, huku UDA ikitaka kila chama kiruhusiwe kuwasilisha wagombea katika maeneo yote isipokuwa kiti cha urais. Gavana wa Mombasa na naibu kiongozi wa ODM Abdullswamad Nassir alisema suala hilo litashughulikiwa na kamati maalum ya vyama hivyo. Suala la nani atakuwa mgombea mwenza wa Rais Ruto 2027 pia limekuwa nyeti. Baadhi ya viongozi wa ODM tayari wamemuunga mkono Waziri wa Ushirika Wycliffe Oparanya kwa wadhifa huo. Hilo limezua ushindani na washirika wa Naibu Rais Kithure Kindiki. ODM inataka ushirikiano huo utoe nafasi ya chama kushiriki katika maamuzi muhimu kuhusu uchaguzi wa 2027. Chama hicho pia kinataka kuwe na mpango wa pamoja wa kuelekea uchaguzi wa 2027. Kiongozi wa wachache katika Bunge la Kitaifa Junet Mohammed alisema mkutano huo utatoa mwelekeo kuhusu uchaguzi ujao. "Kutakuwa na maamuzi mazito yatakayotoa mwelekeo wa kisiasa. Viongozi watatoa mwongozo wa kuelekea 2027," alisema. Mpango huo unatarajiwa kuangazia mikakati ya kampeni, ushirikiano wa vyama na ujumbe wa serikali kwa wapigakura. ODM pia inataka kushiriki katika mjadala kuhusu Ruwaza mpya ya Rais Ruto ya 2060. Rais anatarajiwa kuzindua mpango huo Agosti 12, siku moja baada ya kumalizika kwa mkutano wa Naivasha. Mkutano huo pia unafanyika wakati ODM na UDA zinakabiliwa na ushindani wa kisiasa katika maeneo mbalimbali. Mabadiliko ya uaminifu wa kisiasa, hasa Mlima Kenya, yameongeza presha kwa Rais Ruto. UDA imepoteza baadhi ya washirika wake wakuu, wakiwemo magavana Irungu Kang'ata wa Murang'a na Kiarie Badilisha wa Nyandarua pamoja na Mbunge wa Kiharu Ndindi Nyoro.  Wakati huo huo, vuguvugu la Linda Mwananchi linalohusishwa na Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna linaendelea kupanua mbawa zake.  ODM ina wasiwasi kuwa vuguvugu hilo linaweza kupunguza nguvu zake katika baadhi ya ngome zake za jadi kuelekea uchaguzi wa 2027.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Sat, 08 Aug 2026 02:55:59

Wimbi jipya la mashambulizi ya Al-Shabaab lafanya wakuu wa usalama kujikuna vichwa

KAUNTI za Mandera, Wajir na Garissa zilishuhudia ongezeko la mashambulizi ya kigaidi mwezi Julai, hali ambayo imewalazimu maafisa wa usalama kutafuta mikakati mipya ya kukabiliana na tishio hilo. Mandera iliongoza kwa kuripoti visa tisa, ikifuatiwa na Garissa ikiwa na visa vinne na Wajir viwili, kwa mujibu wa ripoti ya kijasusi iliyosambazwa kwa maafisa wa usalama katika eneo hilo. Shambulio la hivi majuzi lilitokea Alhamisi usiku ambapo watu 10 walinusurika kifo baada ya gari walilokuwa wakisafiria kukanyaga kilipuzi katika barabara ya Takaba-Wargadud-Elwak, Mandera. Tukio hilo lilitokea karibu na kijiji cha Odole saa 12 jioni. Walionusurika walikimbizwa katika Hospitali Ndogo ya Elwak baada ya kujeruhiwa. Mmoja wa manusura alisema walikuwa wakijadili masuala ya siasa za Mandera wakati mlipuko ulipotokea. "Ndani ya sekunde chache kulikuwa kimya. Niligundua damu ikitiririka usoni. Nilikuwa nimekatwa vibaya usoni," alisema. Naibu Kamishna wa Kaunti ya Mandera Kusini, Tobias Otunga alithibitisha tukio hilo na kusema uchunguzi umeanzishwa. Afisa mmoja mkuu wa usalama alisema kumekuwa na ongezeko la watu wanaoshukiwa kuwa wanachama wa Al-Shabaab kuingia katika jamii za eneo hilo. "Ujasusi wetu umeonyesha kiwango kikubwa cha wapiganaji hao kupenyeza katika jamii zetu. Hili bado ni tishio kubwa kwa usalama wetu," alisema afisa huyo. Ripoti za kijasusi za Julai 31 zilionyesha kuwa wafugaji wanaoishi karibu na mpaka wa Kenya na Somalia waliona watu waliokuwa wamejihami kwa silaha nzito. Wafugaji hao waliwaambia maafisa wa usalama kuwa wapiganaji hao walikuwa wameanzisha kambi za muda karibu na mpaka na kuwaonya wakazi wasikaribie maeneo hayo. Mnamo Julai 28, washukiwa wa Al-Shabaab waliwavizia maafisa wa usalama waliokuwa katika doria eneo la Quraqura-Wante, Mandera, na kuwaua maafisa watano. Wanne kati ya waliouawa walitoka Kikosi Maalumu cha Operesheni huku mwingine akiwa polisi wa akiba. Kilipuzi kingine kilicholenga kikosi cha maafisa waliokuwa wakija kutoa msaada kililipuka na kuharibu gari la polisi. Shirika la Armed Conflict Location and Event Data (ACLED) limesema ongezeko hilo ni sehemu ya wimbi pana la mashambulizi ya Al-Shabaab katika kaunti za Kaskazini Mashariki na Lamu. ACLED ilirekodi visa 25 vikiwemo vilipuzi viwili vilivyodhibitiwa katika Mandera, Garissa, Wajir na Lamu katika kipindi cha miezi miwili iliyopita. Shirika hilo limesema baadhi ya wapiganaji hao wanakimbilia upande wa Kenya kutokana na operesheni kali za kijeshi nchini Somalia. Maafisa wa usalama pia wamehusisha ongezeko hilo na mpaka usio na ulinzi wa kutosha, uajiri wa vijana katika makundi ya kigaidi na mapigano yanayoendelea upande wa Somalia. MCA wa Garissa Hajir Dahiye ameitaka serikali kupitia upya sera yake kuhusu Jubaland, akisema usalama wa Garissa hauwezi kutenganishwa na hali ya usalama katika eneo hilo la Somalia. Mnamo Julai 26, washukiwa wa Al-Shabaab walivamia kijiji cha Abakaile, Dadaab, na kuharibu mnara wa mawasiliano. Hakuna aliyejeruhiwa katika shambulio hilo. Julai 17, washukiwa hao walifanya mashambulizi yaliyofuatana katika miji ya Fino na Arabia, Mandera, na kusababisha hofu miongoni mwa wakazi. Barabara ya Elwak-Lafey-Mandera imekuwa imefungwa kwa umma tangu 2015 kutokana na mashambulizi ya mara kwa mara na milipuko ya vilipuzi. Maafisa wa usalama pia wameonya kuhusu ushirikiano wa baadhi ya wenyeji na wanamgambo hao kwa kuwapa taarifa kuhusu mienendo ya maafisa wa usalama na vituo vya polisi. Mkazi wa Wajir Hassan Abdullahi alisema ukosefu wa ajira na ujinga miongoni mwa vijana unawafanya kuwa rahisi kuajiriwa na makundi ya kigaidi. "Tunahitaji mpango wa kuwafikia wananchi kutoka mashinani hadi kitaifa ili kuwaelimisha vijana kuhusu hatari za ugaidi," alisema.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Sat, 08 Aug 2026 01:55:24

Lojini za bei nafuu Eldoret zageuka 'mitego ya kifo' baada ya wanawake wawili kuuawa

WANAHARAKATI wa haki za binadamu na wanaotetea wafanyabiashara wa ngono wameonya kuhusu ongezeko la mauaji ya wanawake Eldoret baada ya wanawake wawili kuuawa katika visa viwili tofauti ndani ya siku tano. Visa hivyo vimeibua wasiwasi kuhusu usalama katika nyumba za kulala ambazo wakazi wanasema zimegeuka kuwa maeneo hatari kwa uhalifu. Kisa cha hivi majuzi kilitokea Alhamisi asubuhi katika mtaa wa Kipkaren ambapo mwili wa mwanamke mwenye umri wa miaka 26 ulipatikana umefungwa kwenye gunia na kutupwa katika nyumba ya kupanga baada ya waliokuwa wakiishi humo kutoroka. Siku chache kabla ya hapo, mwili wa mwanamke mwenye umri wa miaka 38, aliyetambuliwa na wenzake kwa jina la Zeddy, ulipatikana katika nyumba ya gesti eneo la Juakali, kando ya barabara kuu ya Eldoret-Webuye. Mauaji hayo yameongeza hofu miongoni mwa wanawake wanaofanya biashara ya ngono, huku mashirika ya haki yakisema yanaweza kuwa sehemu ya mtindo unaoibuka wa mauaji yanayowalenga wanawake walio katika mazingira hatari. Wakazi wanasema baadhi ya nyumba hizo za kulala wageni hazina rejista za wageni, kamera za usalama wala mifumo madhubuti ya kudhibiti wanaoingia na kutoka. Kiongozi wa Nyumba Kumi eneo hilo, Solomon Musumi, alisema Zeddy alikuwa akiishi katika mojawapo ya vyumba hivyo. Alisema Jumatatu usiku alipokea mwanaume aliyedhaniwa kuwa mteja, kabla ya wanawake waliokuwa katika vyumba vya jirani kugundua mwili wake asubuhi iliyofuata. "Eneo hili haliwezi kuendelea kuwa maficho ya wauaji. Nyumba hizi hazina rejista za wageni wala kamera za usalama, na hivyo kuwa mitego ya kifo," alisema Musumi. Polisi wamethibitisha wameanzisha uchunguzi kuhusu visa hivyo. Kamanda wa Polisi kaunti ndogo ya Kapseret Zaphaniah Kamren alisema washukiwa wawili wamekamatwa kuhusiana na mauaji ya Kipkaren. "Tunaahidi umma kuwa hatutakoma hadi waliohusika na vitendo hivi vya kinyama wakabiliwe na sheria," alisema. Kwa upande mwingine, Kamanda wa Polisi wa Turbo Patrick Wekesa alisema uchunguzi kuhusu kifo cha Zeddy unaendelea.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Sat, 08 Aug 2026 00:55:30

DCI imefichua kuwa maafisa walilipwa kumuuwa Dkt Mutiso

WAPELELEZI wametaja Konstebo wa Polisi Elijah Kibelion Kimoi kuwa ndiye aliyempiga risasi na kumuua Daktari Victoria Mutiso katika shambulizi la kikatili lililotokea wiki iliyopita. Idara ya Uchunguzi wa Jinai (DCI) ilisema Ijumaa kuwa Kimoi, ambaye tayari amekamatwa, alitumia bastola ya polisi kumuua Dkt Mutiso. DCI pia ilimtaja raia Daniel Mwangi Njoroge kuwa mmoja wa waliopanga mauaji hayo. Kulingana na DCI, Njoroge aliajiriwa na mwanasiasa Rose Mbithe Mulwa na mwanawe Christopher Mulwa kwa lengo la kumuua Dkt Mutiso. Inadaiwa mauaji hayo yalitokana na mzozo wa muda mrefu wa kifamilia kuhusu ardhi ya ukubwa wa ekari 20 huko Mlolongo, Machakos. Bi Mulwa amekuwa akizozania ardhi hiyo na aliyekuwa mumewe, Dkt David Musyimi Ndetei, pamoja na mkewe Dkt Mutiso tangu 2001. Mkuu wa DCI Mohamed Amin alisema Njoroge alikodi magari mawili aina ya Toyota Prado kutekeleza mauaji hayo. Alisema Njoroge pia alishirikiana na mhudumu wa bodaboda Kelvin Ngugi Kinuthia, ambaye anadaiwa kumsafirisha Kimoi hadi eneo la tukio na baadaye kumtorosha. Dkt Mutiso alikuwa akisafiri katika teksi ya Uber iliyokuwa ikiendeshwa na Victor Job Chunguli mnamo Julai 29. Walipofika eneo la Mawensi, Upper Hill, Nairobi, Toyota Prado nyeusi ilizuia teksi hiyo.Pikipiki pia ilisimama karibu nao. Mtu aliyekuwa ameketi kiti cha nyuma cha pikipiki alifyatua risasi kadhaa kuelekea Dkt Mutiso kabla ya pikipiki na Prado kutoroka. Bw Chunguli alimpeleka Dkt Mutiso katika Hospitali ya Kitaifa ya Kenyatta, lakini akatangazwa kuwa amefariki alipowasili. Bw Amin alisema baada ya kuwahoji Njoroge na Kinuthia, wawili hao waliwapeleka wapelelezi kwa maafisa watatu wa polisi. Walitajwa kuwa Inspekta Kenneth Kipkemboi Sang, Konstebo Elijah Kibelion Kimoi na Konstebo Collins Kiplangat Bett. Kimoi amekamatwa huku Sang na Bett wakitoroka na wanaendelea kusakwa na polisi . "Kushiriki kwa maafisa hawa ni usaliti mkubwa kwa sare ya polisi na imani ambayo umma umeweka kwao. Lazima wachukuliwe hatua," alisema Bw Amin. Bw Amin pia alisema bastola iliyotumiwa kumuua Dkt Mutiso ilikuwa ya polisi na ilikuwa imewekwa katika kituo kidogo cha polisi cha Nderi, chini ya Kituo cha Polisi cha Kikuyu. Wapelelezi walipokagua sanduku la kuhifadhia silaha katika kituo hicho, walipata bastola aina ya Mini Jericho yenye nambari KP47302127 pamoja na magazini iliyokuwa na risasi 12 za milimita tisa. Ukaguzi wa rejista ya utoaji wa silaha ulionyesha kuwa bastola hiyo ilikuwa imetolewa kwa Inspekta Sang. Silaha hiyo ilipelekwa katika maabara ya uchunguzi wa kisayansi ya Huduma ya Kitaifa ya Polisi kwa uchunguzi wa risasi. Kulingana na DCI, uchunguzi ulithibitisha kuwa bastola hiyo ndiyo iliyotumiwa katika kumuua Dkt Mutiso. Maganda ya risasi yaliyopatikana eneo la tukio na kichwa cha risasi kilichopatikana mwilini mwa marehemu wakati wa uchunguzi wa mwili vililingana na risasi kutoka kwa bastola hiyo. Bastola hiyo pamoja na pikipiki ya Kinuthia zimechukuliwa na polisi kama ushahidi. Uchunguzi wa mauaji hayo ulihusisha pia kuangalia picha za kamera za usalama, ushahidi wa kisayansi na taarifa nyingine za kijasusi. DCI ilisema ushahidi uliopatikana unaonyesha kuwa baadhi ya washukiwa wa mauaji ya Dkt Mutiso huenda pia walihusika katika mauaji ya wakili Kyalo Mbobu mnamo Septemba 9, 2025. Mbobu alipigwa risasi na mtu aliyekuwa nyuma ya pikipiki akiendesha gari kuelekea nyumbani kando ya Barabara ya Magadi. Mauaji hayo yalifanana na yaliyompata Dkt Mutiso kwa kuwa mshambuliaji alitumia pikipiki. Bw Amin pia alidai kuwa matamshi ya Naibu Rais wa zamani Rigathi Gachagua kuhusu uchunguzi huo huenda yalifikia Sang na Bett na kuwafanya kutoroka. Alimtaka Bw Gachagua kuwasilisha kwa DCI taarifa yoyote aliyo nayo ambayo inaweza kusaidia uchunguzi wa mauaji hayo. Bw Gachagua alikuwa amedai kuwa maafisa wawili wa polisi kutoka Kituo cha Polisi cha Kikuyu walihusika katika mauaji ya Dkt Mutiso. Alisema madai yake yalitokana na "taarifa za kuaminika". "Maafisa hawa wawili katika Kituo cha Polisi cha Kikuyu ndio waliomuua wakili Kyalo Mbobu na pia Dkt Victoria Mutiso," Bw Gachagua alisema.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Fri, 07 Aug 2026 23:55:58

Umoja: Kalonzo ateua washirika wa Gachagua katika uongozi wa Wiper

KIONGOZI wa Wiper Patriotic Front , Kalonzo Musyoka Ijumaa alitangaza mabadiliko katika uongozi wa chama hicho kwa kuwateua washirika wa aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua, huku akilenga kuonyesha umoja wa upinzani kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2027. Bw Musyoka alimteua aliyekuwa waziri, Jamleck Kamau kuwa mwenyekiti wa chama, Mbunge wa Nyali, Mohamed Ali kuwa naibu kiongozi wa chama, na wakili wa masuala ya Katiba Ndegwa Njiru kuwa msemaji wa chama. Uteuzi huo ulianza kutekelezwa mara moja na unaashiria upanuzi mkubwa wa uongozi wa Wiper vyama vya upinzani vinapoendelea na mashauriano kuhusu muungano w kukabiliana na Rais William Ruto mwaka 2027. Bw Kamau, ambaye pia aliwahi kuwa Mbunge wa Kigumo, amewahi kuhusishwa kisiasa na Bw Gachagua, huku Bw Njiru akiwa mmoja wa mawakili mashuhuri waliowahi kumtetea kiongozi huyo wa DCP. Bw Musyoka alisema uteuzi huo ulitokana na jukumu alilopewa na wajumbe wa chama wakati wa Kongamano la Kitaifa la Wajumbe la Oktoba 10 mwaka jana. "Jukumu la kwanza nililopewa na wajumbe lilikuwa kutafuta urais wa Jamhuri ya Kenya mnamo Agosti 2027. Jukumu la pili lilikuwa kupanua na kujenga uongozi wa chama hiki hadi kiwe sura ya Kenya," alisema. Alisema mabadiliko hayo ni sehemu ya juhudi za kuimarisha Wiper pamoja na muungano mpana wa upinzani kuelekea uchaguzi wa 2027. Bw Musyoka alisema mashauriano yanaendelea kuunganisha vyama vinavyopinga utawala wa Rais Ruto chini ya mwavuli mmoja wa kisiasa. "Huu si uteuzi wa kujipendekeza, bali ni uteuzi wa imani. Kila mmoja wao anafaa kikamilifu katika chama ambacho ajenda yake pekee ni 'Komboa Kenya'," alisema. Kando na mabadiliko hayo ya uongozi, Bw Musyoka alisema hataruhusu tofauti kati ya viongozi wa upinzani kuvuruga juhudi za kuunda muungano mmoja dhidi ya Rais Ruto. Alisema viongozi wa upinzani wanaendelea na mashauriano ya kuleta pamoja Wakenya na akaonya kuwa mgawanyiko utawanufaisha viongozi wa Kenya Kwanza. "Tunapoendelea na kazi hii, mashauriano yanaendelea ili kuleta upinzani chini ya mwavuli mmoja wa kuaminika. Tumekubaliana kuwa mgawanyiko ndiyo mkakati pekee wa utawala huu," alisema. Bw Musyoka pia aliwataka Wakenya kutotafsiri tofauti zinazojitokeza kati ya viongozi wa upinzani kama ishara kwamba mchakato wa kuunda muungano umevunjika. "Hata mkiona tofauti kati ya viongozi wa vyama ndani ya muungano, tafadhali msizichukulie kwa uzito sana. Tumeungana kwa sababu tukigawanya upinzani, William Ruto atapata muhula wa pili," alisema. Alisema mashauriano yataendelea hadi vyama na viongozi wote wanaopinga serikali waungane. "Mashauriano hayo yanaendelea na hayatasitishwa hadi kila chama na kila kiongozi anayepinga serikali awe chini ya paa moja, tayari kuunda serikali moja inayosubiri kuchukua uongozi," alisema.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Fri, 07 Aug 2026 22:55:01

Hofu virusi vya ukimwi vikizidi kukosa kusikia dawa muhimu

WANASAYANSI wamegundua hali mpya ya kutisha ya virusi vya Ukimwi kuanza kustahimili dawa muhimu inayotumika katika matibabu ya ugonjwa huo katika nchi nne za Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara. Utafiti uliowasilishwa katika mkutano wa International Aids Society (IAS) mjini Rio de Janeiro, Brazil, umeonyesha hali hiyo miongoni mwa watu wanaoishi na Ukimwi nchini Kenya, Tanzania, Msumbiji na Lesotho. Watafiti wameonya kuwa hali hiyo ikiendelea, maambukizi mapya ya Ukimwi yanaweza kuongezeka. Kinga ya mwili ya wagonjwa ambao virusi vyao vitakuwa vimekuwa sugu kwa dawa hiyo inaweza pia kudhoofika na kuwa katika hatari ya kupata magonjwa mengine ambayo yanaweza kusababisha kifo. Dawa inayohusika ni dolutegravir, inayojulikana kwa kifupi kama DTG. Tangu 2018, dawa hiyo imekuwa chaguo la kwanza na la pili katika matibabu ya Ukimwi. Shirika la Afya Duniani (WHO) linasema DTG ina ufanisi mkubwa, ni rahisi kutumia na husababisha madhara machache ikilinganishwa na baadhi ya dawa nyingine zinazotumika. Dawa hiyo pia inajulikana kwa kuwa na uwezo mkubwa wa kuzuia virusi vya Ukimwi kuzoea na kustahimili matibabu. Daktari Loice Ombajo, mtafiti mkuu wa utafiti huo na mtaalamu wa magonjwa ya kuambukiza, alisema sampuli za kwanza za utafiti zilikusanywa kutoka kwa watu 2,994 katika vituo 131 nchini Kenya. Washiriki hao walikuwa wametumia matibabu yenye DTG kwa angalau miezi sita.  Baadhi ya washiriki waliopatikana kuwa na mabadiliko ya virusi yanayohusishwa na usugu wa DTG waliingizwa katika utafiti maalumu ili kupata ushahidi wa kusaidia kuboresha matibabu ya wagonjwa ambao dawa hiyo imeshindwa kuwasaidia. "Bado kuna ushahidi mdogo kuhusu namna ya kuwahudumia watu wanaoishi na Ukimwi ambao virusi vyao vimekuwa sugu kwa dolutegravir," alisema Dkt Ombajo. Alisema utafiti huo unalenga kutoa ushahidi utakaosaidia wataalamu kufanya maamuzi bora kuhusu matibabu ya wagonjwa hao. Takriban watu tisa kati ya 10 wanaotumia DTG hufikia kiwango ambacho virusi vya HIV havionekani kwa wingi katika damu. Hata hivyo, baadhi yao hushindwa kufikia kiwango hicho. Dkt Ombajo alisema sababu kubwa ni kutotumia dawa ipasavyo. Alisema baadhi ya wagonjwa huchoka kutumia dawa kila siku, wengine husahau, huku wengine wakikosa hamu ya kuendelea na matibabu kutokana na hali yao.  "Usipotumia dawa au ukaitumia mara kwa mara bila kufuata ratiba, virusi vinaweza kubadilika na kuwa sugu kwa dawa hiyo," alisema. Katika utafiti huo, watafiti walifanya kazi na washiriki waliokuwa hawatumii dawa ipasavyo ili kuwasaidia kuendelea na matibabu. Takriban asilimia 70 walifikia kiwango cha kudhibiti virusi, huku asilimia 30 wakishindwa. Watafiti walilenga kundi hilo kubaini iwapo kiwango kikubwa cha virusi kilisababishwa na kuzoea dawa. Waligundua kuwa watatu kati ya kila washiriki 10 katika kundi hilo virusi vilikuwa sugu kwa DTG. Dkt Ombajo alisema hali hiyo ni ya kutia wasiwasi kwa sababu dawa hiyo inaweza kushindwa kufanya kazi hata mgonjwa akiendelea kuitumia. Tatizo jingine ni gharama kubwa ya vipimo vya kubaini hali ya dawa kwa virusi, huku nchi nyingi zikikosa rasilimali za kutosha kufanya vipimo hivyo mara kwa mara. Utafiti pia ulibaini baadhi ya wanawake wajawazito na wanaonyonyesha wanakumbwa na hali hiyo. Alisema hali hiyo inaweza kuongeza hatari ya mama mwenye kiwango kikubwa cha virusi kumwambukiza mtoto au mwenzi wake wa ngono.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Fri, 07 Aug 2026 21:55:08

Wantam, tutam: Uchaguzi wa urais ulifaa kufanyika Agosti 2026 mahakama yasema

MAHAKAMA Kuu imesema uchaguzi ujao wa urais nchini ulifaa kufanyika Agosti 2026, badala ya 2027, lakini imekataa kuamuru uchaguzi huo uandaliwe mara moja ikisema hatua hiyo inaweza kutumbukiza nchi katika vurugu. Jaji wa Mahakama Kuu ya Malindi Mugure Thande alisema Katiba inahitaji uchaguzi wa urais ufanyike Jumanne ya pili ya Agosti katika mwaka wa tano baada ya uchaguzi mkuu uliopita. Jaji huyo alisema Ibara ya 136(2)(a) ya Katiba inataka uchaguzi huo ufanyike katika mwaka wa tano na si baada ya mwaka huo kukamilika. Alisema mwaka wa tano baada ya uchaguzi wa Agosti 9, 2022 ulianza Agosti 9, 2026. "Kufanya uchaguzi ujao wa urais katika tarehe nyingine yoyote isipokuwa Jumanne ya pili ya Agosti 2026 kutakiuka Katiba," Jaji Thande alisema. Hata hivyo, mahakama ilisimamisha utekelezaji wa uamuzi huo hadi baada ya uchaguzi mkuu ujao. Hatua hiyo inamaanisha kuwa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) haijaamrishwa kuandaa uchaguzi wa urais mwezi huu wa Agosti. Walalamishi katika kesi hiyo, Dkt Owiso Owiso, Khelef Khalifa na Ashioya Biko, walitaka mahakama itoe uamuzi kuhusu tarehe sahihi ya uchaguzi na pia iamuru IEBC kufanya uchaguzi huo Agosti 11, 2026. Jaji Thande alikataa ombi la kuamuru uchaguzi ufanyike mara moja. Alisema kesi hiyo iliwasilishwa Oktoba 2025 wakati maandalizi ya uchaguzi wa 2027 yalikuwa tayari yameanza. Alisema IEBC, wagombea watarajiwa na Wakenya kwa ujumla walikuwa tayari wamejiandaa kwa uchaguzi wa Agosti 2027. "Kuamuru tume ya uchaguzi kuandaa uchaguzi wa urais Agosti 2026 kutakuwa kutoa amri ambayo haiwezekani kutekelezwa kwa njia ya kiutendaji," alisema. Jaji huyo aliongeza kuwa hatua kama hiyo inaweza kuingiza nchi katika machafuko. Mahakama ilisema ililazimika kusawazisha utekelezaji wa Katiba na tahadhari ya kimahakama ili kuepuka kusababisha "vurugu kubwa kitaifa ambazo haziwezi kudhibitiwa". Mzozo huo ulitokana na tafsiri ya Ibara ya 136(2)(a), inayoweka wakati wa kufanyika kwa uchaguzi wa urais. Walalamishi walidai kuwa mwaka wa tano baada ya uchaguzi wa Agosti 9, 2022 ulianza Agosti 9, 2026 na kumalizika Agosti 8, 2027. Kwa hesabu hiyo, walisema Jumanne ya pili ya Agosti 2026, ambayo ni Agosti 11, ndiyo tarehe iliyowekwa na Katiba kwa uchaguzi. Walitegemea pia Ibara ya 259(5)(c), inayoweka namna vipindi vinavyotajwa kwa miaka vinavyopaswa kuhesabiwa. Walalamishi walitaja uchaguzi wa 2013 na 2017 kama mifano ya kuonyesha kuwa Katiba haimpi rais haki ya lazima ya kutawala kwa miaka mitano kamili iwapo kufanya hivyo kutapingana na tarehe iliyowekwa kikatiba ya uchaguzi. Jaji Thande pia alisema ratiba ya uchaguzi iliyowekwa na Katiba ina uzito kuliko dhana kwamba rais lazima atumikie miaka mitano kamili. Alisema IEBC inaposhindwa kutekeleza wajibu wake wa kikatiba, mahakama inaweza kuingilia kati. Hata hivyo, mahakama ilisitisha utekelezaji wa uamuzi kwamba uchaguzi utakaofanyika nje ya Agosti 2026 utakuwa batili hadi baada ya uchaguzi mkuu ujao. Hii ina maana kuwa ingawa mahakama imesema tarehe inayofaa kikatiba ilikuwa Agosti 2026, haijaamuru Kenya kufanya uchaguzi wa urais mwezi huo. Mahakama pia ilisema muhula wa rais si miaka mitano chini ya Ibara ya 136(2)(a), na kwamba, Ibara ya 142 au kifungu kingine chochote cha Katiba hakimpi rais muhula wa miaka mitano. Kesi hiyo iliwasilishwa kupitia kampuni ya mawakili ya Otieno Ogola Company Advocates na Osundwa Company Advocates. Miongoni mwa waliotajwa kuwa wahusika wenye maslahi katika kesi hiyo ni Chama cha Wanasheria Kenya (LSK), Katiba Institute, kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka, UDA, aliyekuwa Jaji Mkuu David Maraga, mwanaharakati Okiya Omtatah, mwanasiasa Jimi Wanjigi, aliyekuwa Waziri Fred Matiang'i na Kenya Human Rights Commission.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Thu, 06 Aug 2026 21:55:35

Ruto afufua mbinu za Moi kujenga mtandao wa ushawishi mashinani kuelekea uchaguzi mkuu

RAIS William Ruto anaonekana kufufua baadhi ya mikakati iliyotumiwa na mlezi wake wa siasa hayati rais Daniel arap Moi ya kuimarisha utawala wa mashinani, baada ya kuwatambua rasmi wazee wa vijiji na kuwaingiza katika mfumo wa Utawala wa Serikali ya Kitaifa (NGAO). Hatua hiyo imezua mjadala mpya kuhusu iwapo serikali inalenga kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi au inajenga upya mtandao wenye ushawishi mkubwa wa kisiasa kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027. Kwa miaka mingi, machifu, manaibu wao na makamishna wa mikoa walikuwa nguzo kuu ya serikali za Moi. Mbali na kusimamia usalama na utekelezaji wa sera za serikali, walitumiwa pia kuhamasisha wananchi kuunga mkono chama tawala cha Kanu. Lakini mfumo huo ulikosolewa vikali wakati wa harakati za kurejesha mfumo wa vyama vingi vya siasa miaka ya 1990, huku viongozi wa upinzani wakidai ulitumiwa kuwanyanyasa wakosoaji wa serikali na kuvuruga shughuli za kisiasa. Ingawa Katiba ya mwaka 2010 na ugatuzi ulipunguza mamlaka ya utawala huo, serikali zilizofuata ziliendelea kuuhifadhi kwa kuubadilisha na kuuita Utawala wa Serikali ya Kitaifa. Sasa, miaka 16 baadaye, Rais Ruto ameupanua zaidi kwa kuwaingiza rasmi wazee wa vijiji katika mfumo huo. Akizungumza katika Ikulu ya Nairobi mbele ya zaidi ya wazee wa vijiji 10,000 kutoka sehemu mbalimbali nchini, Rais alisema wazee 106,000 wameingizwa rasmi katika utawala wa mikoa. Alitangaza kuwa kila mmoja wao ataanza kupokea posho ya Sh3,000 kila mwezi, baada ya kuhudumu kwa miaka mingi bila malipo. Aidha, alisema serikali italipia bima yao ya afya kupitia Mamlaka ya Afya ya Jamii (SHA), kuwapatia simu za kisasa za kurahisisha kazi zao na kuongeza maafisa wa Polisi wa Utawala katika maeneo yao. Pia alimwagiza Waziri wa Fedha, Bw John Mbadi, kutenga fedha katika bajeti ya ziada ili serikali ilipie michango ya SHA kwa wazee hao, wake au waume wao pamoja na watoto wao kuanzia Januari 2027. Rais alisema lengo ni kuwapa wazee wa vijiji nafasi rasmi katika utawala wa serikali na kuimarisha ushirikiano wao na machifu, manaibu wa machifu na maafisa wengine wa serikali. Katibu wa Wizara ya Usalama wa Ndani, Dkt Raymond Omollo, alisema huo ni uamuzi wa kihistoria kwa sababu ni mara ya kwanza wazee wa vijiji kutambuliwa rasmi na kupewa malipo ya kila mwezi. Alisema hatua hiyo itaimarisha uongozi mashinani, kuongeza uwajibikaji na kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi. Hata hivyo, mkutano huo uligeuka wa kisiasa baada ya Kiongozi wa Wengi katika Bunge la Kitaifa, Bw Kimani Ichung'wah kuwataka wazee hao kumuunga mkono Rais Ruto katika uchaguzi wa 2027. "Mmengoja kutambuliwa kwa miaka mingi. Rais Ruto ametimiza ahadi hiyo. Mkumbukeni na wakati ukifika, muungeni pia," alisema Bw Ichung'wah. Gavana wa Mombasa, Bw Abdulswamad Nassir, pia alitaka Rais aungwe kwa muhula wa pili, akisema ametambua mchango wa wazee wa vijiji kwa kiwango ambacho hakijawahi kushuhudiwa. Mkuu wa Mawaziri, Bw Musalia Mudavadi, alisema serikali itaendelea kuwaunga mkono wazee hao ili kuimarisha usalama na huduma kwa wananchi, huku akieleza kuwa uongozi wa Rais Ruto umeifanya Kenya kuwa na ushawishi mkubwa zaidi barani Afrika. Lakini viongozi wa upinzani walikosoa mpango huo. Kiongozi wa chama cha DCP, Bw Rigathi Gachagua, alisema serikali imekuwa ikitoa ahadi nyingi ambazo hazijatekelezwa. "Aliahidi machifu vipakatalishi lakini mpaka leo hawajazipata. Sasa anawaahidi wazee wa vijiji simu za kisasa. Kwa nini wamwamini?" alihoji. Pia alisema baadhi ya wazee wa vijiji wamemweleza kuwa posho ya Sh3,000 haitoshi kukabiliana na gharama ya maisha. Wachambuzi wa siasa wanasema hatua ya serikali kuimarisha mtandao wa utawala mashinani inaweza kuboresha huduma kwa wananchi, lakini pia inaweza kupatia utawala huo uzito mkubwa wa kisiasa huku uchaguzi mkuu wa 2027 ukikaribia.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Thu, 06 Aug 2026 22:55:40

Jinsi ya kusafisha korodani na makosa yanayofanywa na wanaume

WANAUME wengi hawazingatii sana jinsi wanavyosafisha sehemu zao za siri. Wengi huamini kwamba kuoga kila siku kunatosha, lakini madaktari wa mfumo wa mkojo wanasema si kila wakati. Kutumia sabuni kali, kukaa muda mrefu na chupi zenye jasho au kupuuza usafi wa sehemu za siri kunaweza kusababisha mwasho, fangasi, harufu mbaya na matatizo mengine yanayoweza kuzuiliwa. Daktari mtaalamu wa mfumo wa mkojo, Dkt Victor Albert Okoth, anasema usafi wa korodani ni sehemu muhimu ya afya ya uzazi wa mwanaume. "Usafi mzuri ni kusafisha sehemu hizo bila kupita kiasi. Ngozi ya sehemu za siri ni nyepesi na kuisugua sana kunaweza kusababisha majeraha na mwasho," anasema. Anashauri wanaume waoge sehemu za siri angalau mara moja kila siku kwa kutumia maji ya uvuguvugu. Wakati wa kuoga, mwanaume anapaswa kuosha uume, korodani, kinena na eneo lililo kati ya korodani na njia ya haja kubwa. Kwa wanaume ambao hawajatahiriwa, anashauri wavute govi nyuma, waoshe sehemu iliyo chini yake vizuri, wasuuze kwa maji kisha warudishe govi mahali pake. "Hakuna haja ya kusugua korodani kwa nguvu. Tumia mikono. Kusudi ni kuondoa uchafu, si kuua kila kimelea," anasema. Dkt Okoth anaongeza kuwa wanaume wanaofanya mazoezi mara kwa mara, wanaofanya kazi nje au wanaokaa katika mazingira yenye joto wanapaswa kuoga tena baada ya kutoa jasho. Anasema jasho hutengeneza mazingira yenye unyevunyevu yanayochochea ukuaji wa fangasi na bakteria. "Hali ya hewa ya Kenya huwa na joto katika maeneo mengi. Kuoga baada ya mazoezi na kubadilisha chupi yenye jasho ni tabia muhimu ya kujikinga na maambukizi," anasema. Hata hivyo, anaonya kuwa kuosha sehemu hizo mara nyingi kupita kiasi kunaweza kuharibu kinga ya ngozi na kusababisha ukavu, mwasho na uvimbe. Dkt Okoth anashauri matumizi ya maji pekee au sabuni laini isiyo na manukato makali. Anasema wanaume wengi huamini sabuni zenye povu nyingi au harufu kali husafisha vizuri zaidi, jambo ambalo si kweli. Bidhaa kama dawa za kuondoa harufu vinaweza kusababisha mwasho isipokuwa kwa ushauri wa daktari. Baada ya kuoga, sehemu za siri zinapaswa kukaushwa vizuri kwa taulo safi. Anasema unyevunyevu unaobaki kwenye ngozi huchochea ukuaji wa fangasi. Kwa wanaume ambao hawajatahiriwa, sehemu iliyo chini ya govi inapaswa kukaushwa vizuri kabla ya kuirudisha. Pia anashauri wanaume kuvaa chupi zinazopitisha hewa na kuzibadilisha kila siku au mara moja zinapolowa na jasho. Dkt Okoth anasema makosa yanayofanywa mara nyingi ni kutosafisha chini ya govi, kutumia sabuni kali au manukato kwenye sehemu za siri, kuvaa chupi yenye jasho kwa muda mrefu na kunyoa nywele za sehemu za siri kwa ukali kiasi cha kujeruhi ngozi. Anasema kosa kubwa zaidi ni kudhani kila tatizo la sehemu za siri husababishwa na uchafu. "Harufu, vipele, uvimbe au usaha si lazima vitokane na ukosefu wa usafi. Magonjwa ya zinaa kama kisonono huenezwa kupitia ngono na yanahitaji uchunguzi na matibabu ya kitaalamu," anasema.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Thu, 06 Aug 2026 23:55:52

Linda Mwananchi yalenga ngome za Raila ambazo ODM inapambana kuzihifadhi kwa ajili ya Ruto

BAADA ya kufanya mikutano iliyofanikiwa katika kaunti za Bungoma na Trans Nzoia wiki mbili zilizopita, viongozi wa vuguvugu la Linda Mwananchi sasa wamehamishia kampeni zao katika ngome za kisiasa za aliyekuwa kinara wa ODM, Raila Odinga, wakilenga kuimarisha ushawishi wao huku wakipanua mtandao wao nchini. Vuguvugu hilo linaloongozwa na Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna, Gavana wa Siaya James Orengo, Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino na Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi, linatarajia kufanya mikutano Busia Ijumaa kabla ya kuelekea Kakamega Jumamosi na Jumapili. Viongozi hao wananuia kuvutia wafuasi wa ODM katika eneo la Magharibi huku chama hicho kikijitahidi kulinda ngome zake za jadi. Gavana wa Trans Nzoia George Natembeya, ambaye ameahidi kuunga mkono azma ya Bw Sifuna ya kuwania urais mwaka 2027, anatarajiwa kuwa mstari wa mbele katika juhudi za kuunganisha kura za jamii ya Mulembe kabla ya kampeni hizo kusambazwa kote nchini. Ziara ya Kakamega pia inalenga ngome ya viongozi wanaounga mkono Rais William Ruto akiwemo Waziri wa Vyama vya Ushirika Wycliffe Oparanya, Gavana Fernandes Barasa, Naibu Gavana Ayub Savula pamoja na zaidi ya wabunge wanane wanaounga mkono serikali jumuishi. Ziara hiyo inafanyika wiki chache baada ya Bw Oparanya kufanya mkutano Malava ambapo alipendekezwa kuwa mgombea mwenza wa Rais Ruto na kuahidi kuongoza juhudi za kuunganisha eneo la Magharibi kumuunga mkono Rais huku akiimarisha ODM. Mnamo Agosti 16, msafara wa Linda Mwananchi utaelekea Homa Bay, mojawapo ya ngome kuu za ODM, ukiongozwa na Gavana Orengo. Hii itakuwa mara ya pili kwa kundi hilo kuingia eneo la Luo Nyanza baada ya kufanya mkutano Kisumu. Bw Orengo pia analenga kuimarisha nafasi yake kama msemaji wa kisiasa wa jamii ya Waluo kupitia mikutano Homa Bay, Kisumu na Siaya, huku mipango ikisukwa kupeleka kampeni hizo Migori. Hata hivyo, maandalizi ya mkutano wa Homa Bay yamekumbwa na misukosuko baada ya kuripotiwa visa vya vurugu. Mratibu wa muda wa Linda Mwananchi katika eneo hilo, Samuel Nyauke, alishambuliwa na kundi la vijana waliomshutumu kwa kupuuza uongozi wa kisiasa wa eneo hilo. Mali iliharibiwa baada ya mawe kurushwa katika ofisi yake, huku vijana sita wakikamatwa na baadaye kuachiliwa. 'Kwa wanaotumia vurugu kulinda maeneo yao ya kisiasa, Kenya ni ya Wakenya wote. Hakuna vitisho vitakavyotuzuia. Tutakuwa Homa Bay kama ilivyopangwa,' alisema Bw Orengo. Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Taifa wa ODM ambaye pia ni Gavana wa Homa Bay, Gladys Wanga, aliwataka wakazi kudumisha amani na kuruhusu kila chama kufanya siasa kwa uhuru. 'ODM ilipigania uhuru wa kila Mkenya. Kila mtu ana haki ya kufika sehemu yoyote ya nchi na kuuza sera zake. Wanaotaka kuja Homa Bay wanakaribishwa,' alisema Bi Wanga. Aliwahimiza vijana kutoruhusu kutumiwa kuzua vurugu za kisiasa, akisisitiza kuwa tofauti za kisiasa hazipaswi kuvuruga amani. Bi Wanga alisisitiza kuwa Homa Bay bado ni ngome ya ODM, huku akifichua kuwa chama hicho kina mpango wa kuongeza wanachama wake na kuimarisha mtandao wake kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2027. Pia alithibitisha kuwa ODM itaendelea kushirikiana na serikali jumuishi na iko tayari kuanza mazungumzo na UDA kuhusu ushirikiano wa kisiasa kabla ya uchaguzi ujao. 'ODM inaamini katika ushirikishaji wa wote na kuheshimiana kati ya jamii mbalimbali. Tuko tayari kwa uchaguzi wa 2027 na hatuna hofu ya kukabiliana na yeyote,' alisema.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Fri, 07 Aug 2026 00:55:27

Wanamazingira wajaa hofu baada ya kunguru hatari kutoka India kutua jijini

KUNGURU wavamizi kutoka India, wanaojulikana kwa kuharibu mazingira na kuangamiza ndege wa asili, wameonekana kwa mara ya kwanza jijini Nairobi, hali iliyozua hofu miongoni mwa wataalamu wa uhifadhi wa mazingira. Ndege hao walionekana awali katika Soko la Burma na mfanyabiashara mmoja aliyewaona akawafukuza bila kujua hatari wanayoweza kusababisha. Hata hivyo, picha yao ilipofikia wataalamu wa uhifadhi, ilithibitisha hofu ambayo wamekuwa nayo kwa miaka mingi. Kunguru hao, wanaojulikana kama Indian house crow, wamekuwa wakisambaa kutoka ukanda wa Pwani na sasa wameingia Nairobi, zaidi ya kilomita 400 kutoka Mombasa. Kwa miaka mingi, wengi walidhani tatizo hilo lilikuwa la Mombasa pekee. Historia inaonyesha kuwa ndege hao waliletwa Zanzibar miaka ya 1890 kusaidia kusafisha taka za chakula bandarini. Walipoongezeka, walivuka hadi Mombasa mwishoni mwa miaka ya 1940 na kuenea haraka katika ukanda wa Pwani kutoka Diani hadi Lamu. Mtafiti wa Makavazi ya Kitaifa ya Kenya, Bw John Musina, alisema kuongezeka kwa idadi yao kuliwaruhusu kusonga kuelekea maeneo ya bara. "Wamekuwa wakifuata miundombinu kama barabara. Walivuka eneo Tsavo, wakafika Makindu na sasa wameingia Nairobi,' alisema. Alisema kunguru hao ni miongoni mwa viumbe hatari zaidi kwa sababu hushindana na ndege wa asili kwa makazi na chakula huku wakivamia viota vyao na kula mayai pamoja na vifaranga. "Wanazaana kwa kasi kubwa kuliko ndege wa hapa, hivyo kuwafanya kupungua," alisema. Kwa mujibu wa Bw Musina, taka zinazotupwa ovyo katika majaa zimekuwa chanzo kikubwa cha chakula kinachowafanya kuongezeka kwa kasi. "Majaa yanawapa chakula kingi. Hiyo huwafanya wazaane kuliko ilivyo kawaida. Ukifika Mombasa utaona jinsi walivyo waharibifu," alisema. Wataalamu sasa wana hofu kuwa iwapo kunguru hao wataenea Nairobi, wataathiri ndege wanaopatikana katika Hifadhi ya Taifa ya Nairobi, ambayo ni miongoni mwa hifadhi chache duniani zilizo ndani ya jiji kuu. Pia kuna wasiwasi kuwa idadi yao inaweza kuongeza hatari ya ndege kugongana na ndege za abiria katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta (JKIA) na Uwanja wa Wilson. Kwa sasa, Makavazi ya Kitaifa ya Kenya kwa ushirikiano na Huduma ya Wanyamapori Kenya (KWS) zimeanza kufanya uchunguzi kubaini idadi ya ndege hao na maeneo waliyotua. Hadi sasa wameonekana katika eneo la Shauri Moyo na Soko la Burma pekee.Musina alisema hatua za mapema zinaweza kuzuia kuenea kwao. "Tunataka kutumia mbinu zilizofanikiwa Mombasa ili kudhibiti idadi yao kabla hawajaongezeka Nairobi," alisema. Kenya pia inachunguza mbinu zilizotumiwa nchini Afrika Kusini na Sri Lanka kudhibiti ndege hao. Hata hivyo, Bw Musina alionya kuwa juhudi hizo haziwezi kufanikiwa bila ushirikiano wa nchi jirani. "Tukiwadhibiti hapa lakini wasidhibitiwe Tanzania, watarejea tena. Lazima tushirikiane kikanda," alisema.

read more