T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Sat, 05 Sep 2026 22:55:48

Sifuna na Orengo wazika tofauti zao za kisiasa kuelekea 2027

GAVANA wa Siaya, James Orengo na Seneta wa Nairobi, Edwin Sifuna, wameanza juhudi za kupunguza mvutano uliokuwa ukiongezeka ndani ya vuguvugu la Linda Mwananchi baada ya wiki moja ya ushindani wa kisiasa uliochochewa na tangazo la Orengo kwamba atawania urais. Viongozi hao wawili walikutana Ijumaa pamoja na Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino na wasaidizi wao wa karibu katika kikao ambacho duru za ndani zinasema kililenga kuwatuliza wafuasi wao na kuonyesha umoja kabla ya mikutano ijayo ya kisiasa. Mkutano huo ulifanyika siku chache baada ya Orengo kutangaza hadharani kwamba yuko tayari kushindania tiketi ya urais ya Linda Mwananchi dhidi ya Sifuna au mgombea mwingine yeyote, akisisitiza kuwa umoja wa upinzani haupaswi kuzuia viongozi wenye tofauti za malengo ya kisiasa. "Hakuna ubaya katika ushindani wa kisiasa ndani ya Linda Mwananchi au upinzani. Muhimu ni kuwa na mchakato wa kuaminika wa uteuzi na hatimaye tutoe mgombea mmoja wa kukabiliana na Rais William Ruto," alisema Orengo. Kauli hiyo ilizua wasiwasi miongoni mwa sehemu ya wafuasi wa vuguvugu hilo ambao tayari walikuwa wameanza kujipanga nyuma ya Sifuna kama mgombea wao wa urais. Baadhi ya viongozi wamekuwa wakimkosoa Orengo kwa kile wanachodai ni kuanzisha ushindani usio katika vuguvugu ambalo kwa kiasi kikubwa lilikuwa limekubaliana kuhusu mgombea wake wa urais. Gavana wa Trans Nzoia George Natembeya amesema kaulimbiu ya "Sisi Ndiyo Sifuna" ni ushahidi kuwa wananchi wengi tayari wameamua wanachotaka. Mbunge wa Bumula Jack Wamboka, ambaye ni mshirika wa karibu wa Sifuna, pia amekuwa mkosoaji mkubwa wa hatua ya Orengo. "Wakenya tayari wameamua ni nani wanayetaka apeperushe bendera ya vuguguvu hili katika uchaguzi wa 2027," amesema. Naye mwanasiasa Pauline Njoroge, akizungumza katika mkutano wa Linda Mwananchi mjini Meru, alisema wafuasi wengi wa Linda Mwananchi wanaamini Sifuna ndiye anafaa kugombea urais. "Wafuasi wetu wako wazi kabisa kwamba mgombea wao wa urais ni Edwin Sifuna," alisema. Hata hivyo, Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi alisema Linda Mwananchi inamheshimu Orengo kutokana na mchango wake mkubwa katika mageuzi ya kisiasa nchini, huku akisisitiza kuwa vuguguvu hilo lina mifumo ya ndani ya kutatua suala la mgombeaji wa urais. Kwa mujibu wa vyanzo vilivyoshiriki mazungumzo ya Ijumaa, Sifuna na Orengo walitaka kuonyesha umoja baada ya baadhi ya washirika wao kuanza kushambuliana kupitia majukwaa ya kisiasa. "Baadhi ya wafuasi wao walikuwa wameanza kueneza mashambulizi hasa dhidi ya Orengo baada ya kutangaza nia ya kuwania urais. Ndiyo maana viongozi hao waliona ni muhimu kukutana na kuonyesha mshikamano," alisema mmoja wa watu waliofahamu yaliyojiri. Muda wa mkutano huo unachukuliwa kuwa muhimu huku Linda Mwananchi ikijiandaa kwa mkutano mkubwa wa hadhara mjini Nairobi mnamo Septemba 13. Inatarajiwa kwamba mkutano huo utatumika kuendeleza ajenda ya vuguvugu hilo na kutangaza hatua zake zijazo za kisiasa. Duru nyingine zinasema kuwa Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino alihusika pakubwa katika kupanga kikao hicho. Inadaiwa kuwa Owino, ambaye anahusishwa na azma ya kuwania ugavana wa Nairobi, anataka kuhakikisha Linda Mwananchi inafanya mkutano huo ikiwa imeungana ili kuongeza nafasi zake za kisiasa dhidi ya Gavana Johnson Sakaja. Akizungumzia mkutano huo, Sifuna alikataa madai kwamba ulifanyika kwa sababu ya mvutano kuhusu urais. "Hakuna tatizo lolote. Tulikuwa tukipanga mkutano wetu wa Septemba 13," alisema seneta huyo. Hata hivyo, wachambuzi wanasema kuingia kwa Orengo katika kinyang'anyiro cha urais kumeweka wazi changamoto kubwa ndani ya vuguvugu hilo. Wafuasi wa Sifuna wanaamini kuwa tayari amejijengea umaarufu mkubwa kupitia mikutano ya hadhara na shughuli za mashinani. Kwa upande mwingine, Orengo anasisitiza kuwa umaarufu wa mikutano hautoshi kuchagua mgombea wa urais bila mchakato rasmi wa uteuzi. Orengo amekuwa akinukuu mifano ya historia ya siasa za upinzani nchini, ikiwemo mchakato wa ODM mwaka 2007 na mazungumzo ya upinzani yaliyozaa muungano wa Kibaki-Wamalwa mwaka 2002, akisema kuwa ushindani wa ndani si jambo jipya.

read more
T

taifaleo.nation.co.ke

@taifaleo Sat, 05 Sep 2026 21:55:18

Wanasiasa wanaocheza kamari hatari kuelekea 2027

UCHAGUZI mkuu wa mwaka wa 2027 unavyokaribia, siasa za Kenya zinashuhudia mwelekeo mpya ambapo baadhi ya viongozi waliochaguliwa wanaonekana kuwa tayari kuacha nyadhifa walizo nazo kwa sasa ili kutafuta kubwa na zenye mamlaka zaidi, ushawishi na umaarufu kitaifa. Kuanzia kwa maseneta wanaolenga ugavana, wabunge wanaotaka kuwa magavana, hadi magavana na wabunge wanaomezea mate urais, hali hii imegeuza uchaguzi wa 2027 kuwa mchezo hatari wa kubadilishana nafasi za kisiasa. Kwa baadhi ya viongozi, hatua hiyo ni ya kimkakati. Magavana wanaokamilisha mihula yao miwili hawana chaguo jingine isipokuwa kutafuta nafasi nyingine za kisiasa. Wengine wako tayari hata kuwania nyadhifa za chini ili waendelee kubaki katika uongozi. Hata hivyo, kwa wabunge na maseneta wengine, uamuzi huo ni hatari zaidi. Mbunge anayedhibiti vizuri eneo alilochaguliwa anaamua kuacha kiti chake salama ili kuwania ugavana wa kaunti nzima, huku maseneta wakihatarisha nyadhifa zao kwa kuwania ugavana.  Miongoni mwa viongozi maarufu waliotangaza au kuonyesha nia ya kuwania urais ni Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna, Gavana wa Siaya James Orengo na Mbunge wa Kiharu Ndindi Nyoro. Sifuna ameonyesha wazi kuwania urais kupitia vuguvugu la Linda Mwananchi. Kwa upande wake, Orengo amesema yuko tayari kushindania tiketi ya urais ya vuguvugu hilo dhidi ya Sifuna au mgombea mwingine yeyote. "Hakuna ubaya kuwa na viongozi wenye malengo tofauti ndani ya Linda Mwananchi au upinzani. Muhimu ni kuwa na mchakato wa haki wa uteuzi ili hatimaye tupate mgombea mmoja wa kumenyana na Rais William Ruto," akasema Orengo. Wachambuzi wa siasa wanasema kauli hiyo inaonesha changamoto inayokabili upinzani, yaani ikiwa viongozi wanaoshikilia nyadhifa muhimu wanapaswa kuhatarisha nafasi walizonazo kwa kuwania urais. Mbali na urais, viongozi wengi nchini wanahama kutoka nyadhifa walizonazo kuelekea ugavana.  Katika Kaunti ya Bungoma, Mbunge wa Westlands Tim Wanyonyi anajiandaa kuwania ugavana na anatarajiwa kukutana na Mbunge wa Kimilili Didmus Barasa katika kinyang'anyiro hicho. Barasa amemtaja Wanyonyi kama "mtalii wa kisiasa" kwa kubadilisha maeneo ya kuwania nyadhifa.  Nairobi pia imekuwa kitovu cha ushindani mkali. Wabunge Babu Owino wa Embakasi Mashariki, James Gakuya wa Embakasi Kaskazini na Ronald Karauri wa Kasarani wanatajwa kuwa miongoni mwa wanaojipanga kugombea ugavana katika jiji kuu. Hatua hiyo ni hatari kwa kuwa wanaacha maeneo yao ya uchaguzi yenye wapigakura wanaowafahamu na kuingia katika ushindani unaohusisha mamilioni ya wapigakura wa kaunti nzima. Katika Kaunti ya Siaya, Mbunge wa Ugenya David Ochieng' anataka kumrithi Orengo kama gavana. Kiongozi wa ODM Oburu Oginga tayari amemhimiza avunje chama chake cha Movement for Democracy and Growth na kujiunga na ODM ili kupata uungwaji mkono katika mbio hizo. Kisumu nayo imekuwa na orodha ndefu ya wanaotazamia kurithi Gavana Anyang' Nyong'o. Naibu Gavana Mathews Owili, Mbunge wa Kisumu ya Kati Joshua Oron, Mbunge wa Kisumu Magharibi Rosa Buyu, Mwakilishi wa Kike Ruth Odinga na Seneta Tom Ojienda wote wanatajwa kutamani ugavana. Katika Kaunti ya Migori, Mbunge wa Uriri Mark Nyamita ameweka macho yake kwenye ugavana. Kisii, Seneta Richard Onyonka tayari ametangaza wazi kuwa atapambana na Gavana Simba Arati mwaka 2027. "Ninagombea ugavana wa Kisii mwaka wa 2027, hilo ni jambo la uhakika," akasema Onyonka. Mwelekeo huo unaonekana pia Magharibi mwa Kenya ambapo Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi na Seneta wa Kakamega Boni Khalwale wanalenga ugavana wa kaunti zao. Orodha ya maseneta wanaowania ugavana pia inajumuisha James Murango (Kirinyaga), Kanar Seki (Kajiado), James Lomenen (Turkana), Danson Mungatana (Tana River), Abass Sheikh (Wajir), Fatuma Dullo (Isiolo) na Enoch Wambua (Kitui). Kwa mujibu wa wachambuzi, maseneta tayari wana mamlaka ya kisiasa yanayoenea katika kaunti nzima, lakini ili wawe magavana, lazima washinde tena kura za wananchi na wapitie changamoto za uteuzi wa vyama, siasa za kikabila, fedha za kampeni na ushindani kutoka kwa walio madarakani. Swali kuu linaloibuka ni: kwa nini mwanasiasa aache kiti alicho nacho tayari? Mchambuzi wa siasa Javas Bigambo anasema wanasiasa wana haki ya kikatiba kuwania nyadhifa wanazotaka.  Akizungumzia azma ya urais ya Ndindi Nyoro, alisema hakuna mtu au kundi lenye mamlaka ya kuzuia wengine kutumia haki zao za kisiasa. "Hakuna mtu mwenye haki ya kumiliki eneo au wadhifa kisiasa kana kwamba ni mali yake binafsi," anasema Bigambo.  Kisa cha Nyoro kinaonyesha hatari kubwa inayowakabili wanasiasa wanaoondoka katika ngome zao za kisiasa. Akiwa amejiondoa UDA na kuanzisha chama cha People's Party of Kenya, Nyoro ameonyesha nia ya kuwania urais na hata kudai kuwa anaweza kumshinda Rais Ruto mwaka 2027. Wachambuzi wanaonya kuwa uchaguzi wa 2027 unaweza kuwaacha viongozi wengi mashuhuri bila nyadhifa.

read more