taifaleo.nation.co.ke
@taifaleo Mon, 20 Jul 2026 00:55:23
Ruto kufungua rasmi kichinjio cha Sh1 bilioni kilichokamilika baada ya miaka 17
KICHINJIO cha kisasa mjini Isiolo cha thamani ya Sh1 bilioni kinatarajiwa kufunguliwa rasmi wiki ijayo, miaka 17 baada ya ujenzi wake kuanza. Kichinjio hicho kilifanyiwa majaribio ya kufanya kazi mnamo Ijumaa. Wakati wa majaribio hayo, ng'ombe, mbuzi na ngamia walichinjwa ili kupima ufaafu wa mashine na mifumo ya kisasa kabla ya uzinduzi wake unaotarajiwa kufanywa na Rais William Ruto. Mradi huo ulianza mnamo 2009, huku serikali ya Kaunti ya Isiolo ikichangia Sh538 milioni na serikali kuu ikitoa Sh451 milioni. Kichijio hicho kimejengwa kwenye ardhi ya ekari 500,000 na ina sehemu mbalimbali ambazo zitarahisisha na kuharakikisha shughuli za utayarishaji wa nyama. Afisa Mkuu wa Idara ya Mifugo katika Kaunti ya Isiolo, Godana Dida, alisema ng'ombe 300, ngamia 100 na kondoo pamoja na mbuzi 2,500 wanaweza kuchinjwa kila siku kwa muda wa saa nane. Msimamizi wa mradi huo, James Munyoki naye alisema kituo hicho kimejengwa kwa viwango vya kimataifa ili kuiwezesha Kenya kupanua mauzo ya nyama katika masoko ya nje. "Kichinjio cha Isiolo ni miongoni mwa kile cha kisasa zaidi katika Kusini mwa Afrika. Tumefuata miongozo ya Shirika la Afya Duniani (WHO) na viwango vya kimataifa vya usalama na usafi wa nyama," akasema Bw Munyoki. Mtaalamu wa usimamizi wa majitaka, Dkt Lucy Murira, alisema kichinjio hicho kitakuwa kikisafishwa na kutumia tena zaidi ya lita milioni mbili za maji taka kila siku kupitia mfumo unaoondoa harufu mbaya. Hata hivyo, Bw Dida alisema uwezo wa kuchinja mifugo 3,000 kwa siku unamaanisha kuwa Isiolo pekee haiwezi kukidhi mahitaji ya mifugo. "Tunashirikiana na kaunti jirani kubaini maeneo ya usambazaji wa mifugo. Kwa ushirikiano wa kaunti za Kaskazini na maeneo jirani, tutatosheleza mahitaji ya kichinjio hicho," akasema. Kichinjio hicho kitategemea kaunti za wafugaji ambazo zina zaidi ya ng'ombe milioni tatu, kondoo na mbuzi milioni 12.9 na ngamia zaidi ya milioni tatu. Mwenyekiti wa Chama cha Wafugaji wa Isiolo, Mohamed Wario, alisema mradi huo utawapa wafugaji soko la uhakika na kufungua nafasi za uwekezaji katika uzalishaji wa malisho na maeneo ya kunenepesha mifugo.
read moreOther Headlines
taifaleo.nation.co.ke
@taifaleo 50 minutes ago
Aladwa: Nitakuwa debeni na ODM lazima iungwe mkono kiti cha ugavana Nairobi
BAADHI ya viongozi wa ODM jijini Nairobi wamekataa wazo la kugawana nyadhifa za kisiasa na UDA kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2027, wakisisitiza kuwa ODM ndiyo inafaa kutoa mgombeaji wa ugavana wa Nairobi. Wakiongozwa na Mwenyekiti wa ODM Nairobi ambaye pia ni Mbunge wa Makadara, George Aladwa, viongozi hao walisema chama hicho kimekubaliana kumuunga mkono Rais William Ruto na Naibu wake Profesa Kithure Kindiki katika azma yao ya kutetea viti vyao mnamo 2027. Kwa hivyo ODM inastahili kupewa nafasi ya kuwania ugavana wa Nairobi na iungwe mkono na wanasiasa wa vyama vingine tanzu ndani ya Kenya Kwanza. "Kiti cha ugavana wa Nairobi lazima kibaki ODM na hakuna njia ya mkato kuhusu hilo. Tumesema tutamuunga mkono Rais Ruto na Naibu wake katika uchaguzi ujao. Hatutaki siasa za ugavi wa nyadhifa katika ngome za ODM," alisema Bw Aladwa. Mbunge huyo pia alitangaza rasmi nia yake ya kuwania ugavana wa Nairobi. "Nimeijenga na kuihudumia ODM kwa miaka mingi pamoja na marehemu Raila Odinga. Wale wanaopanga kujiunga na chama wawe tayari kwa mchujo. Madiwani na wajumbe wengi wako nyuma yangu, na mchujo utakuwa wa haki na uwazi," akaongeza. Bw Aladwa pia alimtetea Inspekta Jenerali wa Polisi Douglas Kanja, akimtuhumu aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua kwa kuwashambulia viongozi ambao anajua hawatajibu matamshi yake hadharani. "Kanja alipitia taratibu zote za kuajiriwa na akathibitishwa kisheria. Gachagua aache kusambaza propaganda na amruhusu afanye kazi yake bila kuingiliwa," alisema. Viongozi hao walimtaka Waziri wa Usalama wa Ndani, Kipchumba Murkomen kuchukua hatua dhidi ya Bw Gachagua wakidai matamshi yake yanayolenga jamii fulani yanaweza kuchochea mvutano wa kisiasa. "Akihitaji kutofautiana na Rais afanye hivyo bila kuwahusisha wananchi wengine. Anapaswa kuheshimu Rais ambaye alichaguliwa na Wakenya," akasema. Aidha, walimtetea Waziri wa Afya Aden Duale, wakisema kauli tata anazodaiwa kutoa zilifasiriwa vibaya na baadhi ya viongozi kwa ajili ya maslahi ya kisiasa. "Hakuna jamii iliyo bora kuliko nyingine nchini Kenya. Wanaomshambulia Duale wanapaswa kwanza kumkosoa Gachagua kwa matamshi yake," akasema Bw Aladwa. Bw Aladwa ndiye mgombeaji pekee wa ODM kutoka mrengo unaoongozwa na Dkt Oburu Oginga ambaye ametangaza analenga ugavana wa Nairobi. Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino pia anataka ugavana ila kuna uwezekano finyu atatumia ODM kwa sababu anaegemea mrengo wa Linda Mwananchi.
read moretaifaleo.nation.co.ke
@taifaleo 1 hours ago
Ruto amwaga miradi ya mamilioni Magharibi, Oparanya akipigiwa debe 2027
RAIS William Ruto jana alisema serikali yake itaendelea kutekeleza miradi ya mabilioni ya pesa Magharibi mwa nchi huku wabunge wanaounga serikali yake wakiahidi kuwa eneo hilo litaendelea kuunga serikali katika Uchaguzi Mkuu wa 2027. Kiongozi wa nchi jana alikuwa katika Kaunti ya Busia ambapo alipigia debe miradi ambayo serikali yake imetekeleza na inaendelea kutekeleza kuinua eneo hilo kimaendeleo. Kwa upande mwingine, Kiongozi wa Wachache katika Bunge, Junet Mohamed, Waziri wa Vyama vya Ushirika Wycliffe Oparanya na wabunge wa ODM na UDA nao walishiriki mchango eneobunge la Malava ambapo walipuuza umaarufu wa Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna. Huku Rais akiwa Busia, kundi la wabunge wa chama cha ODM likiwa Magharibi nalo lilisema kuwa Bw Oparanya ndiye atakuwa mgombeaji mwenza wa Rais 2027. "Watu wakuje polepole na wajue huwezi kuruka laini na wajue kuna watu walikaa na Raila miaka na mikaka. Oparanya ndiye anatosha kutuongoza hapa Magharibi kama kiongozi wa ODM baada ya Oburu Oginga. UDA wakipata rais, sisi ODM lazima tupate naibu rais na huyo ni Oparanya," akasema Bw Mohamed. "Hii pesa yote ambayo inataka kugawanya ODM ni pesa ya Uhuru Kenyatta na ndiyo anatumia kugawa chama chetu lakini hatafaulu. Kama Uhuru alishindwa kufanya baba kuwa rais 2022 sasa ndiye atasaidia mtu yeyote, sisi hatuwezi kuelekea barabara hiyo," akaongeza mbunge huyo wa Suna Mashariki. Mbunge huyo alisisitiza kuwa ODM haitarejelea siasa za maasi na nguvu zao zote sasa ni kuhakikisha kuwa chama kitaendelea kuwa imara. Bw Oparanya alisema amekuwa na uzoefu wa siasa na hatikiswi na wimbi la Bw Sifuna huku akisema kuwa hawezi kusaliti ndoto ya marehemu Raila Odinga. "Mimi mpaka watu wamekuja kuniambia nitengeneze chama kipya lakini nikakataa. Hakuna kiongozi ambaye alikuwa na ufuasi kuliko Raila na wakati huu kama Magharibi tunaingia moja kwa moja kwa serikali ya Rais Ruto," akasema Bw Oparanya. Rais Ruto alisema eneo la Magharibi ni sehemu ya nchi wala haliwezi kuachwa nyuma huku maeneo mengine yakiendelea kupiga hatua kimaendeleo. Alitaja baadhi ya miradi ambayo serikali yake imetekeleza huku akijizuia kuzungumzia suala la umaarufu wa Sifuna. "Tulianzisha barabara ya Mundere kule Seo Port, Matayos na Funyula. Mliniuliza barabara kutoka Butula-Nambale-Amukura-Kocholia, na mwezi ujao nitakuja hapa kuanzisha barabara hiyo ya kilomita 58 kwa sababu nimepata mwanakandarasi," akasema Rais. Alikuwa akihutubu wakati wa kutawazwa kwa Askofu wa nne wa Kanisa la ACK Vitalis Job Ekuru, hafla ambayo pia ilihudhuriwa na Makamu wa Rais wa Uganda Jesca Alupe. "Tuna reli kutoka Narok na tumesema itakuja ifike hapa Malaba ili kurahisisha usafiri. Mimi na Rais wa Uganda Yoweri Museveni tulikubaliana huu ni mradi ambao tufanya pamoja kurahisisha usafiri na kusaidia nchi zetu kuimarisha uchumi," akaongeza Rais Ruto "Kuna barabara itakayofika hapa Malaba kutoka Mau Summit. Nitakuja kuzindua barabara ya Malava-Kimaeti-Bungoma. Barabara nyingine ambazo ziko hapa Busia ambazo ni kilomita 225 zimetengewa Sh5 bilioni na serikali," akasema Rais Ruto. Hafla hiyo ilihudhuriwa na Gavana Paul Otuoma, mwenzake wa Kakamega Fernandes Barasa na Kenneth Lusaka wa Bungoma miongoni mwa wabunge wengine kutoka Magharibi mwa Nchi. "Tumeweka Sh1.2 bilioni za kuongezea miradi ya stima hapa Busia. Nilikuja kuzindua soko Amagoro na tunaendelea kuwajengea masoko mengine 19 mapya kwa sababu tunataka wafanyabiashara wetu waendelee kufanya biashara mahali safi na kuna umeme," akasema "Tumetoa Sh3.6 bilioni kuwajenga wanafunzi nyumba kupitia mradi wa nyumba ili wasome mahali ambao kuna usafi na panatoshana," "Nimeona wengine wananiambia eti niondoke kwa serikali niunge mtu mwengine mkono (Sifuna) eti ataunda serikali nisiyoijua. Hao viongozi hawajui wanaenda wapi na wao watuheshimu badala ya kututusi ndipo tuwaunge mkono kwa lazima," akaongeza Bw Oparanya.
read moretaifaleo.nation.co.ke
@taifaleo 2 hours ago
Sifuna apokelewa kishujaa Magharibi, Wantam ikitanda hewani
ENEO la Magharibi limegeuka uwanja mkuu wa mapambano ya kisiasa kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2027, huku Rais William Ruto na viongozi wa upinzani wakilenga zaidi ya milioni 3.3. Magharibi kwa sasa ina jumla ya wapigakura waliosajiliwa milioni 2.92 katika kaunti tano, na inachukuliwa kuwa ngome muhimu inayoweza kuamua mshindi wa urais. Kufikia 2027, eneo hilo lenye kaunti za Bungoma, Kakamega, Trans Nzoia, Vihiga na Busia litakuwa na zaidi ya kura milioni 3.3. Katika uchaguzi wa 2022, Rais Ruto alipata ushindi mkubwa katika Kaunti ya Bungoma kwa kura 255,906, dhidi ya kura 145,280 za aliyekuwa mpinzani wake Raila Odinga. Matokeo hayo yalimsaidia kuingia Ikulu kwa tofauti ndogo ya kura. Sasa, ikiwa zimesalia chini ya miezi 12 kabla ya uchaguzi mkuu, vita vya kuhifadhi au kurejesha kura hizo vimeanza rasmi. umapili, Kiongozi wa kundi la Linda Mwananchi na Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna alikamilisha ziara ya siku mbili katika kaunti za Bungoma na Trans Nzoia huku Rais Ruto akiwa katika Kaunti ya Busia akizindua na kukagua miradi ya maendeleo. Pande zote mbili zilijitokeza zikisisitiza kuwa zinaungwa mkono na wakazi wa Magharibi. Katika mikutano yake, Bw Sifuna aliendelea kujisawiri kama mgombeaji anayetarajia kupeperusha bendera ya upinzani katika uchaguzi wa urais wa 2027, huku akiwataka wakazi wa Magharibi wasimwache njiani. "Watu wengi wanasema mnanipigia debe tu. Mmenihimiza niende hadi kwenye debe? Msije mkaniacha njiani. Simameni nami ili nikabiliane na Rais William Ruto uso kwa macho," akasema Alisema kundi la Linda Mwananchi limezunguka maeneo mengi nchini na kupokea ahadi za kuungwa mkono. "Nimeunda kikosi imara kutoka Pwani, Mlima Kenya, Nyanza, Magharibi na maeneo mengine. Kwa mapenzi ya Mungu, ndani ya miezi 12 tutakuwa tumekamilisha safari yetu kuelekea Ikulu," akaongeza. Bw Sifuna alisema safari yake ya kisiasa ilianzia Magharibi alipojaribu kuwania ubunge wa Kanduyi kabla ya marehemu Raila Odinga kumlea kisiasa na kumwezesha kuwa Seneta wa Nairobi, Katibu Mkuu wa ODM na Kiranja wa Wachache katika Seneti. Aidha, alidai kuwa viongozi wanaomuunga mkono Rais Ruto wanampotosha kwa kumwambia anaungwa mkono Bungoma. "Kuna watu wanamdanganya Rais kuwa ana kura Bungoma. Ukweli ni kwamba hana kura hapa. Safari ya mabadiliko tayari imeanza," akasema. Ziara hiyo ilihudhuriwa na Gavana wa Trans Nzoia George Natembeya, Gavana wa Siaya James Orengo, Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino, Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi na Waziri wa zamani Musikari Kombo ambaye alihudumu katika utawala wa marehemu Rais Mwai Kibaki. Tangu asubuhi, mamia ya wafuasi walifurika mjini Bungoma wakiwa na mabango yenye picha ya Bw Sifuna huku wakiimba nyimbo za jadi za Bukusu na nyimbo zilizokuwa zikitumika katika kampeni za marehemu Raila Odinga. Msafara huo ulianza kwa ibada katika Kanisa Kuu la St Immaculate mjini Kitale kabla ya kupitia Kiminini, Sikhendu, Kamukuywa, Kimilili, Chwele na Kanduyi. Katika ishara ya kumuunga mkono, wakazi walichangia kati ya Sh50 na Sh1,000 kufanikisha kampeni zake za urais. "Afadhali nidaiwe Sh10 na kila mwananchi wa Bungoma kuliko kudaiwa na tajiri mmoja ambaye baadaye atanitaka nimlipe kwa zabuni nikichaguliwa," akasema Bw Sifuna. Aliahidi kuwa serikali ya upinzani itafuta Ushuru wa Nyumba, ushuru wa mafuta na kodi nyingine alizosema zimekuwa mzigo kwa wananchi. Kwa upande wake, Gavana Natembeya alisema Magharibi imekuwa ikikosa nafasi za kisiasa kutokana na migawanyiko ya viongozi wake, akitoa wito wa kuungwa mkono kwa mgombeaji mmoja wa urais. "Historia yetu imejaa migawanyiko. Watu walidhani mimi na Sifuna tungepambana, lakini tuliketi na kukubaliana. Wenzangu wa upinzani wawe jasiri na waseme wazi, 'Sifuna tosha'," akasema Bw Natembeya. Aliwataka pia viongozi wa Nyanza kuunga mkono mgombeaji kutoka jamii ya Mulembe kama walivyofanya kwa Raila Odinga kwa miaka mingi. Viongozi hao pia waliwashambulia Gavana wa Bungoma Kenneth Lusaka na Mbunge wa Kimilili Didmus Barasa, kwa kumpotosha Rais Ruto kuwa Bw Natembeya alisema serikali ya upinzani itafuta Mamlaka ya Afya ya Jamii (SHA), Ushuru wa Nyumba, Mtaala wa Umilisi na Utendaji (CBC) na kodi nyingine alizodai zinawaumiza raia. Gavana Orengo alisema safari ya upinzani kuelekea Ikulu haiwezi kuzuiwa isipokuwa kupitia wizi wa kura, huku Seneta Osotsi akitaka kizazi kipya cha viongozi kupewa nafasi Magharibi. Naye Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino alisema Linda Mwananchi tayari imefanya ziara katika kaunti 16 na inalenga kufika kaunti zote 47 kabla ya 2027. Alisema baada ya Magharibi, kundi hilo litaelekea Nyanza, Kisii, Mlima Kenya na Ukambani kukutana na viongozi wa upinzani akiwemo Fred Matiang'i, Rigathi Gachagua na Kalonzo Musyoka ili kuunda muungano mmoja utakaompinga Rais Ruto mwakani.
read moretaifaleo.nation.co.ke
@taifaleo 15 hours ago
Mwanamume apigwa risasi Siaya wakazi wakipinga kiwanda cha nyuklia
MTU mmoja amelazwa hospitalini baada ya kupigwa risasi mguuni vurugu zilizozuka katika mkutano wa uhamasishaji kuhusu mradi wa kujenga kiwanda cha nyuklia cha thamani ya Sh1 trilioni katika eneo la Central Sakwa, Bondo, Kaunti ya Siaya, Ijumaa alasiri. Mkutano huo uliofanyika katika Kituo cha Biashara cha Ka'John ulihudhuriwa na maafisa wa KenGen, Shirika la Nishati na Umeme wa Nyuklia na Mbunge Gideon Ochanda. Waliokuwa wakielezea mradi huo kwa wakazi kabla ya vurugu kuzuka. David Otieno Mboya, mchimbaji mdogo wa madini kutoka kijiji cha Lenya, alisema hakuwa miongoni mwa waliohudhuria mkutano huo bali alikuwa akirejea nyumbani kutoka kazini alipopigwa risasi. "Nilikuwa napita karibu na eneo la mkutano vurugu zilipoanza. Wakazi walikuwa wakirusha mawe huku polisi wakifyatua risasi. Ghafla nilihisi maumivu makali kwenye mguu wa kushoto na nikagundua nimepigwa risasi," alisema. Alisema hajui iwapo alipigwa risasi na walinzi wa Mbunge Ochanda au maafisa wa polisi waliokuwa eneo hilo. Wasamaria wema walimkimbiza katika Hospitali ya Nango kabla ya kuhamishwa hadi Hospitali ya Bondo. Otieno alisema wakazi wengi wanapinga mradi huo kwa sababu utawalazimu kuhamishwa kutoka makazi yao ya muda mrefu. Mkazi mwingine, Otieno Ombok, alisema NuPEA imepuuza maswali ya jamii kuhusu usalama, fidia na uhamishaji wa wakazi, jambo lililosababisha hasira. Kamanda wa Polisi wa Bondo Peter Leparsare, alisema hakuna aliyekuwa ameripoti rasmi kupigwa risasi kufikia Ijumaa usiku, lakini alithibitisha kuwa polisi walifyatua risasi angani kutawanya umati baada ya mzozo kati ya wakazi na walinzi wa mbunge. Mradi huo ulihamishwa kutoka Kilifi hadi Siaya baada ya kupingwa na wakazi wa Kilifi. Serikali inapanga kuongeza uzalishaji wa umeme nchini kwa kati ya megawati 3,000 na 6,000 kupitia mradi huo. Gavana wa Siaya James Orengo amesisitiza kuwa mafanikio yake yatategemea ushirikishaji wa wananchi, uwazi na ridhaa kamili ya jamii itakayoathirika.
read moretaifaleo.nation.co.ke
@taifaleo 16 hours ago
Mtego wa kutoka jadi unaovunja upinzani ufikapo uchaguzi mkuu
KUGAWANYIKA kwa upinzani si jambo geni katika siasa za Kenya. Mwaka 1992, chama cha FORD kilichokuwa kimeibuka kama tishio kubwa kwa utawala wa KANU kilisambaratika baada ya viongozi wake Kenneth Matiba na Jaramogi Oginga Odinga kutofautiana kuhusu nani angewania urais. Kutoka kwa mgawanyiko huo vilizaliwa vyama vya FORD-Asili chini ya Matiba na FORD-Kenya chini ya Jaramogi. Badala ya kupambana na Rais Daniel arap Moi, viongozi hao waligeukiana, kila mmoja akidai ndiye aliyekuwa na haki ya kupeperusha bendera ya upinzani. Zaidi ya miaka 30 baadaye, hali kama hiyo inaonekana kujitokeza tena. Viongozi wa upinzani wanakubaliana kuwa Rais William Ruto anapaswa kukabiliwa na mgombea mmoja mwaka 2027. Hata hivyo, bado hawajakubaliana ni nani atakayebeba bendera hiyo. Muungano unaowaleta pamoja Rigathi Gachagua, Kalonzo Musyoka, Fred Matiang'i, Martha Karua, Eugene Wamalwa na Justin Muturi unasema unataka mgombea mmoja. Lakini kila upande unaonekana kutaka mgombea huyo atoke katika kambi yake. Wakati huo huo, kiongozi wa Safina Jimi Wanjigi ameendelea na mkakati wake tofauti. Kama alivyofanya Mwai Kibaki mwaka 1992, Wanjigi amesema atazingatia ajenda ya uchumi badala ya kujiingiza katika mvutano kuhusu nani anafaa kuongoza muungano. Kwa sasa, wafuasi wa upinzani hawaonekani tu kumpinga Rais Ruto, bali pia wanapambana wao kwa wao. Kila kambi inatumia matokeo ya kura za maoni na nguvu za maeneo yao kama ushahidi wa kwa nini mgombea wao anastahili kupewa tiketi. Historia ya FORD inaonyesha hatari iliyopo. Kwanza, KANU haikuiangusha FORD. FORD ilianguka kwa sababu ya migawanyiko yake yenyewe. Katika harakati za kutafuta mgombea bora, upinzani wa sasa unaweza kujikuta ukijenga migawanyiko itakayompa Ruto nafasi ya kushinda. Wakati FORD ilipoanzishwa, ilionekana kama serikali inayosubiri kuingia madarakani. Mikutano yake ilivutia umati mkubwa na viongozi wake waliheshimiwa kwa mchango wao katika mapambano ya kurejesha mfumo wa vyama vingi. Lakini chama hicho hakikuwahi kuafikiana kuhusu namna ya kumpata mgombea wake wa urais. Matokeo yake yalionekana wazi katika uchaguzi wa mwaka 1992. Upinzani uliingia uchaguzini ukiwa umegawanyika kati ya Matiba, Jaramogi na Kibaki. Moi aliibuka mshindi huku kura za upinzani zikigawanyika. Hilo lilichelewesha kuondolewa kwa KANU madarakani kwa takriban muongo mmoja. Leo, viongozi wa upinzani wanakabiliwa na mtihani kama huo. Gachagua amesema mgombeaji anaweza kutangazwa hata Mei 2027, ilhali Muturi ametaka uamuzi ufanywe mapema na tayari ameonyesha kumuunga mkono Kalonzo. Martha Karua pia amehoji mfumo unaopendekezwa wa kumpata mgombeaji. Wachambuzi wanasema miungano mingi haisambaratiki siku ya uchaguzi. Huvunjika mapema kila upande unapoanza kujijengea mtandao wake, kukusanya fedha na kuwashawishi wafuasi kuwa hakuna mgombeaji mwingine anayefaa. Hapo ndipo kinachoitwa athari ya Matiba huanza. Kila mwanasiasa anakubali umuhimu wa umoja, lakini kwa sharti kwamba umoja huo umuunge mkono yeye. Somo jingine muhimu ni kwamba sheria na taratibu zinapaswa kuwekwa kabla ya majina ya wagombeaji. FORD haikuwahi kukubaliana kuhusu mfumo wa kumpata mgombeaji wake, jambo lililochochea mzozo ulioigawa. Kwa upinzani wa sasa, bado hakuna makubaliano kuhusu sifa za mgombeaji, ratiba ya uteuzi wala mfumo wa kutatua migogoro. Historia pia inaonyesha kuwa umati mkubwa wa watu kwenye mikutano si lazima uwe ishara ya ushindi. Matiba aliporejea nchini mwaka 1992 na kupokelewa na maelfu ya watu, wengi waliamini alikuwa tayari ameshinda. Lakini mvutano kuhusu mgombeaji ndio uliovunja FORD. Aidha, muungano wowote unaotegemea tu kumpinga aliye madarakani huwa katika hatari ya kusambaratika. Swali ambalo Safina amekuwa ikiuliza ni: Baada ya Ruto, nini kitafuata? Kwa mujibu wa Wanjigi, upinzani unapaswa kueleza sera zake kuhusu ushuru, deni la taifa, ukosefu wa ajira, ufisadi, afya, elimu na gharama ya maisha badala ya kutegemea kaulimbiu ya "Wantam" pekee. Somo la mwisho ni kwamba umoja wa kweli huhitaji viongozi wengine kujinyima kwa manufaa ya lengo la pamoja. Hilo lilitokea mwaka 2002, Raila Odinga alipomuunga mkono Mwai Kibaki kwa kauli maarufu ya "Kibaki tosha", hatua iliyosaidia kuondoa KANU madarakani. Historia ya FORD si simulizi ya zamani tu. Ni onyo kwamba upinzani unaweza kuwa na uungwaji mkono mkubwa wa wananchi, lakini ukashindwa ikiwa viongozi wake watashindwa kuweka maslahi ya taifa mbele ya tamaa zao binafsi. Tatizo jingine ambalo lilichangia kusambaratika kwa FORD ni kwamba kila kiongozi aliamini historia yake ya kisiasa ilimpa haki ya kuwania urais. Jaramogi alijiona ndiye aliyekuwa amepigania demokrasia kwa miongo mingi dhidi ya tawala za Jomo Kenyatta na Daniel arap Moi. Kwa upande wake, Matiba aliamini mateso aliyopitia, ikiwa ni pamoja na kuzuiliwa bila kesi na kuugua kiharusi akiwa kizuizini, yalikuwa yamemjengea uhalali wa kuongoza upinzani. Kila mmoja alitumia historia yake kama msingi wa kudai tiketi ya urais. Hali kama hiyo inaonekana kujitokeza katika upinzani wa sasa. Baadhi ya viongozi wanategemea ukongwe wao kisiasa, wengine wanajivunia idadi ya wapiga kura kutoka maeneo yao, huku wengine wakisisitiza tajriba yao serikalini, uadilifu wao au mateso wanayodai kuyapata kutokana na kupambana na utawala uliopo. Ingawa hoja hizo zinaweza kuwapa nguvu kisiasa, hazitoshi kuwapa haki ya moja kwa moja ya kupeperusha bendera ya muungano. Kwa mujibu wa historia ya FORD, umoja wa kisiasa haujengwi kwa hoja za nani ameteseka zaidi au nani anaungwa mkono na watu wengi zaidi, bali kwa kuweka utaratibu unaokubalika na wote. Bila makubaliano ya wazi kuhusu namna ya kumpata mgombeaji na jinsi ya kushughulikia malalamishi yatakayojitokeza, tofauti za viongozi zinaweza kugeuka chanzo cha mgawanyiko na kuudhoofisha upinzani kabla hata ya kampeni rasmi kuanza.
read moretaifaleo.nation.co.ke
@taifaleo 16 hours ago
Ruto, Sifuna walumbana kuhusu 'uwezo wa kuku kupanda orofa ya 12' ya Affordable Housing
RAIS William Ruto na Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna wamezua mjadala mkali kuhusu ujenzi wa nyumba za ghorofa chini ya Mpango wa Nyumba za Gharama Nafuu, baada ya kutofautiana kuhusu iwapo nyumba hizo zinafaa kwa maisha ya wakazi wa Magharibi mwa Kenya. Mzozo huo ulianza baada ya Sifuna kuhoji ujenzi wa nyumba za orofa 12 katika eneo la Funyula, akisema hazilingani na mtindo wa maisha wa jamii za eneo hilo. Akizungumza kwenye mahojiano katika kituo cha redio cha Mulembe FM Jumatano, Julai 22, 2026, Sifuna alitumia mfano wa kufuga kuku kukosoa mpango huo. "Wamejenga nyumba za orofa 12 za gharama nafuu Funyula. Sisi Waluhya hatuwezi kuishi mahali ambapo kuku wetu hawawezi kuishi. Niambie, kuku wako atafikaje kwenye orofa ya 12?" alihoji. Rais Ruto alimjibu Alhamisi, Julai 23, wakati wa katika Ikulu ya Nairobi.
read moretaifaleo.nation.co.ke
@taifaleo 20 hours ago
Wataalam watetea kiwanda cha mafuta cha Dangote Lamu
WATAALAMU wa miundomsingi, viwanda na maendeleo ya kimaeneo wameutetea mradi wa Sh2.2 trillioni wa ujenzi wa kiwanda cha kusafisha mafuta ghafi Lamu. Kiwanda hicho kitafadhiliwa na kampuni ya Dangote Group kutoka nchini Nigeria inayomilikiwa na tajiri wa Afrika, Bw Aliko Dangote. Licha ya kiwanda hicho kutajwa kuwa na manufaa tele endapo kitawekezwa Lamu, Kenya, wenyeji wanasema kwamba lazima watambuliwe, kushirikishwa na matakwa yao kuzingatiwa kwanza kabla ya hatua zozote za kutekeleza mradi huo kuendelezwa maeneo yao. Katika mahojiano na Taifa Jumapili, wataalamu, ikiwemo wafanyakazi wa idara za serikali, waliutaja mradi huo wa kiwanda cha mafuta kuwa suluhu ya pekee itakayobadilisha eneo la Lamu kwa uzuri. Kamishna wa Petroli kwenye Wizara ya Kawi na Petroli nchini, Bw Joseph Otieno, alisema mradi huo utabadilisha eneo hilo kuwa jungu la kiviwanda na maendeleo. Bw Otieno alisema Kenya imekuwa ikinunua na kusafirisha bidhaa za petroli kwa bei ghali kutoka nje, hasa mataifa ya Mashariki ya Kati kupitia bandari ya Mombasa. "Watu wa Lamu waondoe shaka. Mradi utatekelezwa kwa kuwazingatia. Kutakuwa na mikutano na makongamano ya kuwaelimisha wenyeji na umma kwa jumla ili wauelewe vyema mradi. Kutakuwa na vikao vya wadau wa serikali, mwekezaji na wakazi wa mashinani Lamu ambao ndio wenyeji wa mradi," akasema Bw Otieno. Aliongeza, "Lamu itapanuka kimaendeleo. Barabara zitaboreshwa, biashara zitanoga na sekta zote kunufaika. Hata utendakazi wa bandari ya Lamu pia utaboreka na kufanyika kwa njia ya haraka endapo kutakuwepo na kiwanda cha mafuta." Afisa Mtendaji na Mkurugenzi Mkuu wa Zamani wa Mradi wa Bandari ya Lamu, Uchukuzi na Miundomsingi ya Kenya, Sudan Kusini na Ethiopia (LAPSSET), Dkt Silvester Kasuku alisema kuwekezwa kwa kiwanda cha Sh2.2 trilioni cha kusafisha mafuta kutaleta mwamko na taswira mpya ya Lamu kama eneo ambalo kihistoria lilikuwa limetelekezwa. Dkt Kasuku aliwahakikishia wakazi kwamba serikali itafanya kazi na kushirikiana nao kwa karibu wakati wa kutekelezwa kwa mradi huo. "Tushafanya kazi kwa karibu na jamii ya Lamu wakati tukitekeleza mradi wa Bandari ya Lamu na tukafaulu. Wananchi wa Lamu watambue kuwa tunawazingatia. Masuala ya ajira, utunzi wa mazingira, ufadhili wa kimasomo na mambo mengine, yote tutayajadili kwa pamoja na kuyakidhi katika kila hatua tutakazopiga wakati mradi utakapokuwa ukitekelezwa eneo hilo," akasema Dkt Kasuku. Mwenyekiti wa Zamani wa Muungano wa Save Lamu, Bw Mohamed Athman alitisha kuwa endapo vilio vyao kama jamii kuuhusu mradi vitakaidiwa basi hawatakuwa na budi ila kuelekea mahakamani kuuzuia mradi usifanyike eneo lao. Afisa Mtendaji wa Muungano wa Wanawake wa Lamu, Bi Raya Famau alishikilia haja ya jamii kuhusishwa kwenye vikao mbalimbali vya umma kutoa maoni kuhuuhusu mradi. Alisema wao hawapingi mradi ila furaha yao ni kuona haki zao za kijamii zikiheshimiwa. Naye Mwenyekiti wa Baraza la Wazee wa Lamu, Bw Shee Mbwana alimuomba mwekezaji, Bw Dangote kuweka kikao cha moja kwa moja na wanajamii ili waweze kutoa maoni na vilio vyao kuuhusu mradi. "Hatuna imani na serikali. Imekuwa ikitudhulumu ardhi zetu kila kunapowekezwa miradi mikuu eneo letu. Sasa tunamsihi Dangote afanye kikao cha moja kwa moja na sisi wanajamii ili tumpe vilio na mapendekezo yetu kabla mradi uendelee," akasema Bw Mbwana. Utakapokamilika, mradi huo utakuwa na uwezo wa kusafisha mapipa 700,000 ya mafuta ghafi kwa siku. Kiwanda hicho ambacho ni kikubwa zaidi Afrika Mashariki kinatarajiwa kujengwa kwa muda wa miaka mitatu. Kitasambaza bidhaa za petroli iliyosafishwa Kenya na pia nchi jirani, hivyo kupunguza hali ya ukanda wa Afrika Mashariki kutegemea mafuta yanayonunuliwa kutoka nje. Kiwanda hicho kinalengwa kujengwa eneo la Magogoni karibu na mradi wa Bandari ya Lamu ulioko Kililana, Lamu Magharibi.
read moretaifaleo.nation.co.ke
@taifaleo 18 hours ago
Salasya sasa adai Sifuna hana umaarufu kisiasa
HUKU viongozi vijana wakichangamkia kuimarika kwa umaarufu wa Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna, Mbunge wa Mumias Mashariki, Peter Salasya amepuuzilia mbali matokeo ya kura ya maoni uliofanywa na kampuni ya TIFA ambao kinara huyo wa Linda Mwananchi aling'aa. Akizungumza kupitia kurasa zake za mitandao ya kijamii Julai 24, 2026, mbunge huyo alidai kuwa utafiti huo ulifadhiliwa na Shirika la Kitaifa la Ujasusi (NIS) kwa lengo la kuzua mgawanyiko ndani ya muungano wa upinzani. Salasya alidai kuwa madhumuni ya utafiti huo yalikuwa kuonyesha kuwa vuguvugu la Linda Mwananchi linaungwa mkono zaidi kuliko muungano wa upinzani, jambo alilosema lilinuia kudhoofisha ushawishi wa viongozi wa upinzani kama kvile Kalonzo Musyoka na Rigathi Gachagua. Pia aliubeza utafiti huo kwa kejeli, akisema iwapo mwelekeo huo utaendelea, basi Sifuna atakuwa na asilimia 80 ya umaarufu katika utafiti ujao. Alisisitiza kuwa matokeo hayo hayana uhalali. "NIS wanafanya kazi ya punda kugawanya upinzani kwa kuonyesha Linda Mwananchi inaungwa mkono zaidi kuliko Muungano wa Upinzani. Tiketi ya Sifuna/Matiang'i sasa ndiyo inaongoza, na hivyo kumfanya Kalonzo na Rigathi waonekane si lolote kisiasa. Kwa kweli, wiki ijayo Sifuna atakuwa na asilimia 80 katika kura za maoni kama mgombeaji bora wa urais," alisema Salasya. Kauli za Salasya zilijiri muda mfupi baada ya TIFA kutoa matokeo ya utafiti wake wa hivi punde kuhusu wanaopendelewa kuwania urais, uliomweka Rais William Ruto kileleni kwa asilimia 24 ya uungwaji mkono. Kwa mujibu wa utafiti huo, Sifuna alishika nafasi ya pili kitaifa kwa kupata asilimia 15, na hivyo kuwa mwanasiasa wa upinzani aliyeongoza kwa umaarufu. Aliyekuwa Waziri wa Usalama wa Ndani Fred Matiang'i alifuatia kwa asilimia 14, huku kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka akishika nafasi ya nne kwa asilimia 13.
read moretaifaleo.nation.co.ke
@taifaleo 22 hours ago
Ndoa kati ya Ruto na Oburu ni ya kulazimisha- TIFA
Wakenya wengi wanapinga ushirikiano wa kisiasa kati ya ODM na UDA, hali inayozua maswali kuhusu mustakabali wa mpango huo kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027. Haya ni kwa mujibu wa utafiti mpya wa kampuni ya Trends and Insights for Africa (TIFA) uliofanywa kati ya Juni 13 na 22, 2026, ukihusisha watu 2,048 kutoka kaunti zote 47 nchini na ambao matokeo yake yalitolewa Ijumaa. Utafiti huo unaonyesha kuwa asilimia 52 ya Wakenya wanapinga Serikali Jumuishi, huku asilimia 30 pekee wakiunga mkono mpango huo. Asilimia 15 hawakuwa na maoni huku asilimia nne wakisema hawaufahamu ushirikiano huo. Matokeo hayo yanaonyesha kuwa licha ya ushirikiano wa karibu miaka miwili kati ya Rais William Ruto na ODM kufuatia maandamano ya Gen Z ya mwaka 2024, bado umma haujaukubalika kwa kiwango kikubwa. Kwa mujibu wa TIFA, kiwango cha uungwaji mkono kwa ndoa ya vyama hivyo kimeendelea kubaki karibu kilekile kwa mwaka mmoja uliopita. Kilikuwa asilimia 22 Mei 2025, kikaongezeka hadi asilimia 44 Agosti mwaka huo kabla ya kushuka hadi asilimia 30 Novemba 2025. Katika utafiti wa sasa, kimeendelea kusalia asilimia 30. Ripoti hiyo inasema mgawanyiko unaoendelea ndani ya ODM kuhusu iwapo chama hicho kinafaa kuunga mkono azma ya Rais Ruto ya kutetea urais mwaka 2027 umefunga kiwango ambacho ushirikiano huo unaweza kupata uungwaji mkono. Hakuna eneo lolote kati ya kanda tisa za utafiti lililoonyesha wengi wanaounga mkono ushirikiano huo. Eneo la kati la Bonde la Ufa linaongoza kwa asilimia 47 ya wanaounga ushirikiano huo, likifuatiwa na Kaskazini mwa Kenya kwa asilimia 43 na Nyanza kwa asilimia 35. Magharibi ina asilimia 29, Pwani asilimia 31, Kusini mwa Rift Valley asilimia 25, Nairobi asilimia 22, Kusini Mashariki asilimia 30 na Mlima Kenya asilimia 13. TIFA pia imebaini kuwa uungwaji mkono umeshuka kwa kasi zaidi Magharibi mwa Kenya, kutoka asilimia 62 Novemba 2025 hadi asilimia 29 sasa. Nyanza pia imeshuka kutoka asilimia 59 hadi 35, huku Mlima Kenya na Kaskazini mwa Kenya zikisajili kupungua kwa uungwaji mkono. Ripoti hiyo inahusisha hali hiyo na mvutano unaoendelea ndani ya ODM kati ya makundi ya Linda Mwananchi na Linda Ground kuhusu mustakabali wa chama na ushirikiano wake na Kenya Kwanza. Viongozi kama Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna, Gavana wa Siaya James Orengo na Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi wameendelea kupinga ushirikiano wa karibu na serikali. Wapigakura ambao hawajaamua Wakati huo huo, utafiti huo unaonyesha kuwa uchaguzi wa urais wa 2027 huenda ukaamuliwa katika maeneo yenye wapigakura wengi ambao bado hawajaamua upande wa kuunga mkono. Mlima Kenya, wenye takriban wapiga kura milioni 5.7, umejitokeza kuwa uwanja mkubwa wa kisiasa. Asilimia 25 ya wakazi wa eneo hilo bado hawajaamua mgombea watakayemuunga mkono. Nairobi pia imejitokeza kuwa uwanja muhimu wa kisiasa. Kalonzo anaongoza kwa asilimia 23, akifuatiwa kwa karibu na Sifuna kwa asilimia 22 na Matiang'i kwa asilimia 17. Rais Ruto anaungwa mkono na asilimia sita huku Gachagua akiwa na asilimia nane. Asilimia 21 ya wakazi wa jiji bado hawajaamua. Pwani pia imeonekana kuwa eneo la ushindani mkali. Sifuna anaongoza kwa asilimia 27, Rais Ruto asilimia 21, Kalonzo asilimia 10 na Matiang'i asilimia tisa. Asilimia 21 ya wakazi bado hawajafanya uamuzi. Katika eneo la Kusini Mashariki, Kalonzo ameendelea kutawala ngome yake kwa asilimia 58 dhidi ya asilimia 15 za Rais Ruto. Ni asilimia tisa pekee ambao hawajaamua. Magharibi mwa Kenya pia inaonekana kuwa eneo litakaloamua matokeo ya uchaguzi. Sifuna anaongoza kwa asilimia 28, Rais Ruto asilimia 14 na Matiang'i asilimia 12. Hata hivyo, asilimia 31 ya wakazi bado hawajafanya uamuzi. Kwa upande mwingine, Rais Ruto anaendelea kutawala Kaskazini mwa Kenya kwa asilimia 61 ya uungwaji mkono na bado ana nguvu katika baadhi ya maeneo ya Bonde la Ufa. Nyanza nayo inaendelea kuwa ngome ya upinzani, ingawa ushindani unaongezeka huku Matiang'i akipata asilimia 29 na Rais Ruto asilimia 30. Kwa mujibu wa Katiba, mgombea wa urais lazima apate zaidi ya asilimia 50 ya kura halali pamoja na angalau asilimia 25 ya kura katika zaidi ya nusu ya kaunti zote nchini. Kutokana na hali hiyo, TIFA inaeleza kuwa ushindi wa mwaka 2027 hautategemea tu ngome za kisiasa bali pia uwezo wa vyama kuwashawishi mamilioni ya wapiga kura ambao bado hawajaamua katika maeneo kama Mlima Kenya, Nairobi, Magharibi na Pwani. Utafiti huo unatarajiwa kuathiri mikakati ya kampeni za kisiasa, huku Kenya Kwanza na viongozi wa upinzani wakiongeza juhudi za kuvutia wapigakura katika maeneo hayo muhimu kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka ujao.
read moretaifaleo.nation.co.ke
@taifaleo 21 hours ago
KCPE, KCSE zafufua kumbukumbu za shule kwa Wakenya wanaoishi Uingereza
KWA Wakenya wengi, kumbukumbu za mitihani ya KCPE na KCSE huibua picha za usiku wa kukesha wakisoma, wasimamizi wakali wa mitihani na shinikizo kubwa la kufaulu. Lakini sasa, kile kilichokuwa chanzo cha hofu kimegeuzwa kuwa burudani inayowaleta pamoja Wakenya nchini na ughaibuni. Nchini Uingereza, jamii ya Wakenya imeanzisha usiku maalum wa maswali na majibu unaotumia maswali ya KCPE na KCSE kama njia ya kuburudika, kukumbushana maisha ya shule na kuimarisha urafiki. Miongoni mwa walioanzisha shughuli hiyo ni Nicholas Njomo Kamau, mtaalamu wa afya anayefanya kazi katika Huduma ya Kitaifa ya Afya ya Uingereza (NHS). Alivutiwa na hafla kama hizo zilizoandaliwa Nairobi na jumuiya ya ubunifu ya Qwani. "Niliona zinafanyika Kenya nikafikiria kwa nini tusizilete hapa, ambako kuna Wakenya wengi. Nimefurahishwa na zilivyopokolewa," alisema. Hafla hizo sasa zimefanyika mara tatu katika ukumbi wa Vaha Lounge mjini Northampton. Washiriki huwekwa katika makundi na kujibu maswali ya Hisabati, Kiingereza, Kiswahili, Sayansi na Masomo ya Jamii bila presha ya kufaulu. Kwa Njomo, uzuri wa wazo hilo ni kwamba karibu kila Mkenya amepitia mfumo wa elimu wa 8-4-4. "Sote tumewahi kupitia mitihani hiyo," alisema. Kilichoanza kama mkutano wa kujiburudisha sasa kimekuwa jukwaa la kujenga urafiki. Washiriki wameunda makundi ya WhatsApp na huendelea kuwasiliana hata baada ya hafla kuisha. Ingawa washindi hupata zawadi kama vile chupa za pombe, wengi husema zawadi kubwa ni kurejea kumbukumbu za utotoni, walimu waliowapenda, ushindani wa shule na maswali magumu yaliyowasumbua. Njomo alisema jambo lililomshangaza zaidi ni kuona hata Wakenya wa umri mkubwa wakijiunga na kufurahia hafla hizo. "Pia tumewaona watu wasiokuwa Wakenya wakija kudadisi. Huondoka wakifurahia muziki, ushindani na mazingira ya Kikenya," alisema huku akicheka. Baada ya maswali na majibu, hafla hubadilika kuwa sherehe ya nyimbo za zamani za Kenya. Wageni hufurahia ugali, nyama choma, pilau na mboga za kienyeji huku nyimbo za Gengetone na nyimbo za zamani zikichezwa. "Tunawaleta ma-DJ wa Kenya kucheza nyimbo zinazotukumbusha enzi za shule," alisema. Mwanafunzi wa uuguzi nchini Uingereza, Lynn Saina, alisema hafla hizo huwasaidia Wakenya kupunguza hamu ya nyumbani. "Kinachonivutia zaidi ni furaha na vicheko. Chumba kilichojaa wageni hubadilika haraka na kuwa familia moja kubwa," alisema. Aliongeza kuwa kati ya vipengele vinavyovutia zaidi ni maswali ya methali za Kiswahili, ambapo washiriki hujaribu kukamilisha methali lakini mara nyingi huishia kubuni methali mpya zinazochekesha kila mtu. Siku ya kwanza, hafla hiyo ilivutia zaidi ya watu 150 uliwathibitishia kuwa Wakenya walikuwa na hamu kubwa ya kumbukumbu zao za shule.
read moretaifaleo.nation.co.ke
@taifaleo 23 hours ago
Wanawake pia hutumika kueneza uhuni wa kisiasa-Utafiti
WANAWAKE wanazidi kuwa sehemu muhimu lakini isiyoonekana ya mitandao ya wahuni wa kisiasa nchini, huku wakitumika kuhamasisha vijana, kusafirisha silaha kwa siri na kukusanya taarifa za kisiri, utafiti mpya umebaini. Kwa miaka mingi, macho ya umma yamekuwa yakielekezwa kwa vijana wanaume wanaovamia mikutano ya kisiasa na maandamano wakiwa na rungu na mawe. Hata hivyo, ripoti mpya inaonyesha kuwa nyuma ya vurugu hizo kuna mtandao uliopangwa vyema unaowahusisha pia wanawake. Kijana mmoja kutoka Mathare, Nairobi, aliyekubali kuzungumza na Taifa Jumapili kwa masharti ya kutotajwa jina kwa hofu ya usalama wake, alisema wanawake wamekuwa sehemu ya mfumo huo. "Bila shaka wapo. Huenda wasiwe mstari wa mbele, lakini wanashiriki kikamilifu," alisema. Kijana huyo, anayejitambulisha kama mmoja wa "vigogo" wa eneo hilo wanaotafutwa na wanasiasa na wafanyabiashara kuwasaka vijana kwa shughuli za kisiasa, alisema hawabagui wanawake wanapofanya uajiri. "Sisi ndio viongozi wanaotafutwa na wanasiasa wanapohitaji watu. Hatujali jinsia. Tunawaajiri wanawake, nao pia huleta wengine," alisema. Kwa mujibu wake, wanawake mara nyingi hawashiriki moja kwa moja katika mashambulizi, bali hujichanganya na umati ili mikutano ionekane kuwa na watu wengi kuliko ilivyo. Pia hukusanya taarifa, huwatetea wenzao wanapokamatwa na wakati mwingine husafirisha mawe au silaha ndogo wanazofichwa kwenye mikoba yao. "Kama hujui utakula nini mchana au jioni, huwezi kuanza kuuliza kama mwanamke anafaa kujiunga na kundi au la," alisema. Hata hivyo, alisema hajawahi kuona mwanamke akifikia kiwango cha kuwa kiongozi mkuu wa mtandao huo, ingawa wengi hutumiwa kuajiri wengine. Ripoti inayoitwa Goonland: Looking Beyond the Money and Violence in the Political Exploitation of Young Men, iliyoandaliwa na shirika la OdipoDev, inaeleza kuwa magenge ya kisiasa si mkusanyiko wa vijana wasio na ajira pekee, bali ni mtandao wenye viongozi, waajiri, wajumbe na waratibu wanaofanya kazi kwa mpangilio maalumu. Utafiti huo ulifanywa kupitia mahojiano na wanachama 40 wa magenge ya wahuni, waajiri watano na maafisa watano wa usalama kutoka Nairobi, Mombasa na Kiambu. Ripoti hiyo inaonyesha kuwa mawasiliano hufanywa kupitia makundi ya WhatsApp na vituo vya mitaani, huku fedha na silaha zikisafirishwa kwa siri kupitia watu wanaoaminika. Wanawake ni miongoni mwa watu hao wanaoaminiwa kusafirisha na kuficha silaha kwa kuwa hawashukiwi kirahisi wakati wa ukaguzi kuhusu usalama. Mzee wa kijiji cha Mathare, Joseph Ouna, alisema akina mama wachanga wanazidi kuvutwa katika shughuli hizo kutokana na ugumu wa maisha. "Akina mama hawa wana watoto, na vijana hawa ni marafiki wao. Wanawapa pesa na kuwasaidia kwa mahitaji mbalimbali, hivyo huwa rahisi kuwashawishi wakubali kazi za kisiasa," alisema. Aidha, alisema baadhi ya wanawake hujitokeza kuwatetea vijana hao wanapokamatwa kwa kuwasawiri kama waathiriwa badala ya wahusika wa vurugu. Mratibu mmoja wa kisiasa kutoka Kayole ambaye hakutaka kutajwa jina alisema aliwahi kuombwa na mwanamke mwenzake amtafutie vijana kwa shughuli za kisiasa lakini alikataa kwa kuhofia kukamatwa au kushambuliwa. Alidai pia kuwa rafiki yake mmoja alipelekwa Ol Kalou kuvuruga uchaguzi mdogo uliofanyika eneo hilo. "Nilimshawishi asiende lakini alikataa. Hadi leo sijui alilipwa kiasi gani," alisema. Naibu Kamishna wa Kaunti Ndogo ya Nyandarua Central, Kenneth Kiprop, alisema hakuna mwanamke aliyekamatwa kufuatia vurugu za uchaguzi mdogo wa Ol Kalou, wala uchunguzi haukubaini wanawake walioshiriki moja kwa moja katika mashambulizi hayo. Utafiti huo unaonyesha kuwa fedha ndizo kichocheo kikuu cha vijana kujiunga na magenge hayo. Kuvuruga mikutano ya kisiasa hulipwa kati ya Sh500 na Sh1,500, shughuli za kuvuruga maandamano hulipa Sh500 hadi Sh2,500, huku migogoro ya ardhi ikilipa kati ya Sh500 na Sh2,000. Hata hivyo, watafiti wanasema si pesa pekee zinazowafanya vijana wabaki kwenye mitandao hiyo. Wengi walieleza kuwa hupata wanatambuliwa, kupata ulinzi, hadhi na hisia ya kuwa sehemu ya kundi. Ripoti hiyo inaonya kuwa kuanzisha nafasi za ajira pekee hakutamaliza tatizo la magenge ya kisiasa, kwa sababu wanaojiunga nayo hujengewa uhusiano unaotokana na hofu na mshikamano wa kijamii ambao si rahisi kuuvunja.
read moretaifaleo.nation.co.ke
@taifaleo Sat, 25 Jul 2026 22:55:05
Wantam: Sifuna aoshewa lami, apokelewa kishujaa Bungoma
KIFO cha aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga kimebadilisha kwa kiasi kikubwa mwelekeo wa siasa za Kenya, huku Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna akiibuka kama mmoja wa viongozi wanaotikisa hesabu za uchaguzi mkuu wa 2027. Baada ya kuondolewa kama Katibu Mkuu na msemaji wa ODM, Sifuna sasa anaongoza vuguvugu la Linda Mwananchi, ambalo wachambuzi wanasema linaweza kubadili kabisa sura ya siasa za nchi na kutatiza mipango ya serikali pamoja na upinzani. Ndani ya ODM, baadhi ya viongozi wanakiri kuwa kumuondoa Sifuna kutoka uongozi wa chama kulikuwa kosa kubwa. Hata hivyo, sasa anaongoza vuguvugu linalovutia wafuasi wengi, hasa vijana, na ambazo zinazidi kupata nguvu kote nchini. Umaarufu wake umewatia wasiwasi viongozi wa kisiasa wa Magharibi kama Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetang'ula na Mkuu wa Mawaziri Musalia Mudavadi, ambao wamekuwa wakijitambulisha kama vinara wa eneo hilo. Jana, Sifuna aliongoza mikutano mikubwa ya kisiasa katika Kaunti ya Trans Nzoia na kutangaza kuwa yuko tayari kuwania urais katika uchaguzi mkuu wa 2027. Akizungumza katika mkutano wa mwisho mjini Kitale, Sifuna alimshukuru Gavana wa Trans Nzoia George Natembeya kwa kumuunga mkono na kumhimiza azunguke nchi nzima kutafuta uungwaji mkono. "Nimekubali jukumu hilo. Niko tayari kuzunguka Kenya nzima kutafuta kura na sitawaangusha Wakenya," alisema. Sifuna alidai kuwa upinzani utaungana na kumteua mgombeaji mmoja wa urais atakayemenyana na Rais William Ruto katika uchaguzi ujao. Baada ya mikutano hiyo, msafara wa viongozi hao ulipitia Kaplamai na kusimama katika soko la Sibanga, Cherang'any, kabla ya kurejea Kitale kwa mkutano wa mwisho. Kwa mujibu wa utafiti wa hivi karibuni wa TIFA uliotolewa Ijumaa, Sifuna amempiku kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka katika umaarufu wa urais kwa mara ya kwanza. Katika utafiti huo, Sifuna alipata asilimia 15 ya uungwaji mkono, akifuatiwa na Naibu Kiongozi wa Jubilee Fred Matiang'i kwa asilimia 14, Kalonzo Musyoka asilimia 13, kiongozi wa DCP Rigathi Gachagua asilimia saba na Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino asilimia mbili. Kwa jumla, viongozi wa upinzani wanaungwa mkono na asilimia 51 ya Wakenya, huku Rais William Ruto akiongoza kivyake kwa asilimia 24. Hata hivyo, kiwango hicho bado hakitoshi kumwezesha kushinda uchaguzi katika duru ya kwanza. Kinachowashangaza wengi si tu umaarufu wa Sifuna bali kasi aliyopanda nayo. Miezi miwili iliyopita hakuwa hata akitajwa katika mazungumzo ya wagombeaji urais. Sasa ameibuka kama mmoja wa wanasiasa wenye ushawishi mkubwa zaidi nchini. Katika uchaguzi wa Seneti wa Nairobi mwaka 2022, Sifuna alimshinda Askofu Margaret Wanjiru kwa kura 716,876. Leo, umaarufu wake unatajwa kuwa unaweza kubadili mazungumzo ya muungano wa upinzani kuhusu mgombeaji mmoja wa urais. Hata baada ya kuondolewa katika uongozi wa ODM, utafiti unaonyesha karibu nusu ya wafuasi wa chama hicho wangependa awe mgombeaji wao wa urais. Matokeo hayo yanaendana na utafiti wa awali wa Infotrak uliomuonyesha Sifuna akipunguza pengo kati yake na viongozi waliokuwa wakitajwa kama vigogo wa upinzani, jambo linaloashiria kuwa kupanda kwake si bahati bali ni mwelekeo mpya wa kisiasa. Akizungumza baada ya matokeo ya utafiti huo kutolewa, Sifuna alisema jambo muhimu si asilimia aliyopata, bali ni kwamba Rais Ruto anaendelea kushuka chini ya kiwango kinachohitajika kushinda uchaguzi kwa urahisi. Alisema iwapo upinzani utaungana nyuma ya mgombeaji mmoja, utaweza kumshinda Rais Ruto. "Tukijumlisha asilimia za Sifuna, Kalonzo, Matiang'i na viongozi wengine wa upinzani, ziko juu zaidi ya za Rais Ruto. Tunahitaji umoja ili kuwasikiliza Wakenya wanaotaka mabadiliko," alisema. Mchambuzi wa siasa Arnold Maliba alisema wengi wanakosea kuchukulia Linda Mwananchi kama muungano wa kawaida wa kisiasa. Kwa mujibu wake, vuguvugu hilo linalenga kubadili mjadala wa kisiasa kutoka ukabila na makubaliano ya viongozi kuelekea masuala ya utawala bora, uwajibikaji, Katiba na ushiriki wa wananchi. "Linda Mwananchi si chama cha kawaida. Ni vuguvugu linaloweka shinikizo kwa serikali na pia kwa upinzani uliopo," alisema. Kwa Rais Ruto, kupanda kwa Sifuna kunamaanisha hatari ya kupoteza kura za eneo la Magharibi, ambazo ni muhimu katika azma yake ya kutetea urais, hasa baada ya kupoteza uungwaji mkono mkubwa katika Mlima Kenya. Ndani ya upinzani, kuibuka kwa Sifuna kumebadili hesabu zilizoweka Kalonzo Musyoka na Fred Matiang'i kama wagombeaji wakuu wa urais.
read moretaifaleo.nation.co.ke
@taifaleo Sat, 25 Jul 2026 23:55:46
Gachagua aapa kuzima njama za kuleta mgawanyiko Mlimani
KIONGOZI wa chama cha Democracy for Citizens Party (DCP), Rigathi Gachagua, ameapa kupinga kile alichokitaja kama njama za Rais William Ruto kugawanya eneo la Mlima Kenya kabla ya Uchaguzi Mkuu wa 2027. Akizungumza katika mikutano ya hadhara mjini Embu, Kathangariri, Karurumo, Gategi na Siakago Jumamosi, Gachagua alimshutumu Rais Ruto kwa kutumia Waziri wa Utumishi wa Umma Geoffrey Ruku kuendeleza mpango wa kugawanya eneo hilo kuwa Mlima Kenya Mashariki na Magharibi. "Lazima nimzuie Ruto kugawanya Mlima Kenya. Tunataka tubaki pamoja ili tumpeleke nyumbani katika uchaguzi ujao," alisema Gachagua katika soko la Kathangariri, Embu. Alidai Rais Ruto amewasaliti wakazi wa Mlima Kenya waliomuunga mkono kwa wingi 2022 kwa kuwaita wakabila. Pia alimshutumu Rais kwa madai ya kuruhusu makundi ya wahuni kuwashambulia wakazi wa Mlima Kenya na kuharibu mali yao. "Nitahakikisha Ruto anakuwa rais wa muhula mmoja. Kilichotokea Ol Kalou kitajirudia katika Mlima Kenya mzima," alisema. Gachagua pia alimkosoa Waziri wa Afya Aden Duale kwa madai ya kutoa matamshi ya kuwadhalilisha wakazi wa Mlima Kenya, akisema atawajibishwa kisiasa katika uchaguzi ujao.
read moretaifaleo.nation.co.ke
@taifaleo Sat, 25 Jul 2026 13:55:35
Kavulani amwonya Asefa, aapa kumlaza mapema kwenye pambano Ndondi
Bondia wa Kenya Jane Kavulani ametuma onyo kali kwa mpinzani wake Roman Asefa Abate wa Ethiopia akiahidi kumwangusha kwa kushinda kwa 'Knockout' yaani KO katika raundi za kwanza, watakapokutana katika mashindano ya ndondi yatakayofanyika Jumamosi hii kwenye ukumbi wa Edge Convention Centre jijini Nairobi. Kavulani, anayefanya mazoezi katika ukumbi wa Pal Pal Gymnasium uliopo Gikomba jijini Nairobi, alisema amejiandaa vya kutosha na hana shaka ya kuibuka mshindi dhidi ya Methiopia huyo ambaye atakuwa akicheza pambano lake la kwanza la kulipwa. "Nimefanya maandalizi ya kutosha. Lengo langu ni kumaliza pambano mapema kwa KO na kuwapa mashabiki ushindi wa kujivunia," alisema Kavulani. Hata hivyo, Asefa naye ameonyesha kujiamini akisema ananuia kuanza maisha yake ya ndondi za kulipwa kwa ushindi na kurejea Ethiopia akiwa ameshinda pambano lake la kwanza. Zaidi ya mapambano hayo ya wanawake uzani wa featherweight, mashabiki watashuhudia jumla ya mapambano 11 kwenye usiku huo wa ngumi uliofadhiliwa na SportPesa na kuandaliwa na promota Maurice Odera kupitia kampuni ya UFS BXNG. Pambano kuu la usiku litamshuhudia bingwa wa Kenya na Afrika Mashariki Javan Buyu akipambana na Ramadhani Idd wa Tanzania kuwania taji la Universal Boxing Organisation (UBO) Inter-Continental Lightweight katika pambano la raundi 10. Buyu anatarajiwa kutumia uzoefu wake mbele ya mashabiki wa nyumbani huku Idd akinuia kuvuruga mipango ya Mkenya huyo kwa kutwaa taji hilo na kuliondoka nalo Tanzania. Buyu, ambaye ni bingwa wa Kenya na Afrika Mashariki, ana nafasi ya kutwaa taji lake la tatu la kulipwa na kuwa miongoni mwa mabondia wachache wa Kenya kushinda mkanda wa ngazi ya mabara. Bondia huyo amesema yuko tayari kwa mtihani huo baada ya kufanya maandalizi ya miezi mitatu bila kuacha jambo lolote kwa bahati. "Nimekuwa nikifanya mazoezi na kumuomba Mungu kwa ajili ya taji hili. Mimi na timu yangu tumefanya kazi kubwa kujiandaa kwa Julai 25 na tuko tayari. Tumeimarisha kila eneo muhimu litakalotupa ushindi," alisema Buyu. Buyu alitwaa ubingwa wa Kenya Oktoba mwaka jana baada ya kumshinda Christopher Osicho kabla ya kuongeza mkanda wa PST kwa kumcharaza Mtanzania Nasoro Madimba kwa Technical Knockout katika raundi ya tatu mapema mwaka huu. Amesema tayari amemchunguza Ramadhani kupitia video zake. "Ni bondia mzuri, ningempa alama saba kati ya 10, lakini nina kila kitu kinachohitajika kumlazimisha akate tamaa. Namwahidi pambano zuri, lakini aandae moyo wa kukubali kushindwa," alisema.
read moretaifaleo.nation.co.ke
@taifaleo Sat, 25 Jul 2026 10:22:43
Wetang'ula: Ukabila hauna nafasi katika siasa za Kenya
Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetang'ula amewataka viongozi wa kisiasa kuachana na siasa za ukabila na kuhubiri umoja wa kitaifa, akionya kuwa matamshi ya chuki yanaweza kugawanya taifa kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2027. Akizungumza Jumamosi katika eneo la Oloiborsoito, Kilgoris, Kaunti ya Narok, wakati wa hafla ya kuchangia fedha Shirika la Wanawake la Olerai, Wetang'ula alisema tofauti za kisiasa hazipaswi kugeuka kuwa chuki, vurugu au uhasama wa kikabila. "Mtu yeyote anayehubiri ukabila ana fikra za zamani. Tunaweza kutofautiana kisiasa, lakini hiyo si sababu ya kutukanana au kuumizana," alisema. Aliwataka wanasiasa kuepuka matamshi ya uchochezi yanayoweza kuwashawishi vijana kuingia katika vurugu, akisisitiza kuwa viongozi wana wajibu wa kuimarisha amani na mshikamano wa kitaifa. "Siasa hazipaswi kuwa sababu ya umwagaji damu. Vijana ni mustakabali wa taifa na hawapaswi kutumiwa katika migogoro ya kisiasa," alisema. Wetang'ula alisema kuwawezesha wanawake na vijana kupitia ujuzi na fursa za kiuchumi ni muhimu kwa maendeleo ya taifa. Pia alisifu jamii ya Wamaasai kwa kuhifadhi utamaduni wao, akisema umechangia kukuza utalii nchini. Spika huyo alimkosoa aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua kwa madai ya kutoa matamshi yanayoweza kudhoofisha sekta ya utalii, huku akitoa wito wa kutungwa kwa sheria zitakazolinda wachimbaji madini na kuwawezesha kunufaika na rasilimali za taifa. Katika hafla hiyo, mshauri wa Rais William Ruto, Farouk Kibet, aliwataka wakazi wa Kilgoris kuishi kwa amani, huku Kiongozi wa Wengi katika Seneti Aaron Cheruiyot akilaani siasa za ukabila na kuitaka Wizara ya Usalama kuchukua hatua dhidi ya viongozi wanaotoa matamshi ya uchochezi. Mbunge wa Kitutu Chache North Japheth Nyakundi aliwataka viongozi kuzingatia sera za maendeleo badala ya siasa za kikabila, huku Mbunge wa Kibwezi West Mwengi Mutuse akitetea rekodi ya maendeleo ya serikali ya Rais William Ruto.
read moreRight Column Content